Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi yake ya uhai, pia nimpongeze Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hasssan kwa kazi nzuri ambayo ameendelea kuifanya wote tunaiona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI pamoja na Wasaidizi wake wote kwa kazi nzuri ambazo wamekuwa wakizifanya nasi tutawapa ushirikiano, tunaomba tu yale ambayo tutakuwa tunajadiliana basi ya ninyi mpate kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania hii tunaona kabisa maeneo mengi ya pembezoni, Halmashauri za pembezoni Tanzania nzima zina upungufu mkubwa sana wa watumishi ukilinganisha na maeneo mengine, Serikali inaenda kuajiri Sekta ya afya na elimu watumishi 21,000, ombi langu kwa TAMISEMI pamoja na afya ni kuona kwamba tupange idadi ya watumishi hawa kulingana na uhitaji wa maeneo husika, siyo kusambaza tu kwasababu kila mmoja apate, kuna maeneo hali ni mbaya huduma haziendi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka wa fedha 2021/2022 na 2022/2023 Halmashauri ya Wilaya ya Newala imepokea zaidi ya Bilioni 8.5, nini matarajio ya wananchi? Matarajio ya wananchi ni kuona kwamba thamani ya fedha iliyotolewa inafanana au inaenda sambamba na huduma inayopatikana katika maeneo husika, hilo ndiyo tarajio kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo changamoto ambayo inazifanya Halmashauri zetu zishindwe kufikia katika utoaji wa huduma iliyo bora. Mfano, ukienda kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Newala, upande wa afya watumishi mahitaji ni 526 waliopo ni 172 upungufu ni 354, hali ambayo inaleta malalamiko kati ya watoa huduma na wahudumiwa, kwa sababu kunakuwa na msuguano wale wahudumiwa wanaona hawafanyiwi ipasavyo lakini wakati mwingine ni kutokana na uchache wa watumishi waliopo, wanashindwa namna ya kujigawa ili waweze kutoa huduma ipasavyo. Kwa hiyo, niombe sana watumishi wa kada ya afya wapelekwe kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Newala ili wakaweze kutoa huduma kwa wananchi kulingana na fedha ambazo Mheshimiwa Rais pamoja na Serikali imekuwa ikizitoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda elimu - Elimu ya msingi upungufu wa walimu ni 327 kwenye uhitaji wa 787. Kwa hiyo, unaona kwamba walimu waliopo msingi wanapata kazi kubwa sana, mzigo ni mkubwa wa ufundishaji na ikumbukwe kwamba mwalimu ili akafundishe lazima aandae somo, sasa Mwalimu huyu anafundisha Darasa la Kwanza, Darasa la Pili mpaka Darasa la Saba anawezaje kuandaa masomo yote, vipindi vyote ili akaweze kufanyakazi inayostahili. Kwa hiyo, tuangalie kwa jicho la pekee namna ambavyo upungufu huu unaathiri utoaji wa elimu iliyo bora kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekondari pia hali ni hiyo hiyo. Mzigo wa walimu ni mkubwa, mwalimu anafundisha Biology kuanzia kidato cha kwanza, cha pili, cha tatu cha nne. Fikiria mzigo ambao anaubeba, hajasahihisha bado, ukiacha kuandaa lazima asahihishe aone kazi ambayo imefanywa na mwanafunzi kama inaendana na kile ambacho amekifundisha, kwa hiyo unakuta mzigo anaobeba ni mkubwa kuliko hali halisi, kuliko uwezo wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikitoa fedha zile za elimu bila ada, inapeleka kwa wanafunzi hawa kuanzia darasa la kwanza mpaka kidato cha sita sasa. Lakini kwa sababu ya hali ya upungufu wa walimu uliyopo inalazimika jamii kutafuta walimu wa kwao ili wakawafundishe watoto wao ku - cover lile gap, lakini wale wanaowafundisha hawatoki mikono mitupu lazima wazazi wachangishane, wawalipe walimu wale. Sasa katika mazingira hayo unakuta wazazi wanalalamika kwamba tunabebeshwa mzigo mkubwa na kwamba ile fedha ambayo tunaipeleka hawaioni ile thamani yake kwa sababu tu ya uhaba wa watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama watumishi wa kada ya ualimu wangekuwepo wala hilo gap lisingeonekana. Niombe sana tupeleke walimu katika Halmashauri hizi za pembezoni. Pia tunao Maafisa Maendeleo ya Jamii wa Kata, Jimbo la Newala Vijijini lina Kata 22 lakini ina Maafisa Maendeleo ya Jamii Wanne tu. Maafisa Maendeleo ya Jamii hawa ndiyo ambao wanaenda kusimamia zile fedha asilimia 10 inayoenda kwenye Halmashauri, kama hawapo nani atasimamia, matokeo yake fedha zinashindwa kurudishwa kwa sababu hakuna ufatiliaji.

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, labda…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Maimuna Mtanda kwa mchango wako.

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)