Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa mchango wangu kwenye hotuba ya bajeti ya Wizara hii muhimu sana kwa maisha ya Watanzania. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya. Hakika Mheshimiwa Rais katika wakati wake ameonesha namna nzuri na namna bora ya kuzilea na kuzisaidia Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuteuliwa kuwa Waziri kwenye Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mchango kwenye maeneo machache. Eneo la kwanza ni eneo lenyewe la Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 145 (1), inaeleza kuwepo kwa vyombo mbalimbali kwenye maeneo ya Serikali za Mitaa. Vile vile ibara ya 146 (1) inaeleza madhumuni ya kuwepo kwa Serikali za Mitaa ikiwa ni kurudisha madaraka kwa wananchi na vyombo hivi viweze kuwashirikisha wananchi. Sasa sisi Tanzania kwenye mfumo wa Serikali za Mitaa tume-buy mfumo wa wenzetu wa British mode. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye British mode, moja ya tabia yake ni kuwa na double accountability. Kwa maana watendaji wetu wanakuwa accountable kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa, lakini at the same time wanakuwa accountable kwenye Serikali Kuu. Kwenye mazingira ya namna hii, kama kusipokuwa na proper coordination, lazima kutakuwa na kigongano kati ya mamlaka hizi mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ombi langu kwa TAMISEMI, mwaka 2019 tulianza mapitio ya kuboresha sera ya ugatuaji wa madaraka, lakini mpaka leo kumekuwa na ukimya. Mheshimiwa Waziri ukija kwenye majumuisho utuambie, tumefikia wapi kwenye zoezi la kuboresha Sera ya Ugatuaji wa Madaraka? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, kwa sababu, tayari kuna double accountability, ni lazima wenzetu wa Serikali Kuu wakubali kuwa flexible ili kuweza kuchukua mawazo ya wananchi katika kutekeleza ile azma ya kurudisha madaraka kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba wenzetu wa TAMISEMI, mnafanya vitu vizuri, lakini kuna maeneo ambayo hamtutendei haki. Serikali za Mitaa siyo za kupokea tu maelekezo, lazima zishirikishwe; na katika kushirikisha lazima muwe flexible kusikiliza na mawazo ya waliokuwa chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano wanataka kujenga masoko, unatoa mfumo mmoja wa kujenga masoko nchi nzima. Aliyekwambia Soko la Korogwe linafanana na Soko la Sumbawanga ni nani? Aliyekwambia jiografia ya Korogwe na ya Sumbawanga inafanana ni nani? Haiwezekani, lazima tuangalie mazingira halisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, tumemsikia Mheshimiwa Rais akisema mara kadhaa kwamba, kugawa maeneo ya utawala ni gharama kubwa. Nami nakubaliana naye, lakini moja ya chombo muhimu kwenye Serikali za Mitaa ni mamlaka ya kwenye Kijiji kwa maana ya Halmashauri ya Kijiji na Mkutano wa Kijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunaotoka vijijini, vijiji vinakua. Ukiwaona maeneo mawili tofauti kwa vijiji yamekua, yanaanza kuwa na msigano, na shughuli za maendeleo hazifanyiki vizuri. Tunaomba mumshauri Mheshimiwa Rais, kuna gharama kubwa kutangaza mikoa mipya, kutengeneza Halmashauri mpya, lakini hata kutengeneza vijiji! Hakuwezi kuwa na gharama kubwa namna hiyo! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vijiji vimekuwa ni vikubwa, vinahitaji kugawanywa ili wananchi wasogezewe huduma karibu na waweze kufanya shughuli za maendeleo. Kule Korogwe Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuja na aliahidi kwamba atatoa vijiji vipya, lakini mpaka leo kumekuwa na ukimya. Tunaomba muishauri mamlaka ili mambo yaweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni vituo vya afya. Sera yetu inasema tuwe na vituo vya afya kila Kata, tuwe na zahanati kila Kijiji. Tukaona utekelezaji wake umekuwa mgumu tukasema, tuwe na vituo vya afya vya kimkakati na vya Tarafa. Nimeahidiwa vituo vya kimkakati tangu mwaka 2020 hapa, mpaka leo sijaona hata kimoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri alipoingia tu kwenye Wizara ametuita, amekaa vikao na Wabunge, yale tuliyoyasema siyaoni yakiwa reflected kwenye bajeti hii. Vituo hivi tunavipata lini? Vinajengwa wakati gani? Tumewaahidi wananchi, tunakwenda kwenye uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kwenye mikopo ya akinamama, vijana na watu wenye ulemavu ya asilimia 10. Ninaungana kabisa na alichokisema Mheshimiwa Rais. Pia nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa mawazo na maelekezo aliyoyatoa jana. Naomba niwashauri, mnapoenda kutekeleza maelekezo ya Mheshimiwa Rais, muongeze. Tukipeleka fedha hizi kwenye mfumo wa kibenki, tutafanikiwa kwenye lengo moja la kuhakikisha tunakuwa na utaratibu mzuri wa utoaji na urejeshaji, lakini bado hatutakuwa na utaratibu mzuri wa kuziwezesha jamii zetu kubaki na matokeo baada ya kumaliza kufanya mrejesho wa hiyo mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna haja ya TAMISEMI kutoa maelekezo kuziunganisha idara; Idara ya Maendeleo ya Jamii, Idara ya Kilimo, Idara ya Mifugo, Idara ya Biashara, ili mikopo hii inapotolewa, itolewe kulingana na mazingira halisi ya biashara kwenye maeneo yale, ili baada ya kumaliza kurejesha marejesho ya mkopo huu, wananchi hawa waone biashara hizi zikiendelea, tuone matokeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotusumbua sasa hivi kwenye kurejesha pia, hakuna mipango mizuri na elimu nzuri ya kuzitumia hizi fedha. Tukiziunganisha idara hizi; Idara ya Kilimo, Idara ya Mifugo, Idara ya Maendeleo ya Jamii, tutafanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, nikuombe sana Mheshimiwa…

(Hapa kengele ililia kushiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa nakuongezea dakika moja umalize jambo la mwisho.

MHE. TIMOTEHO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, naipongeza Serikali kwa ajira ambazo imetangaza. Ukisoma ripoti ya CAG, alifanya tathmini kwenye Halmashauri 23 tu, lakini upungufu ulikuwa ni asilimia 35, karibia watumishi 10,000 kwenye Idara ya Elimu peke yake. Hawa walimu 13,000 wanakwenda kuishia kwenye hizo Halmashauri 23 tu. Tuna Halmashauri 184. Tukifanya tathmini kwa nchi nzima, upungufu huu ni mkubwa sana kwa watumishi wa elimu na watumishi wa afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ajira hizi, bado hazitoshi. Tunaomba wekeni mikakati zaidi ili tupeleke watumishi kwenye maeneo yetu, lakini siyo kuajiri tu wapya, vile vile na mlinganisho na msawazo wa watumishi hasa kati ya Halmashauri za Mijini na Halmashauri za Vijijini. Halmashauri za Vijijini zimechoka kuwa sehemu za watu kupatia ajira na kuondoka kwenda kukaa maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naunga mkono hoja. (Makofi)