Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa na mimi niweze kuchangia hoja iliyopo mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya. Pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri na timu yake yote na wenyewe kwa kazi kubwa wanayoifanya kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kutekeleza maono yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo napenda kuchangia ni kuhusiana na masuala ya usimamizi wa fedha katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Sisi sote ni mashahidi na tunafahamu kwamba katika vihatarishi vikubwa vya kufikia malengo na utekelezaji wa mpango wa maendeleo ni kukosekana kwa rasilimali fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi. Sisi wote ni mashahidi wa jitihada kubwa anazozifanya Mheshimiwa Rais katika kutafuta pesa nyingi kwa ajili ya kuchochea maendeleo na utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tunaweza tukaona kwamba kuna fedha zile za TCRP, fedha za UVIKO ambazo zimekuja na zimechochea kwa kiwango kikubwa maendeleo katika sekta za afya, elimu, maji pamoja na wajasiriamali wadogo na tumeona kwamba kwa mfano Wamachinga wanajengewa masoko. Sasa hizi ni jitihada kubwa sana ambazo zinafanywa na Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hizi tu, mfano mwingine kuna hizi pesa za ECF (Extended Credit Facility) ambazo na zenyewe zimeelekezwa kwenye sekta za uzalishaji. Kwa mfano sekta za kilimo, nishati, mifugo na uvuvi; hizi zote ni jitihada ambazo Mheshimiwa Rais anazifanya za makusudi ili kuhakikisha anachochea maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili fedha hizi ziwe na tija kuna haja kubwa sana ya kudhibiti upotevu wa fedha hizi katika utekelezaji wa miradi. Natambua jitihada za Wizara, kwanza katika kusimamia halmashauri katika ukusanyaji wa mapato ya ndani, lakini pia katika jitihada za kudhibiti mianya ya kuvuja kwa pesa hizo na kudhibiti matumizi ya fedha hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna changamoto ya matumizi ya fedha mbichi kwenye halmashauri zetu. Namna pekee au nzuri ya kukabiliana na changamoto hii ni kutengeneza utaratibu wa kutoa mkono wa binadamu katika ukusanyaji wa mapato na ili kutimiza lengo hilo au katika utekelezaji wa lengo hilo, kutengeneza mifumo thabiti ya TEHAMA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali kwa sababu imetengeneza mifumo ya TEHAMA, kuna Mfumo wa TAUSI, kuna Mfumo wa MUSE, kuna Mfumo wa POS, yote hii ni mifumo ya TEHAMA ambayo inakwenda kuondoa na ikisimamiwa vizuri itaondoa kabisa changamoto ya upotevu wa makusanyo, upotevu wa rasilimali fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili mifumo hii iwe na tija, kwanza lazima kuwe na mtandao (connectivity) kwa sababu matumizi ya TEHAMA yanahitaji mtandao wa uhakika. Sasa kama kukiwa kuna changamoto ya mtandao ina maana mifumo hii haitakuwa na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kama huu Mfumo wa MUSE ambao ni mfumo wa uhasibu Serikalini ambao unawezesha Maafisa Masuuli kukusanya au kufunga mahesabu ya mwaka kwenye mtandao na uzuri wa mfumo huu ni kwamba zile nyaraka za malipo zinakuwa zinaambatishwa au zinawekwa kwenye mfumo, kwa hiyo inaondoa ile changamoto ya upotevu wa nyaraka ambayo mara nyingi ndiyo hoja za ukaguzi. Anapokuja CAG kufanya ukaguzi hoja nyingi zinatokana na upotevu wa nyaraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mifumo hii ni mizuri.kwa mfano kuna huu Mfumo wa TAUSI ambao mteja anaweza kujihudumia yeye mwenyewe kwenye mtandao, kwa maana ya kuomba kwa mfano kama vibali vya ujenzi au tuseme kulipia viwanja vile ambavyo vinapimwa na halmashauri au kuomba leseni za biashara. Kwa hiyo ili mifumo hii iweze kuwa na tija na tuweze kudhibiti mianya ya upotevu wa hizi fedha nyingi ambazo zinatafutwa na Mheshimiwa Rais kwa ajili ya maendeleo, ni lazima kuhakikisha kwamba mifumo inakuwa thabiti na kwamba kunakuwa na mtandao wa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Mheshimiwa Mbunge mmoja amechangia amesema kuangalia mifumo iwe airtight, kusiwe kuna loophole yoyote ya upotevu wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo napenda kuchangia, ni suala la asilimia kumi ile ya mapato ya ndani ambayo inakwenda kwa ajili ya kuwawezesha kimtaji vijana, wanawake pamoja na watu wenye ulemavu. Napongeza sana Serikali na Wizara kwa sababu walibuni ule mfumo wa TEHAMA ambao unaitwa Ten Percent Loan Management Information System ambao uliwezesha waombaji wa mikopo hii wafanye maombi hayo kupitia mfumo wa TEHAMA na mchakato ufanyike kupitia TEHAMA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizi bado kumekuwa na changamoto kwa sababu vikundi visivyostahili vimeendelea kupewa hii mikopo, lakini urejeshwa wa mikopo bado umeendelea kuwa ni changamoto. Sisi sote tumesikia maelekezo ya Mheshimiwa Rais ambaye amesema sasa fedha hizi ziende kutolewa kupitia taasisi za kifedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu katika kuboresha au tuseme katika utekelezaji wa agizo la Mheshimiwa Rais, suala la kwanza, taasisi za fedha ambazo tutazipa kazi ya kusimamia Mfuko huu, Wizara iangalie kwamba zile gharama za usimamizi (management fee) au zile commissions za hizi taasisi zisitokane na Mfuko wenyewe zikaenda kupunguza mtaji kwenye Mfuko ule na Serikali iangalie chanzo kingine cha kulipa hiyo gharama ya management fee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, programu hii ya kuwezesha kimtaji vijana, wanawale na watu wenye ulemavu ni programu nzuri, lakini kuna component moja ambayo ni muhimu sana; kuwajengea uwezo hawa wanufaika wa Mfuko huu ili waweze kuanzisha na kuendeleza biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuweza kufanikiwa mfuko huu ni lazima kutenga fungu au kutengeneza programu maalum kwa ajili ya capacity building, kutoa mafunzo ya msingi ya namna ya kuanzisha na kuendeleza biashara na kutoa pia msaada wa kitaalam (technical assistance).

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu, ni kuvilea vikundi hivi kibiashara, kwa sababu kazi kubwa wanayoifanya hawa maafisa wetu wanaokwenda kufuatilia hivi vikundi ni kufuatilia marejesho, lakini hakuna mtu anayekwenda kufanya mentorship kwa hivi vikundi ili viweze kusimama viwe vina biashara endelevu ambazo zitaweza kuajiri vijana, wanawake na watu wengine wengi zaidi, lakini ambavyo vitaweza kuwa na multiplier effect kwenye uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo katika mpango wa muda mrefu, naomba Serikali yote itengeneze utaratibu mzuri kwenye mitaala ya elimu, wanafunzi wanapokuwa wanasoma wapewe mafunzo ya msingi ya namna ya kuanzisha na kuendeleza biashara.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Zainab Katimba.

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema machache hayo, naunga mkono hoja na nashukuru sana. (Makofi)