Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa. Nianze moja kwa moja kwa kumpongeza sana Waziri wetu, Mheshimiwa Angellah Kairuki na wasaidizi wake wawili, Mheshimiwa Dkt. Dugange na Mheshimiwa Ndejembi na Mkuu wangu wa Mkoa wa Kilimanjaro na Mkuu wangu wa Wilaya Makori Kisare na DED wangu, kwa kazi nzuri wanayoifanya katika Jimbo langu la Moshi Vijijini. Ukweli watatutendea haki na tunashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TAMISEMI ni Wizara mama ambayo ni muhimu sana kwenye maendeleo ya watu wetu, kwa sababu utaona bajeti yake imeongezeka kutoka trilioni
8.7 mpaka trilioni 9.0, karibu asilimia 20 ya bajeti yetu ya Taifa. Ni kutokana na umuhimu wa hii Wizara. Kwa hiyo niwaombe waende wakasimamie hii Wizara vizuri ili hizi fedha zinazotolewa na Rais wetu zitumike vizuri na ziletee wananchi wetu maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Rais haraka sana; kwamba mama anaupiga mwingi, ametusaidia sana kwenye kuboresha ajira. Tumeona juzi ametoa ajira 21,200. Miundombinu ya afya ni nchi nzima kuanzia hospitali za rufaa, za mkoa, za wilaya, vituo vya afya, zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukija kwenye elimu; Mama amefanya makubwa sana, madarasa usiseme kitu, nami nimepata hospitali ya wilaya kule, kwa hiyo tunashukuru sana. Mambo ni mengi ambayo Mama amefanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kutokana na muda, naona leo umebana sana, hivyo, niende moja kwa moja kwenye mchango wangu. Katika mchango wangu ntaongelea tatizo la miundombinu ya barabara Jimboni kwangu Moshi Vijijini na pia ntaongelea mambo ya afya kama muda utaruhusu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Moshi Vijijini changamoto yetu kubwa ni barabara, ndiyo changamoto kubwa na kule Moshi Vijijini tuna bahati nzuri kwamba tuko milimani na mvua huwa zinanyesha. Hii mvua ni agent mkubwa wa kuharibu barabara zetu kule Moshi Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano, tunaishukuru Serikali kupitia TARURA walitutengenezea barabara nyingi, Barabara ya Gate Fonga - Mabogini mpaka Kahe; Barabara ya Boro – Sangiti; Barabara ya Kiboriloni kwenda Mbokomu; Barabara ya Mandaka – Mnono; Barabara ya Uru Madukani – Materuni; Barabara ya Mweka Junction – Singa Hospitali; Barabara ya Samanga – Chemchem. Nina masikitiko kidogo, barabara hizi zimejengwa kwa kiwango cha chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakandarasi ambao wamepewa pesa nyingi kutengeneza hizi barabara kuacha ile ya Samanga – Chemchem, barabara hizi zipo kwenye kiwango cha chini kabisa. Kitu kikubwa ambacho kimetokea nilivyosema mvua ni agent wa kuharibu barabara, ni kwamba hakuna mitaro. Barabara zimejengwa, zimechongwa vizuri, wameweka moramu. Kwa mfano ile ya Mabogini, tumewekeza shilingi milioni mia tatu na hamsini na kitu pale, lakini hata kabla haijaanza kutumika mvua ilivyonyesha imesafisha ile moram yote kwa sababu hatukuweka mitaro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe huu ujenzi ambao umefanyika nimwombe Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake, Engineer Seif, hii itawaharibia. Fedha za Serikali zinatumika vibaya na haijakaa vizuri. Tuwatumie ma- Internal Auditors wa kwetu wa Wizarani waende wakakague hizi barabara, siyo za kwenye jimbo langu tu, naona Wabunge wengi wanalalamika kwamba barabara hazijajengwa kwa viwango. Tutumie Internal Auditors wa TAMISEMI au ikibidi pia CAG aende kule aangalie, akague aone kama zile hela zimetumika vizuri. Ombi langu ni hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina ombi lingine; katika barabara inayokwenda kwenye Kijiji cha Chemchem kupitia Samanga kule Jimbo la Moshi Vijijini, Kata ya Arusha Chini, tulikuwa tumeomba kujengewa daraja linalounganisha hivi vijiji viwili kupita pale Mto Ronga. Bahati mbaya hela zilikuwa ndogo tulitengewa shilingi milioni 475, na pesa hizi zimetumika kutengeneza ile barabara, lakini lile daraja bado haliko kwenye mpango. Kwa hiyo nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, ikimpendeza tunaomba lile daraja litengenezwe ili tuweze kuunganisha Vijiji vyetu vya Chemchem na Samanga ili watu waweze kupita na kwenda kufanya shughuli za uzalishaji kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu la pili, ni kuhusu kuiongezea TARURA fedha. Kama nilivyosema Jimbo la Moshi Vijijini tuna tatizo kubwa la barabara. Yaani sisi changamoto yetu kubwa ni barabara. Na kuna barabara nyingi ambazo hazijatengenezwa. Niombe kwenye zile hela za tozo, mimi sijatendewa haki pia kwenye hizi hela za tozo; mwanzo ule mgao wa kwanza ulikuwa sawasawa, lakini huu mgao wa pili nimepata shilingi milioni 700 tu na wengine wamepata bilioni moja, bilioni ngapi. Kwa hiyo niombe zile pesa za tozo tuzigawe vizuri ili niweze kufanya ukarabati wa barabara ambazo nitazitaja hapa kwenye jimbo langu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ambazo ziko kwenye mfumo wa TARURA na hali ni mbaya. Barabara inayotoka pale Weruweru Sekondari kupanda Manushi mpaka pale Mrama Estate; barabara ya kule Mabogini eneo la Shabaha kwenda Newland; barabara ya kule Bonite Relini kwenda Chekereni, Weruweru; barabara ya Kisawio – Uru Seminari – Molangi; hizi ni barabara muhimu chache tu pamoja na nyinginezo. Naomba chonde chonde tusaidiane ili wananchi katika maeneo haya waweze kutengenezewa hizi barabara na wapite.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu la tatu ni ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami. Kuna barabara ambazo zilikuwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi mara tatu, nne, lakini bado hazijakamilika. Kule Moshi wanatuangalia wanasema tusipojengewa hizi barabara kama mlivyoahidi kwenye Ilani yenu ya Chama cha Mapinduzi tutakuwa kwenye matatizo makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe, barabara ya Gate Fonga – Mabogini – Kahe iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, hii ni mara ya tatu haijatengenezwa. Tunaomba Wizara iitengee pesa itengenezwe kwa kiwango cha lami kwani kule ndiko inakojengwa hospitali ya wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya pili, ni Barabara ya Uru – Mamboleo – Materuni na Uru – Mamboleo – Shingwe; ziko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, zimejengwa kwa mita 300, 400 tu. Niombe sana watufikirie na hizo barabara zijengwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara nyingine ni ile ya Kibosho Shine…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Profesa, muda wako umekwisha. Unga mkono hoja.

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)