Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwanza nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutupa uzima lakini pili nami niungane na wenzangu na Watanzania wengi kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa na jitihada ambayo anaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika niipongeze Waziri hii chini ya kiongozi wetu Mama Angellah Kairuki, kwa kazi kubwa inayofanywa. Kwa sababu Wizara hii ni Wizara ambayo ni kuunganisha cha Wizara nyingine ambazo kama Wizara ya Afya, hata Wizara za Ujenzi. Unakuta Wizara hii ndio kila kitu ndio mama wa kila kitu na ndio maana hata kwenye bajeti yake unaona kwamba ni fedha nyingi sana inatengwa lakini ukiangalia mahitaji ambayo yapo ni hazitoshi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, binadamu ameumba kupenda kusikia neno lile linalomfurahisha ndio binadamu wanafurahi lakini mtu anapenda kusikia neno lenye utu. Neno ambalo linagusa watu na mahangaiko ya watu, shida za watu huyo ndio mtu. Kwa hiyo, naamini Wizara hii chini ya Mama Angellah Kairuki, ninyi ni watu, sasa kwa sababu ni watu mna utu naomba mnisikilize haya nayojaribu kuyasema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, majimbo yetu yanatofautiana sana, kuna majimbo ambayo yameeanza kupata fursa za kiwekezaji, fursa za migao ya Serikali miaka nenda rudi. Toka wakati huo enzi za mkoloni yalipata hiyo bahati lakini kuna majimbo yalisemwa kwamba haya ni pembezoni tusubiri kwanza. Yakasubiri kwa muda mrefu, sasa hivi ndio yanaanza kuibuka sawa na lile Jimbo langu la Nyasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, majimbo haya au wilaya hizi za aina hii ndizo ambazo zinachangamoto kubwa na siku nyingine nilikuwa naziita Wilaya za TASAF yaani ni maskini. Sasa wilaya hizi ndizo zinazokumbana na changamoto nyingi lakini kwa sasa kwa utaratibu unaoendelea naona pia hizo wilaya au haya majimbo ya aina hiyo itakuwa ni ngumu sana yenyewe kupiga hatua ya kuyafikia hayo majimbo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu gani nasema hivi? Tuna ile hali ambayo tunaizungumza hasa katika migao yetu ya fedha, kiurahisi tunagawa fedha kila jimbo tupate sawa. Kweli sisi Wabunge ni vizuri tupate sawa lakini mtu mwenye kata 20, vijiji 84, vitongoji 423 kama Wilaya yangu ya Nyasa. Unategemeana kwamba tukipeana kwa mtindo huo sisi tutawafikia lini hawa wenzetu ambao sasa wameshaanza kupata kwenye zile kata au vijiji vinajirudia. Vijiji 84 unahangaika upate angalu zahanati 20 za kukaa angalau kwa umbali umbali watu wapate huduma, unakuta wewe unapata zahanati moja wenzako wengine wanapata zahanati 3, 4. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo hatuwezi kulifumbia macho lazima tuseme, na tunatabia ya sisi wakati mwingine kusema tukishakuwa kwamba yule mtu tunayemfikiria hayupo dunia au hayuko kwenye kiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Mheshimiwa Mama Angellah Kairuki, kwa sababu wewe una utu tunasema hapa hapa sasa hivi. Haturidhiki na mgao unavyokwenda. Kwa mfano, hata hizi shule za sekondari kuna wengine kata zao hazina hata hiyo sekondari lakini pia hata hizo kata ukiziangalia zina hali mbaya sana au zimetengwa kijiografia. Kata kama ya Mipotopoto ukienda kule Mitomoni unavuka katikati kilometa 40 ndo unafikia kijiji kingine cha Mipotopoto. Sasa kwa mazingira kama hayo hao watoto watasomaje? Lakini tumeshaandika barua nyingi ziko kwenye mabenchi yenu, tumezileta, tumelalamika na tunasema kwa dhati lakini unakuja ikija migao inaendelea kwa mtindo ule ule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najiuliza changamoto ni nini? Kwamba sisi Wabunge tunasema uongo kiasi kwamba hatustahili kusikilizwa au ni nini? Lakini pia kuna hali ya kutokuwaamini wale ambao wapo kwenye maeneo. Unakuta jambo la kuweza labda pengine kuifanyia kazi kwa haraka mpaka atoke mtu Wizarani aende huko na yeye kwa sababu ya muda wake ni mfupi ataenda kukagua sehemu fulani atachagua tofauti na kile ambacho pengine hata wewe Mbunge umekipendekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shule niliitembelea, mfano inaitwa Songambele, shule ile nilikuta madarasa mawili yapo pamoja yana nyufa yana hali mbaya na mle watoto walikuwa wanaingia wanacheza. Nikaona kwa nini tuunde tume ya kukagua mtu gani amesababisha kifo, nikasema wananchi hali hii si hatari wenyewe tunaiona na walinilalamikia. Nikasema ndio, nikasema tubomoe kwa usalama tutaendelea na masuala ya ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka leo nimeandika barua chungumbovu kwenye Wizara hata sisikilizi hivi mlitaka nifanyaje? Angekufa kwanza mtu halafu ndio niwaambie, ndugu zangu tusiende hivyo. Mama anafanya kazi kubwa ya kutafuta hizo fedha basi tuzitendee wema na kwa haki zaidi lakini kuna majengo. Kuna jengo la Sekondari Mbamba Bay, nimeshasema…

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Stella Manyanya, kuna taarifa.

TAARIFA

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mchangiaji anayechangia kwamba jambo hili limekuwa likijirudia sana na kwa kuwa jambo hili limekuwa likijirudia na wewe umekuwa ukiomba mara kwa mara na husikilizwi. Unaonaje leo Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya sisi kama Wanaruvuma tuondoke na Siwa hapa mpaka Siwa hili litakapokuja kufuatwa Ruvuma na darasa hili liwe limeshajengwa. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Stella Manyanya.

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nasmhukuru sana Mheshimiwa Msongozi, mdogo wangu kwa kunipa hiyo taarifa ambayo imeongeze thamani, isipokuwa Siwa nakusihii tusiondoke nayo maana yake Bunge litakuwa limeshasimama na itakua tumekosa kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba ni mambo ambayo yanahuzunisha kuna majengo yapo. Kwa mfano pale Mbamba Bay Sekondari kuna jengo la ghorofa chini ya ofisi ya utawala juu makataba, kwa sababu ule mradi ulikwisha basi hakuna hela ya kumalizia. Tunaambiwa tutenge mapato ya ndani, mapato ya ndani kwenye wilaya, Halmashauri ya Nyasa ndio hiyo ya Ki - TASAF. Sasa hivi tunaishusia kwamba ipunguze hata hela ya kupeleka kwenye maendeleo, tutakamilisha lini?

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Stella.

MHE. ENG. STELLA MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nisaidiwe, twende tutembelee ile wilaya tuione vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naunga mkono hoja. (Makofi)