Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika hoja iliopo mbele yetu hoja ya TAMISEMI. Kwanza kabisa nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima lakini pia nichukue nafasi hii kumpongeza Dada yangu Kairuki na Manaibu wake wawili mapacha kwa kazi nzuri wanazozifanya hakika nimejionea. Mheshimiwa Kairuki hata ukipiga simu saa nane usiku anapokea. Anapokea anakusikiliza lakini pia hata Manaibu wake wawili wanapokea simu wanakusikiliza wanakutatulia changamoto, hongera sana, huo ndio uwajibikaji na utumishi ulio wa kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kumsahau Mkuu wangu wa Mkoa Queen Sendiga, naye nampongeza sana anaisimamia ilani vizuri katika Mkoa wetu wa Rukwa. Kipekee nimpongeze sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anazozifanya. Wanawake na wananchi wa Mkoa wa Rukwa wamenipa salamu tunamshukuru sana, tumeweza kupokea miradi; miradi ya madarasa, miradi ya maji, miradi ya barabara, miradi mingi fedha nyingi sana tumezipokea katika Mkoa wetu wa Rukwa. Hongera sana Rais wetu, chapa kazi tuko pamoja na wewe, 2025 kitaeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kuwapongeza Simba. Wamembamiza mtu jana, wamembamiza vibao viwili. Hongera sana Simba Sports Club. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie sasa kwenye hoja zangu za msingi. Mkoa wangu wa Rukwa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa kuna taarifa.

TAARIFA

MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kuniona. Naomba kumpa taarifa mchangiaji kwamba wananchi hawakututuma huku ndani kuja kuongea ushindi ushindi wa michezo. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Bupe naomba uipokee hiyo taarifa, uipokee hiyo taarifa.

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namsamehe ngoja niendelee asinipotezee muda.

MWENYEKITI: Uipokee hiyo taarifa.

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sipokei. Niingie kwenye suala la 10% ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu…

MWENYEKITI: Taarifa inatoka wapi? Haya taarifa Mheshimiwa.

TAARIFA

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mchangiaji kwamba miongoni mwa mambo ambayo Mheshimiwa Rais anayaunga mkono ni pamoja na mambo ya michezo. Kwa hiyo kilichofanyika jana ni jambo ambalo linaendeleza hamasa kubwa ya Mheshimiwa Rais na Simba wameitekeleza kwa vitendo. Naomba kutoa taarifa. (Makofi)

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, hiyo taarifa ya mwisho kuhusu suala la michezo. (Makofi)

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepokea kwa mikono miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie sasa kwenye mambo yangu ya msingi nianze kuongelea suala la 10% ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Nimshukuru sana Rais na Serikali yetu. Kwa kweli jambo hili la 10% ni zuri sana na limefanya hamasa kubwa sana kwenye jamii yetu, lakini nimesikia juzi Mheshimiwa amesema kunakuwa na ubadhirifu wa fedha ambazo zinapotea bila sababu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi fedha kama zinapotea tusiwahukumu wanawake wale wanaokopa. Wale wanawake wanaokopa na vijana wanarudisha kwa uaminifu mkubwa sana. Wanacheza VICOBA wanarudisha. Hizi fedha kama zinapotea inawezekana kuna vikundi hewa ambavyo vinapoteza hizo fedha kwa asilimia kubwa. Naomba tuliangalie vizuri. Hii fedha ibakie kwanza halmashauri, wanawake wakihamishiwa mikopo hii kwenye mabenki wengi wao watashindwa kwenda kukopa kwa sababu ya dhamana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, 10% hii inasaidia sana makundi haya na sisi kama Mkoa wa Rukwa tunasubiri sana hii utaratibu ulioanza wa kilimo tunasubiri tunajua kwamba 10% hii itasaidia sana wanawake wengi wanalima Mkoa wa Rukwa kwa hiyo 10% hii, 4% na 2% itawasaidia sana makundi haya kwa ajili ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya pili. Nichukue nafasi hii pia kumpongeza Rais kwa kutangaza ajira 21,200. Ajira ni nzuri, nyingi sana na tunamshukuru sana Rais kwa kujali watoto wake ambao wamesoma lakini wanaishi mitaani hawana kazi. Ushauri wangu, hizi nafasi 21,200 zigawanywe kwenye mikoa husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi nafasi ni Rais na Serikali yetu inatangaza kila mwaka. Mwaka uliopita ilitangaza ajira 6,000 lakini wengine mikoa mingine hatukuona kama kuna vijana wetu ambao wamepata hizi ajira. Ushauri wangu, hizi ajira zigawanywe kwenye mikoa tugawanye kwa uwiano bila kupendelea ili vijana wa mikoa yote waweze kufaidika na hizi ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Bupe ahsante sana, muda umekwisha.

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)