Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ilio nichangie kwenye hii Wizara ambayo ni Wizara muhimu sana iliyotubeba sisi Wabunge, Wizara ya TAMISEMI chini ya Ofisi ya Rais, lakini ambayo inasimamia Tawala za Mikoa, halmashauri zetu na kule kwetu tunakotoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze moja kwa moja kwanza kushukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi ambayo anawafanyia Watanzania. Anatubeba Watanzania kama watoto wake, kama mama anavyobeba watoto wake. Amesambaza fedha majimboni, kila jimbo, ukijaribu kufuatilia kila Mbunge akisimama anazungumzia habari ya mabilioni mabilioni na sisi kule Arumeru Mashariki pia tumepata hiyo neema ya kupokea mabilioni. Kwa kweli tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kipekee kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, Dada yetu Mheshimiwa Angellah Kairuki pamoja na wasaidizi wake Mheshimiwa Dkt. Dugange na Mheshimiwa Deo Ndejembi ambao kusema kweli wanafanya kazi nzuri. Kwa dhati kabisa niseme kwamba hawa vijana wawili ni vijana wema sana lakini Mheshimiwa Waziri naye ni mwema sana, kila Mbunge amesema kwamba akipigiwa simu anapokea, kama asipopokea anarudisha ujumbe kwamba nitakupigia. Tunakupongeza sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema tumepokea fedha nyingi kwa ajili ya maendeleo Jimboni kwangu. Naomba niseme machache kisekta kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jimboni kwangu changamoto kubwa sana ni miundombinu ya barabara. Ni ngumu kwa sababu lile jimbo letu sehemu kubwa limebeba Mlima Meru, kwa hiyo wananchi wanaishi kwenye miinuko, miteremko ya Mlima Meru na kwa hiyo miundombinu barabara huwa zinaharibika sana kila msimu wa mvua na barabara nyingi ni za udongo na changarawe. Kwa hiyo tuna shida kubwa ya barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo niseme kwamba TARURA wamekuwa wanafanya kazi nzuri. Naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mtendaji Mkuu Engineer Seif, kwa kazi ambayo anafanya. Ni kijana mzuri ambaye ukimpigia simu anapokea na anachukua hatua saa hiyo hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwangu nina barabara ambazo ni ahadi za Viongozi Wakuu. Barabara ya King’ori ni ahadi ya Rais kwamba itajengwa kwa kiwango cha lami, lakini mpaka sasa hiyo ahadi haijatekelezwa. Hiyo barabara inaanzia Malula – Kibaoni - Ngarenanyuki lakini inapitia King’ori. Kutoka Ngarenanyuki iko chini ya TANROADS, lakini ni barabara muhimu Mheshimiwa Waziri anisikilize vizuri. Ile barabara ikijengwa kwa kiwango cha lami itakuwa bypass ya mashariki ambayo itasaidia sana utalii kwenye lile jimbo na kuchangia uchumi kwa kuwa itazalisha ajira kwa kata nane ambako inapita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana waifikirie ni ahadi ya Rais na ahadi ni deni na kusema ukweli ahadi za Viongozi Wakuu zinatusumbua na ziko nyingi. Nilitoka kuzungumza na Naibu Waziri Mheshimiwa Silinde akaniambia inatakiwa ifanyike operation ya kuondoa madeni haya ya ahadi za Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA wamepata shilingi bilioni 855. Fedha hizi kila tukizichambua bado ni kidogo. Bajeti ya TARURA iko chini kwa sababu wanahangaika na barabara za vumbi, changarawe ambazo huwa zinaathiriwa sana na hali ya hewa. Kwa hiyo tuiombe TARURA waongezewe fedha na kule kwetu ambako barabara zinapanda milimani na siyo kwetu tu, maeneo yote ambayo yana milima TARURA wanapata shida sana. Waongezewe fedha, sisi kwa mwaka tunapata kama shilingi bilioni mbili kama na nusu. Hizo fedha ni kidogo, tungepata kama shilingi bilioni tano, ungeona Wabunge wangekuwa watulivu. Wangeona kwamba kazi zinafanyika na zinaonekana. Kwa sasa hivi nakiri kwamba Bajeti ya TARURA iko chini. TARURA wanafanya kazi vizuri lakini hawapati fedha za kutosha, muhimu waongezewe fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nafuatilia pia kupanga na kusema kwamba tunatoa fedha kiasi Fulani, ni suala moja lakini kutekeleza kwa maana ya kutoa fedha miradi itekelezwe ni suala lingine. Taarifa nilizonazo ni kwamba sisi tulipata shilingi bilioni 2.1 kwa mwaka huu wa fedha ambao tunamaliza kesho kutwa, lakini mpaka sasa tumepata shilingi bilioni moja na chenji. Utekelezaji unafanyika umeshafikia 46% peke yake. Tunaomba fedha zitoke kwa wakati ili miradi ambayo imepangwa kutekelezwa itekelezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali. Toka kipindi cha miaka miwili ya Mheshimiwa Rais aliyokaa madarakani, Sekta ya Afya tumepata fedha nyingi. Nimepata Kituo cha Afya cha Mareu, kazi iliyofanyika ni nzuri sana, lakini niseme kwamba tulipata ahadi ya vituo vitatu vya kimkakati kwa kila tarafa. Sasa namuuliza Mheshimiwa Waziri, nimepata kituo kimoja, vile viwili viko wapi? Pale Karangai kuna eneo tumetenga kwa ajili ya kuweka kituo cha afya naomba wakumbuke mwaka huu wa fedha tupate kituo kingine. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante sana, kengele imeshalia.

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ni ya kwanza, si bado ya pili?

MWENYEKITI: Mheshimiwa ni ya pili hiyo.

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)