Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Charles Muguta Kajege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwibara

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipatia nafasi niweze kuchangia katika hotuba ya Ofisi ya Rais – TAMISEMI. Kama walivyofanya watangulizi wangu na mimi napenda nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana ambayo amefanya katika kipindi hiki kifupi. Katika kipindi hiki kifupi tumeona miradi yote mikubwa inaendelea kutekelezwa kawa kasi kubwa na kwa ubora wa hali ya juu, mahusiano yetu na nchi zingine za nje yamepanuka zaidi na kukua zaidi, biashara yetu ya nje na ya ndani imekua na kupanuka zidi yote hii katika kipindi kifupi hiki cha utawala wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nichukue fursa hii kumpongeza Waziri wa TAMISEMI na timu yake kwa uongozi mzuri ambao wamefanya katika kipindi hiki kifupi. Kama walivyozungumza wezangu imekuwa ni raisi zaidi kumpata Mheshimiwa Waziri Kairuki, muda wote ukimpigia simu anapokea simu na bado anakuletea mrejesho ambao ni mzuri. Nakupongeza sana Waziri wetu Kairuki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Mwibara nitazungumzia baadhi ya changamoto ambazo ndiyo kikwazo kikubwa katika maendeleo yetu. Changamoto ya kwanza ipo katika Sekta ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitembelea katika shule za Mwibara nyingi hasa shule za msingi utakuta kuna upungufu mkubwa sana wa vyumba vya madarasa na hata vile vyumba vya madarasa viliyopo bado vimechakaa sana, wanafunzi katika chumba kimoja utakuta ni zaidi ya mia moja, vilevile vyumba hivi vingi havina sakafu kwa hiyo watoto wanasoma katika vumbi. Shule hizi ni kama Shule ya Msingi Gundu, Chitengule, Nampangala, Igundu, Buyomba, Susi, Bwanza, Shabirizi, Visambu, Bunele, Mlagata, Kinkombe na Kabaija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kutembelea katika hizi shule ni kama hazipo, kwa sababu majengo ni mabovu na mengine sasa hivi hawaruhusiwi hata watoto kuyatumia, kwa hiyo ni kama majengo hayapo. Vilevile upungufu wa madawati madarasa mengi hayana madawati kwa hiyo wanafunzi wanasomea chini. Sasa ukiangalia kwamba madarasa kwanza wanafunzi wako wengi katika darasa moja vilevile ni kwamba hawana madawati plus kwamba hata sakafu hazipo, ni chafu, ni vumbi kwa hiyo mazingira ya kusomea hawa wanafunzi yanakuwa ni magumu sana. Sasa inakuwa ni vigumu kumchukua mwanafunzi anatoka katika madarasa haya aka–compete na wanafunzi wengine ambao wanatoka katika mazingira mazuri sana ya elimu, kwa hiyo lazima naiomba Serikali iweze kuangali hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kingine ni upungufu wa walimu. Katiba hotuba ya TAMISEMI Mheshimiwa Waziri amesema kuna upungufu wa Walimu zaidi ya 89,932 katika shule za msingi wanaokuja kuajiriwa mwaka huu tunaona ni kama 13,000 peke yake ambayo ni sawa sawa na asilimia 14 hawa walimu ni wachache sana hawatoshi. Nilikuwa naomba Serikali yetu ifikilie namna ya kuongeza walimu, kwa sababu kama hatuna walimu hizi shule tunatoa elimu ya namna gani kama hatuna walimu na tulikubaliana kuanzia mwanzo kwamba mojawapo ya maadui wetu ni ujinga sasa hatutoweza kutoa ujinga kama walimu hawatoshi katika mashule yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu nyingine ambayo ina changamoto ni katika sekta ya afya. Kwa sasa hivi ninavyo vituo Vitatu vya Afya Kisolya, Kasaunga, Kasuguti lakini bado havijakamilika, hivi bado havina majengo kutosha, vifaatiba havipo na wauguzi hawatoshi. Ningeomba sana Serikali ifikirie namna ya kuvikamilisha vituo hivi ili viweze kutoa huduma inayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna maeneo ambayo sasa huduma ya afya iko mbali sana, kwa mfano Kata ya Igundu na Kata ya Namuhula nilikuwa nasikia kwamba Serikali ifikirie kujenga vituo vya afya katika Kata hizo mbili. Vilevile mwaka jana wakati ziara ya Mheshimiwa Rais katika Wilaya ya Bunda Tarehe Saba Februari, alielekeza kwamba hospitali ya Halmashauri nyingine ijengwe katika Jimbo la Mwibara, hilo agizo bado halijatekelezwa naomba hii Wizara ifikirie namna ya kujenga hiyo hospitali mapema sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ni michango ya wananchi kusaidia katika miradi ya maendeleo. Sina tatizo na michango, lakini tatizo langu ni kwamba michango mingine imekuwa ya holela. Kwa mfano, juzi nilipokuwa Jimboni, nilipita katika Kijiji kimoja cha Busambara. Hawa wameletewa pesa shilingi 54,824,000 kujenga matundu 20 ya choo. Wananchi wameombwa kuchangia tena shilingi 15,000 katika kila kaya. Nikawauliza, hivi gharama ya choo kimoja, tundu moja ni kiasi gani? Wakasema ni shilingi 1,500,000. Sasa kwa hesabu rahisi ni shilingi milioni 30. Nikawauliza, hizi Shilingi milioni 24 zinazobakia zinakwenda wapi? Hawakuwa na jibu. Nikawaambia wananchi msichange, hizo pesa zinatosha. Nilikuwa naomba, Serikali yetu iangalie vilevile kuhusu uchangishaji holela kutoka kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine, bado kuna upotevu wa pesa katika Jimbo langu. Kuna wizi tuseme, kwa mfano, kuna shilingi milioni 300 ambazo zimepelekwa katika Kituo cha Afya cha Kasuguti, hazijulikani zilipo; kuna shilingi milioni mbili nilitoa katika Kata ya Nyamihoro kutoka katika mfuko wangu wa Jimbo, hazijulikani zilipo; kuna Shilingi milioni moja ilikuwa kwa ajili ya ujenzi wa choo katika Shule ya Msingi ya Msambara, VEO kakimbia nazo hazijarudi; na vilevile nilitoa shilingi 500,000 kwa ajili ya Nyamihoro na zenyewe hazijulikani zilipo. Naomba sasa wakati wa majumuisho nipate majibu ya nini kinafanyika au tutapataje hizi pesa ziweze kufanya maendeleo katika jimbo langu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ni kuanzishwa kwa kidato cha tano katika Shule za Sekondari za Nansimo na Buramba. Katika Shule ya Nansimo miundombinu imetosha, yaani kuna mabweni na madarasa, yanatosha; lakini katika Shule ya Buramba kuna madarasa lakini hakuna bweni. Nilipoongea na Afisa Elimu, akasema kwamba haiwezekani kuanzisha Kidato cha Tano katika Shule ya Sekondari ya Buramba kwa sababu hamna bweni. Mimi naona hilo siyo tatizo, haya mambo tumeambiwa kuanzia miaka mitano iliyopita mpaka leo na shule haijaanzishwa. Naomba tuanzishe Kidato cha Tano, bweni litatufata baadaye. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWNEYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Charles Kajege.

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naunga mkono hoja Ofisi ya Rais, TAMISEMI. (Makofi)