Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana; naanimi kuna mtu atajitoa huko mbele ya safari utaniongezea muda kwa kuanzia.

Mheshimiwa Spika, naomba kwanza kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Angellah Kairuki kwa uteuzi wake, Mheshimiwa Kairuki ni mtu muungwana. Tarehe mbili mwezi wa pili aliniahidi hapa kwamba atakuja ukonga nilithibitishie Bunge lako tarehe 23 Februari alikuja na hakuja kufanya kazi ndogo, alifanya kazi kubwa sana, tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda naomba nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. Wakati nachaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Ukonga mwaka 2020 bajeti ya TARURA Wilaya ya Ilala ilikuwa bilioni 8.3 na iliyokuja Jimbo la Ukonga ilikuwa bilioni 2.2. Hivi tunavyozungumza mwaka wa fedha 2022/2023 bajeti hii ya Wilaya ya ilala imefika bilioni 24, na kwa Jimbo la Ukonga peke yake zimekuja bilioni 11.7 zaidi ya mara sita ya bajeti tuliyoikuta; ni kazi kubwa sana imefanyaka tunakupongeza sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Chanika – Umbozi inajengwa kwa kiwango cha lami, Barabara ya Mombasa – Mazizini ile eneo la Mombasa lilioharibika barabara hii tulijenga wengine tukiwa madiwa imerudishwa lami na taa za barabarani.

Mheshimiwa Spika, na barabara nyingine ambazo Mheshimiwa Waziri akija ku-wind up hapa nitataka anipe maelezo ni zile za mapato ya ndani Majoe, Mwanagati na Kitunda. Nilikueleza kwamba halmashauri haiwezi kujenga barabara, ikainyang’anya TARURA jukumu hili leo ni mwezi wa nne hawajaanza wako kwenye mchakato wa manunuzi.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni eneo la ujenzi wa BRT awamu ya tatu ujenzi umeanza na umeanza kwa kwasi sana Gongolamboto – Kariakoo. Ninachoomba Mheshimiwa Waziri miradi hii imeasisiwa mwaka 2004 imeasisiwa kipindi ambacho Gongolamboto ndio mji mkubwa leo mji umeheama, imeasisiwa kipindi ambacho mradi wa SGR haujajengwa leo SGR imechukua eneo. Imeasisiwa kipindi ambacho mwaka 2004 Kilitex kulikuwa na kiwanda, leo kuna kiwqnda cha kioo na kina mkopo wa Benki ya Dunia.

Mheshimiwa Spika, Nimuombe Mheshimiwa Waziri hebu acha alama kwenye mradi wa BRT, mradi uende mpaka Pugu ni kilomita nne tu kuongezea pale. Lipo eneo la kutosha la maegesho, lipo eneo la kutosha la kituo, lipo eneo la kutosha watu wa Kisarawe Chanika na Pugu Stesheni, kwenye stesheni mpya ya SGR watatumia mradi huo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kazi kubwa inayofanywa na Serikali lakini hali ya barabara kwenye Jimbo la Ukonga ni mbaya sana. Pamoja na bilioni hizi 11 bado Barabara za Kitunda, Kivule, Msongola, Mwanagati kuja Kitunda, Magore, Kwa Mperemba, Bombambili, Majohe, Viwege, Pugu Stesheni na Zingiziwa hali ni mbaya sana.

Mheshimiwa Spika, jana Mheshimiwa Bonnah hapa alisema mvua zimeshesha barabara zimekatika. Wananchi wamenituma kuja kuiomba Serikali; tulikuwa tunakaa hapa, Mbunge wa Mbeya mjini anakaa hapa kulilia miradi ya World Bank, Mbunge wa Nyamagana wenzetu TaCTIC imeanza, leo hata tukiwasalimia hamtuitikii. Kuna mradi wa rise upo kwenye majimbo mbalimbali Jimbo la Ruangwa lina rise bilioni 300 zimeenda kule, sijui hata Mbunge wa Ruangwa ni Mheshimiwa nani humu ndani bungeni. Basi! nafuta kauli ya Ruangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sasema hivi kwa sababu ule mradi wa DMDP ule ambao tunaambiwaga utaanza Dar es salaam niseme ukweli hauanzi leo wala kesho. Waheshimiwa Wabunge niwaombe, Waheshimiwa Wabunge wote humu mnakaa majimboni mwenu lakini mnao wananchi wenu wanakaa Dar es salaam hali ya barabara ni mbaya. Niiombe serikali ije na mkakati wa kutatua kero hii kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, hivi ninavyozungumza matumizi ya mafuta kwa siku kwenye nchi yetu ni lita takribani 10,700,000 katika hizo lita 3,400,000 zinatumika Dar es salaam sawa na silimia 31. Ukisikia hotuba ya Waziri jeuri yote ambayo TARURA wanaitumia sasa ni ile shilingi mia iliyoongezwa kwenye mafuta ambayo Wabunge waliipigia kelele kila wakati hapa na Serikali wakati huo ilikuwa inakaidi. Baada ya shilingi mia ile kuongezwa leo mafuta yanapatikana lakini barabara za TARURA zinajengwa.

Mheshimiwa Spika, sisi Wabunge wa Dar es salaam tunaomba kwa mafuta haya ya asilimia 31 iongezwe shilingi mia kwa lita tupate angalau bilini 130 za kujenga barabara. Leo bei ya mafuta Ngara ya EWURA ya mwezi huu ni shilingi 3,050, bei ya mafuta kwa Dar es salaam ni shilingi 2,847. Ukiongeza shilingi 100 kwa Dar es salaam bei ya Dar es salaam itafanana na Arusha itafanana na na Chemba ambako nako kuna Watanzania lakini zitapatikana pesa za kujenga barabara.

Mheshimiwa Spika, hatuwezi kuwa tunataja mradi wa DMDP ilhali mradi huo haupo. Naomba sana zitafutwe fedha za ndani ili Watanzania wanaoishi Dar es Salaam waweze kujengewa barabara.

Mheshimiwa Spika, kwa dakika moja naomba unisaidie mambo mawili. Jambo la kwanza naomba unisaidie kuwaambia wananchi wangu wa Jimbo langu la Ukonga kwamba kazi ya Mbunge ni kusema hapa Bungeni; na ndiyo kazi ninayoifanya sasa. Ilifikia wakati nikataka kutengeneza bango niweke picha ya Mheshimiwa Kairuki na namba yake ya simu na ya Injinia Seff wa TARURA. Maana kule ukisema Mbunge una-post salamu za pasaka yesu amefufuka mwananchi anakujibu achana na mambo ya Yesu jenga barabara; unapost post ya Ramadhani Kareem mtu anakuambia unatoa wapi nguvu za kufuturisha wakati barabara ni mbovu kazi hii hapa.

Mheshimiwa Spika, la pili unisaidie kuwaambia wapiga kura wangu kanuni ile ya 170; maana jana nilikuwa jimboni kule Majohe tukaingia kwenye matope mwananchi mmoja akaniamba Mheshimiwa Mbunge ukienda Bungeni hebu nenda na hayo matope wajue unavyopata tabu. Sasa akiniona hapa na suti inawewezekana akaniona siko serious. Kumbe ni aknuni zako ndio zinatupelekea kuja hapa kwa mavazi haya wala haina maana yoyote kwamba sikereki na kero za barabara kwenye jimbo langu.

Mheshimiwa Spika, naomba kwa dakika hizi sita itoshe, lakini frame ya hiyo shilingi mia ninayo, nitampa Mheshimiwa Waziri, nitampa Waziri wa Fedha. Kwa hiyo sasa kwenye bajeti hii tutafute fedha za ndani tuweze kujenga barabara kwenye jiji la Dar es salaam ili tuwaondolee wananchi hawa kero; ambao wengine ni wapiga kura wenu. Hakuna msiba unao safirishwa kutoka mkoani kuja Dar es salaam, misiba yote inatoka Dar es salaam kwenda mikoani na siasa ya Dar es salaam inaathiri maeneo yote.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja nakushukurusana kwa kunipa nafasi hii, ahsante. (Makofi)