Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia hoja iliyo mbele yetu, ambayo ni hotuba ya Ofisi ya Rais-TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nichukue nafsi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya katika nchi yetu. Pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Mawaziri wote pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya TAMISEMI kwa kazi kubwa wanayofanya katika Wizara hii kubwa inayohudumuia Watanzania.

Mheshimiwa Spika, mimi mchango wangu upo katika maeneo makubwa mawili; eeneo la kwanza ni eneo la sekta ya afya. Niipongeze Serikali kwa ujenzi wa hospitali za halmashauri, vituo vya afya na zahanati katika maeneo yetu, kazi kubwa sana imefanyika.

Mheshimiwa Spika, ili kuipa thamani kazi hii kubwa ya ujenzi wa hospitali za halmashauri vituo vya afya na zahanati tuiombe sana Ofisi ya Rais, TAMISEMI sasa tuweze kupata dawa za kutosha, vifaa tiba lakini pia na watoa huduma katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, tumejenga majengo mazuri sana. Tumejenga zahanati, tumejenga vituo vya afya, tumejenga hospitali ya halmashauri; sasa tunaomba tupate wahudumu ili tuwe na thamani ya majengo haya tumeyajenga.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine muhimu sana katika vituo vya afya zahanati na hospitali zetu ni upatikanaji, utunzaji na utoaji wa dawa. Kumekuwa na upotevu mkubwa wa dawa katika hospitali zetu. Dawa zinapikelewa, zinatunzwa lakini zinavyotoka kuna dawa zinatoka lakini hazijulikani zinaenda kwa nani.

Mheshimiwa Spika, Naibu Waziri wa TAMISEMI ni shahidi, tulifanya ziara takakuta dawa zimepokelewa na zimetunzwa, lakini dawa zimetolewa hakuna mfumo rasmi wa kutoa dawa katika maeneo yetu. Kwa hiyo niombe sana TAMISEMI waliangalie jambo hili kwa umuhimu mkubwa sana kwa sababu ni kero kwa wananchi wanapo kosa dawa kwenye hospitali ya Serikali, anapokosa dawa kwenye kituo cha afya lakini anapata dawa kwenye duka la watu binafsi. Hatukatazi watu binafsi wafanye biashara lakini naomba uwekwe utaratibu wa wazi wa upokeaji, utunzaji na utoaji wa dawa kwenda kwenye huduma za wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo ningependa pia nichangie ni kufanyika ukaguzi wa wataalamu wetu wa kutoa huduma za afya; kwamba kuna Madaktari wangapi, kuna Manesi wangapi kwenye hospitali za halmashauri, vituo vya afya pamoja na zahanati. Ninatoa mfano; kuna zahanati nyingine vijijini kunakuwa na nesi mmoja tu. Inatokea changamoto yoyote zahanati inafungwa. Inapotokea mama mjamzito anachangamoto ya kujifungua unakuta zahanati imefungwa; ni shida kubwa sana kwa wananchi wetu. Kwa hiyo niombe sana ifanyike human resource audit, kwa maana ya Manesi na madaktari ili tuwagawe kwa usahihi katika maeneo yetu waweze kutoa huduma kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, ninasema hayo kwa sababu nina mfano kuna Zahanati ya Meri, Zahanati ya Gosbert kule Babati vijijini yuko nesi mmoja; akifiwa, akiugua zahanati inafungwa. Kwa hiyo niombe sana Ofisi ya Rais, TAMISEMI ifanye tathmini hiyo ili wananchi wote wapate huduma.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni eneo la elimu. Tunashukuru sana Serikali imefanya kazi kubwa ya ujenzi wa madarasa, madarasa 12,000 ya sekondari na madarasa 3000 ya shule za msingi. Tunaomba sasa, baada ya kazi hii nzuri ya ujenzi wa madarasa wapatikane walimu wa kutosha katika maeneo yetu, sambamba na afya, kama nilivyosema. Upande wa elimu pia ifanyike tathmini ya idadi ya walimu nchi nzima tuwagawe kutokana na taaluma pamoja na jinsi pia.

Mheshimiwa Spika, ziko shule za wasichana katika wilaya yetu hazina walimu wa kike. Watoto wetu wadogo wa kike wanakua lakini hawana walimu wa kike; hii ni changamoto kwenye shule zetu. Kwa hiyo niombe sana waangalie taaluma. Ziko shule ambazo kuna walimu wa sayansi wengi lakini walimu wa sanaa hawapo. Zipo shule, kama nilivyosema za wasichana hazina walimu wa kike. Kwa hiyo niombe sana wafanye human resource audit ya Walimu wawagawe vizuri kwenye shule zetu ili wanafunzi wetu wapate huduma hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo pia tulianzisha ujenzi wa Maabara; na sasa kuna maboma mengi sana ya Maabara ya sayansi Biology, Chemistry na Physics. Kwa sababu sasa majengo yameshakamilika niombe sana Wizara ya TAMISEMI ijielekeze katika kumalizia maabara hizi ili wanafunzi wetu wapate kujifunza masomo haya ya sayansi kwa ajili ya manufaa yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine la mwisho niombe sana. Zimetangazwa ajira za walimu, tunajua. Kuna walimu wa kujitolea kwa muda mrefu sana kwenye maeneo yetu; wamefundisha watoto wetu na watoto wamefaulu. Sasa, linapokuja suala la ajira wanakosaje sifa ya kuwa ualimu? Kwa hiyo niombe sana Ofisi ya Rais, TAMISEMI ifanye tathmini ya walimu waliojitolea kwa muda mrefu. Wamefanya kazi kubwa kwenye nchi yetu, wamefundisha watoto wetu na Watoto wamefaulu. Kwa hiyo wapate sifa ya kuajiriwa katika shule zetu ili waendelee kutoa huduma hii kubwa ambayo walishaanza kuitoa kwa kujitolea.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya mimi nashukuru sana naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)