Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuzungumza katika Wizara hii au sekta hii ya TAMISEMI. Awali ya yote, naomba nimpongeze na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana anayoifanya ya kutuletea maendeleo Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru pia na kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI na Naibu wake na Watendaji wote wa Wizara. Nimshukuru Mkuu wa Mkoa wa Kagera Mheshimiwa Chalamila kwa kazi nzuri ya kusimamia maendeleo kwenye Mkoa wetu na wote wanaomsaidia.

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie TARURA kwa kuanza. Kama walivyosema wenzangu hapa TARURA inafanya kazi nzuri, nzuri sana ya kupigiwa mfano chini ya Engineer Victor Seif, wanastahili kupongezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli kwa ujumla wake wanatakiwa waongezewe fedha. Kazi yao ni kubwa sana, barabara za udongo nchi nzima, fedha wanayopewa haitoshi. Nikisema hivyo nizungumzie kwenye Jimbo langu na Mkoa wangu wa Kagera.

Mheshimiwa Spika, Kagera kuna mvua nyingi sana. Kama nilivyosema barabara za TARURA ni za udongo, ni changarawe, kifusi, kwa hiyo ikija mvua inakwangua zote. Wanatengeneza kwa kazi kubwa, wanafanya kazi nzuri lakini baada ya muda ikija mvua inakwangua. Kwa hiyo niombe wanapogawa mgao wa mikoa wajue kwamba Kagera kuna mvua nyingi sana. Tuna mvua miezi saba katika mwaka, mitano tu ndiyo ina ukame au minne. Kwa hiyo barabara zinaharibika sana, ziongezwe fedha katika Mfuko wa Barabara wa TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiwa TARURA bado kwenye Jimbo langu kuna maeneo mawili ambayo ni changamoto. Kivuko cha Chanyabasa na maeneo yanaitwa Kansinda hamna kivuko pale, ni mto mkubwa lakini hamna kivuko. Pale Chanyabasa jana Mheshimiwa Oliver alizungumzia kivuko hicho, ni mto mkubwa na wananchi wanavuka pale kwa tabu sana. Kivuko kipo cha miaka, tangu mwaka 1994, kimekuwa kibovu na kimezeeka sana. Wananchi wanavuka pale kwa tabu.

Mheshimiwa Spika, Kivuko hiki kinaunganisha Kata ya Kasharu, Kishogo, Lyamahoro, Nyakibimbiri, Ibwera, Kaibanja, Katoro, Kyamuraire na nyingine. Bila kivuko hiki hawawezi kwenda kwenye maeneo yao wala kuja kwenye maeneo mengine. Sasa ni ombi langu kwamba hapo pawekwe daraja badala ya kivuko. Pajengwe daraja la uhakika la kudumu ili kuondoa adha kwa wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia pale Kansinda ambako ni mto huo huo unakwenda hadi unaungana na Mto Kagera ni mto mkubwa na hakuna kivuko wala daraja. Wananchi wanavuka kwa mitumbwi ambao ni hatari sana kwa maisha yao. Naomba pale pajengewe daraja napo ili wananchi waweze kupata usalama wa maisha yao.

Mheshimiwa Spika, nikirudi Chanyabasa pale, leo ninavyozungumza ni mwezi wa nne hakuna kivuko. Vile vile wanavuka kwa mitumbwi ambayo inahatarisha usalama wa maisha yao. Kwa hiyo ni jambo jema sana kwamba pale tuwe na daraja ambalo litasaidia kuimarisha usafiri pale. Pale Kansinda ni njia mbadala ya kutokea Uganda. Ikitokea tatizo kwenye njia ya kuja Bukoba mjini pale ndiyo inachepuka inaenda Muleba hadi Dar es Salaam, ni njia pekee ya kupita pale. Kwa hiyo itumike pale kama nja mbadala au alternative route, likitokea tatizo la kuvuka pale.

Mheshimiwa Spika, nishukuru Serikali kwamba kwenye Sekta ya Elimu pale kwenye Jimbo langu nilikuwa na Kata moja ya Ukoma haikuwa na shule. Imejengwa shule ya sekondari nzuri chini ya mradi wa SEQUIP imekamilika kwa 95%. Bado majengo kama manne hayajakamilika. Niombe kwamba Wizara hii iangalie pale ikamilishe majengo hayo ili yatumike. Ni shule nzuri sana ikamilike ili iweze kukidhi malengo yaliyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie vizuizi barabarani kwenye Jimbo langu (barrier). Kwenye jimbo langu kuna barrier nyingi sana, zinasumbua sana wananchi, ni kero kubwa sana na haziko pale tu kama mapambo, yanatoza kodi, ushuru na tozo. Sasa wananchi wanatozwa kodi nyingi sana, tozo nyingi sana. Mtu ana ndizi moja, ndizi mbili anatozwa kidogo, ana nanasi anatozwa, Mheshimiwa Waziri aangalie sana eneo hili kusudi wananchi wasipate kero hii ya usumbufu wa hizi barrier hivi vizuizi barabarani ambavyo havina tija.

Mheshimiwa Spika, niongelee eneo la shule binafsi ambazo hivi karibuni Serikali imetoa waraka wa kwanza, wa pili na watatu inafuta mabweni, inasema mabasi yaendeshwe na wanawake na mkondakta wawe wanawake. Haya ni matatizo makubwa. Nafahamu sababu ya kufanya hivyo, lakini hiyo siyo suluhisho. Mimi niko kwenye sekta ya shule binafsi lakini vile vile nina watu ambao nawawakilisha ambao wana shule binafsi. Sasa wangeshirikisha watu hawa wa shule binafsi kupata ufumbuzi, siyo kutoa tu nyaraka ambazo hazitekelezeki.

Mheshimiwa Spika, mwisho naona umewasha spika ya kunisimamisha, nimalizie kwa kusema kwamba naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)