Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Jonas William Mbunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara ya TAMISEMI. Awali ya yote naomba nichukue nafasi hii nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai, na nimepata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba niwapongeze Mheshimiwa Waziri, Manaibu Waziri na Katibu Mkuu, Ndugu yangu Ndunguru kwa kuandaa randama nzuri na kuileta katika kikao hiki cha bajeti. Pia nichukue nafasi hii nimpongeze Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Kanali Laban Thomas na Wakuu wa Wilaya wa Mkoa huo kwa kusimamia vizuri fedha zinazoletwa na Serikali katika kutekeleza miradi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue pia nafasi hii nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania kwa kazi nzuri anayoifanya ya kusimamia shughuli za nchi na kuleta fedha nyingi kwenye maeneo yetu kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika majukumu haya ya usimamizi wa Serikali na utekelezaji wa miradi kwenye Jimbo la Mbinga Mjini, Mheshimiwa Rais amefanya mambo mengi kwenye ujenzi wa madarasa, ujenzi wa maabara na ujenzi wa vyoo. Pia tumepata fedha nyingi kwenye ujenzi wa vituo vya afya na zahanati, na pia tumepata fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa barabara kupitia TARURA.

Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kupanua wigo wa kutoa elimu bila malipo kuanzia shule za awali hadi kidato cha sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza kuchangia changamoto zilizopo katika jimbo langu nilikuwa naomba niishauri Serikali kupitia TAMISEMI. Kwamba, pamoja na mikakati iliyopo na vyanzo vingi vya maopato vilivyopo katika Halmashauri zetu lakini niiombe Serikali iimarishe mifumo ya ukusanyaji wa mapato. Mifumo yetu ya ukusanyaji wa mapato inaacha mianya mingi, fedha nyingi zinapotea, tunapokuja kupanga matumizi tunakosa fedha kwa ajili ya kupangia matumizi. Kwa hiyo tungeanza kudhibiti kwenye upande wa usimamizi wa mapato tungeweza kuwa na kiasi kikubwa cha fedha kwa ajili ya kupangia mipango yetu. Kwa hiyo niombe sana Wizara ya TAMISEMI kuimarisha mifumo iliyopo ya kukusanya mapato ili tuweze kupata fedha nyingi kupitia mapatao ya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa afya nilikuwa nataka nianze na Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga. Mara kwa mara nimekuwa nikisimama nachangia; Hospitali ya Wilaya ya Mbinga ilijengwa mwaka 1970. Ilijengwa kama kituo cha afya lakini badae ikapandishwa hadhi kuwa hospitali ya wilaya. Sasa hivi majengo yale ni chakavu yana hali mbaya; na mara nyingi nimekuwa nikiomba Serikali wakati inaendela na kujenga upya au kufanya ukarabati wa hospitali kongwe basi inategemea kabisa katika bajeti hii ya mwaka 2023/2024 Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Mbinga itakuwa imepewa kipaumbele. Kwa hilo naomba niseme, pamoja na kwmaba Mheshimiwa Waziri unafanya kazi nzuri, unatukutanisha Wabunge na kupata changamoto zetu, unatupa taarifa, lakini kwenye hili la hospitali ya wilaya kama sitapata mgao wowote kwa ajili ya kutekeleza ujenzi wa hospitali hii mpya nahakikisha kabisa mwishoni nitang’ang’ania shilingi yako ili ujue kwamba na sisi tunaumia kupitia kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa afya nilikuwa naomba pia Serikali itupe mgao wa kituo cha afya katika Kata ya Utiri. Vilevile niiombe Serikali iendelee na mkakati wa kukamilisha maboma yaliyojengwa kupitia nguvu za wananchi, ya vituo vya afya pamoja na upande wa elimu yakamilishwe. Hii ni kwa sababu nguvu za wananchi zimetumika hivyo majengo haya tusipoyakamilisha wananchi hawatatuelewa. Kwa hiyo nikuombe sana kwenye kutekeleza au kwenye kupanga haya majukumu tuhakikishe kwamba haya maboma yanakamilishwa.

Mheshimiwa Spika, suala lingine nilikuwa ninalotaka nichangie ni kwenye upande wa barabara. Kama nilivyosema awali, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutupa fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara katika maeneo mabalimbali kwenye majimbo yetu. Hata hivyo, kwa upande wa Jimbo la Mbinga Mjini kuna barabara ya Mbinga - Mpepai – Mtua, kilomita 42. Barabara hiyo ni mbovu hasa kipindi cha mvua. Sasa hivi ninavyoongea katika Jimbo la Mbinga Mjini mvua zinaendelea kunyesha na barabara hii ni mbovu imeharibika kiasi kwamba magari hayawezi kupita na wananchi hawawezi kusafirisha bidhaa mbalimbali Pamoja na mazao. Kwa hiyo niwaombe sana katika bajeti hii zitengwe fedha kwa ajili ya matengenezo ya barabara hii ya Mbinga – Mpepai – Mtua, kilomita 42.

Mheshimiwa Spika, lakini tena kuna barabara nyingine ya Mbinga – Kitanda - Masimeli hadi miembeni; naomba nayo pia itengenezwe. Pia Barabara ya Uzena - Mlole na barabara ya Mbinga - Ruwahita.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)