Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Nitumie nafasi hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii, lakini nikushukuru.

Mheshimiwa Spika, kwa namna pekee nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii Pamoja na wasaidizi wake wote, kwanza kwa kufanya utaratibu wa kukutana na Wabunge wa Majimbo yote angalau kwa kujua changamoto za majimbo yetu; lakini pili kwa taarifa ya mtiririko wa fedha zilizoenda majimboni kwetu, jambo linalotusaidia kufatilia na kusimamia fedha hizi. Nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri pia kwa kukubali pendekezo letu la kutoa bei elekezi za vifaa vya ujenzi kulingana na jiografia za maeneo yetu. Ingawa ninatambua uamuzi wake ni mzuri lakini bado kwenye eneo kama la Ukerewe bado changamoto ni kubwa sana. Kwa hiyo pamoja na kutoa bei elekezi kwa Mkoa wote wa Mwanza Ukerewe ichukulie kama special area katika kutoa bei elekezi ya ununuzi wa vifaa.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya. Kwa mtitiriko wa fedha kwenye Jimbo la Ukerewe pekee kwa mwaka huu wa fedha mpaka hivi ninavyoongea tumepata takriban bilioni nane kwa ajili ya miradi mbalimbali ya maendeleo, kwa kweli ni jambo kubwa linahitaji kupongezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwenye eneo hili nimshauri Mheshimiwa Waziri, Mhehsimiwa Rais anapoleta fedha hizi kwenye maeneo yetu, pamoja na lengo la msingi la kukamilisha miradi mbalimbali ya maendeleo lakini vilevile ni pamoja na kuchochea uchumi wa maeneo husika. Kwa sababu kwa mfano kwenye eneo la Ukerewe imekuja takriban bilioni nane, inapokuja bilioni nane kwenye eneo la Ukerewe basi ioneshe reflection kwenye maisha ya wananchi wa Ukerewe; kwamba kweli kwenye eneo letu imekuja bilioni nane. Na kwa sababu hiyo inapokuja bilioni nane vifaa vya ujenzi vitanunuliwa nje ya Ukerewe, wananchi wa Ukerewe hawawezi ku - feel ile bilioni nane kama imekuja kwenye eneo lile.

Mheshimiwa Spika, sasa, inawezekana huko nyuma tulikuwa tunanunua vifaa nje ya eneo husika kwa sababu ya bei, lakini sasa kwa hii bei elekezi mlioyitoa, nimuombe Mheshimiwa Waziri atoe mwongozo. Kwamba, kama hakuna sababu zozote za msingi basi vifaa kwa ajili ya ujenzi viweze kununuliwa kwenye maeneo husika ili angalau hata ile hali ya maisha ya wananchi wenye eneo husika iweze kuonekana kutokana na ile fedha iliyoenda kwenye eneo husika.

Mheshimiwa Spika, lakini tunaleta fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwenye maeneo yetu; na kwa mwongozo alioutoa Mheshimiwa Waziri, ametoa maelekezo viongozi wa Serikali za Mitaa washiriki katika kusimamia miradi hii pamoja na kuhamasisha wananchi katika kupanga namna ya kutekeleza miradi hii. Hiyo ni taswira ya umuhimu wa viongozi wa vijiji na vitongoji kwenye utekelezaji wa mirdi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maslahi ya viongozi wa Serikali za mitaa bado yako chini sana. Niombe Mheshimiwa Waziri, hebu tuiangalie, Serikali iangalie ni namna gani kuboresha maslahi ya viongozi hasa wa vijiji na vitongoji. Bado ni changamoto kubwa sana pamoja na kazi kubwa wanayoifanya katika kusimamia miradi yetu ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo nilitamani kuchangia ni eneo la TARURA. Nitumie nafasi hii kupongeza sana Serikali, lakini nimpongeze sana Eng. Seif, Mtendaji Mkuu wa TARURA, anafanya kazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kazi kubwa inayofanyika kwenye eneo hili la TARURA barabara zilizo chini ya TARURA ndio barabara kiunganishi kati ya wananchi kwa maeneo mbalimbali, ili kusafirisha bidhaa zao, lakini na kurahisisha shughuli zao za maendeleo za kila siku.

Mheshimiwa Spika, hali ya barabara zetu kwenye eneo la Ukerewe kwa mfano, bado haziko vizuri sana. Pamoja na jitihada kubwa, Ukerewe tulikuwa tunapata bajeti ya milioni 700 leo tunapata zaidi ya bilioni 2 ni maendeleo, lakini bado pesa hizi hazitoshi. Niombe, kama walivyosema wachangiaji waliotangulia kuna umuhimu wa kuangalia namna ya kuongeza fedha zitakazoweza kusaidia TARURA kuweza kufanya kazi kubwa zaidi kwenye ujenzi wa barabara zetu.

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na kazi hii kubwa inayofanywa na TARURA, kuna mambo mawili ambayo ningependa kushauri. La kwanza ni hili la mgawo wa pesa
ambalo tayari nimekwishalisemea, lakini la pili ni namna wakandarasi wanaotekeleza miradi hii wanavyopatikana.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, tunatoa hamasa na tunahamasisha kwamba, wakandarasi wazawa wapewe fursa za kujenga barabara zetu, lakini kuna wakandarasi wazawa ambao wamekuwa kikwazo kwenye kutekeleza miradi hii ya barabara.

Mheshimiwa Spika, niombe Wizara wakati inapotoa kazi za utengenezaji wa barabara ichunguze na kujiridhisha wakandarasi hawa kama kweli wanaweza kumudu kazi hizi ndipo wapewe kazi hizo, lakini bila kufanya hivyo fedha hii haitakuwa na thamani sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nikushukuru sana na Mwenyezi Mungu awabariki sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)