Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Aleksia Asia Kamguna

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Awali ya yote sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetupatia afya na pumzi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni wajibu wetu kumshukuru Rais wetu, Mama yetu Mama Dkt. Samia, kwa jinsi anavyotupigania Watanzania. Kawaida mama huwa hawezi kuacha kuwalea watoto wake, sisi Watanzania wote ni watoto wake ndio maana anapita hukuhuku katika kututafutia chochote kile ambacho anakipata, tunamshukuru tunasema ahsante. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika maisha kuna hospitali, hospitali maana yake sio majengo, hospitali ni zile huduma ambazo zinapatikana katika sehemu husika. Kwa mfano, wauguzi na dawa na vifaa tiba, katika Tanzania na hususan Mkoa wangu wa Morogoro kuna sehemu zina upungufu, nitachukua kama mifano tu, kuna sehemu zina upungufu wa dawa na wahudumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano hospitali ya Wilaya ya Mahenge, Hospitali ya Wilaya ya mahenge ni hospitali ya Wilaya ya Ulanga inaitwa Mahenge, lakini ni Wilaya ya Ulanga; ile hospitali ina mkunga mmoja tu, jamani ni hatari sana, maana yule mkunga mmoja je, akiumwa? Wale akinamama wanapata wapi huduma? Akiuguliwa ina maana na akinamama wasiende kujifungua kwa sababu yeye anaumwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndugu zangu wana TAMISEMI, tunaomba muingalie ile hospitali. Hata huduma za ndani za mawasiliano hakuna, kwa mfano daktari hayupo, yule mtu ambaye anazalisha yuko wodini kama kuna dharura imetokea hawezi kuwasiliana na daktari maana hakuna mawasiliano ya ndani ya hospitali. Ninaomba hilo muliangalie sana kwa ajili ya mustakabali wa wanawake wa Wilaya ile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, katika Kituo chetu cha Mang’ula. Kituo cha Mang’ula ni kituo ambacho tulikuja kuomba kuomba msaada mkatusaidia tukapata zile huduma, lakini kile kituo tuna hela taslimu ambazo ni milioni 11, tunaomba tununue MSD jokofu, lakini MSD wanasema hawana jokofu kwa wakati huo. Sasa zile hela tutakaanazo mpaka lini? Tunaomba mtusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na pia kuna kituo cha Mtimbira. Kituo cha Mtimbira nimelialia sana tangu muda mrefu kwamba, kile kituo kina x-ray mashine, lakini hakina chumba cha kuhifadhia ile mashine ya x-ray. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hiyo hela ya Serikali si bora ingefanya kazi nyingine kuliko tumeipeleka pale, tumei-dump, mashine ya x-ray haifanyi kazi, huduma watu hawapati, hasa mwanamke akiuguliwa katika ile Wilaya ya Malinyi hakuna mashine yoyote ya x-ray maana tulikuwa tunaitegemea mashine hiyo na mashine haifanyi kazi. Sasa kwa mfano mtu amepata matatizo ya uzazi anafanyaje? Kwa hiyo, Wilaya nzima haina msaada wa aina yoyote wa vitendeakazi kwa mfano mashine ya x-ray.

Mheshimiwa Spika, pia kuna kata ya Mikese, Kituo cha Afya cha Mikese kile nasema ni Tanzania kwa sababu, kile kituo kiko njiani, ukitoka Dodoma, ukitoka mikoa yote, Iringa, wapi, kile kituo kiko njiani, lakini hakina huduma stahiki ambazo zinastahili pale. Wanawake wanaopanda kwenye mabasi, labda amepata tatizo la dharura akajifungue pale, ambacho kingetusaidia au watoto wadogo wakiugua ghafla kingetusaidia, lakini huduma za watoto na akinamama hakuna. Kwa hiyo, naomba mkiangalie hicho Kituo cha Mikese. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na pia nataka niongee kwa ujumla wake, wanawake wengi wanaoishi vijijini wanakabiliwa na shida ya uchumi, lakini unakuta kwamba, wale wanawake lazima wazae. Wakipata ujauzito wakienda hospitali wanaambiwa wakanunue vifaa, hivi jamani tuchukulie maisha tulikotoka, huyo mwanamke hivyo vifaa vya kununua labda vya 120,000 na huduma za mtoto ambazo ni za kuanzia mwaka sifuri hadi mitano, unaambiwa ukalipie, hela zitatoka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali inajua kabisa uzazi ni kitu ambacho mtu lazima akajifungulie hospitali kama tunavyohamasisha watu. Unamwambia akanunue vifaa vya kwenda navyo hospitali; anavipata wapi? Hospitali nyingi za mikoa yetu, siyo lazima iwe Morogoro, lakini naamini maeneo mengi Tanzania tunaambiwa tukanunue vifaa wakati mwanamke anakwenda kujifungua, wakati Serikali inasema kwamba mwanamke anapata huduma bure, lakini bure haipo, hasa katika mambo ya operation.

Mheshimiwa Spika, nataka kuzungumzia upande wa elimu. Upande huu tuna changamoto, kuna wenzangu wengi wamezungumzia kuhusu upande wa elimu. Elimu yetu ya Tanzania tunamshukuru mama Samia wa Awamu ya Sita ametoa elimu bure, lakini ile elimu bure imekuwa na changamoto nyingi kwa kipindi hiki. Elimu kweli ni bure kwenye majengo, lakini ile elimu haiwezi ikawa elimu bila vitendeakazi. Kwa mfano vitabu; shule nyingi hazina vitabu. Sasa vile vitabu tutavitoa wapi?

Mheshimiwa Spika, unaweza ukakuta watu wengi sasa hivi watoto wao wakifaulu kwenda sekondari, wanawaambia waandike vibaya ili wafeli, maana anaona kwamba akienda sekondari atatoa wapi hela za kununua vile vifaa shuleni; uniform, vitabu na vinginevyo.

Mheshimiwa Spika, sasa naishauri Serikali; tuna…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa Kamguna, malizia sentensi.

MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Spika, tuna shirika la ku-print vitabu vya Serikali, naishauri TAMISEMI kwa nini tusitumie zile mashine za kwenda kutengeneza vitabu, hatimaye watoto wetu waweze kupata vitabu kwa bei nafuu badala ya sisi wenyewe kukaa na kuhangaika halafu watu hawaendi shule.

Mheshimiwa Spika, pointi yangu ya pili…

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie; pointi ya pili, ninaomba turudishe elimu ya maarifa ya nyumbani kwa sababu watu wengi tunasema kwamba kuna utapiamlo, watu hawana elimu ya kutosha, turudishe hiyo elimu ya kusoma sayansi ya nyumbani, needlework na cookery.

Mheshimiwa Spika, kwa hayo machache, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)