Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote waTAMISEMI, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Taifa letu katika kuboresha maisha ya wananchi na pia utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni “Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu.”

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miezi tisa ya mwaka huu wa bajeti, Serikali kupitia TAMISEMI imesimamia kwa uadilifu na ufanisi mkubwa mwendelezo wa ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya vituo vya afya na miundombinu ya shule za msingi na sekondari na pia ukarabati wa barabara za vijijini. Jimbo la Mbeya Vijijini limenufaika kwa ujenzi wa shule mbili mpya za msingi na pia ujenzi wa vyumba vya madarasa kwa shule za msingi na sekondari. Ujenzi wa miundombinu ya afya na elimu umeendelea kuweka historia ya kipekee katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya. Wananchi wana imani kubwa ya huduma nzuri zitakazotolewa ikiwemo kuwepo wa watalaam bingwa, vifaa tiba vyote muhimu na dawa.

Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa ikiwemo utaratibu mpya wa mikopo kwa vijana, wakina mama na watu wenye ulemavu kupitia kwenye taasisi za fedha. Huu ni mfumo mzuri sio tu kulinda huo mfuko, lakini itakuwa ni sehemu ya kuboresha sera ya huduma ya fedha jumuishi (financial inclusion).

Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio hayo makubwa, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya bado ina changamoto za kumalizia miundombinu ya zahanati na vituo vya afya vilivyojengwa kwa nguvu za wananchi ikiwemo vituo vya afya kwa Kata ya Ilungu, Kata ya Isuto, Kata ya Bonde la Songwe na zahanati kwa kila kijiji. Wananchi wamejitahidi kujenga maboma ya zahanati na vituo vya afya na wanategemea Serikali itawaunga mkono kumaliza kazi zilizobakia bila kuchelewa.

Mheshimiwa, Spika, Serikali inaendelea na ujenzi wa barabara za lami katika maeneo ya kilimo cha kahawa na mbogamboga. Kazi zinazoendelea ni barabara ya Inyala – Simambwe ya kilometa zaidi ya 16 inayopita Kata za Inyala, Itewe, Maendeleo na Tembela. Pia kuna ujenzi kilometa 10 za barabara ya Lupeta – Wimba - Izumbwe, inayopita Kata za Swaya na Igale. Pamoja na kuwepo fedha ya wafadhili, ujenzi wa barabara hizi unasuasua sana. Serikali ichukue hatua za haraka kunusuru miradi hii muhimu kwa maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio hayo makubwa, katika Halmashauri zetu tumekuwa tunakabiliwa na changamoto hasa kwenye miundombinu ya barabara. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, barabara zinazohudumiwa na TARURA kwa asilimia zaidi ya 90 zipo kwenye hali mbaya sana kutokana na mafuriko. Maeneo mengi ya vijijini barabara hazipitiki kutokana na madaraja kusombwa na mafuriko. Naiomba Serikali ichukue hatua za haraka kunusuru hali hii ili wananchi waweze angalau kusafirisha mazao yao. Hali ya mtandao wa barabara wa zaidi ya kilometa 1,000 ni mbaya na hazipitiki kirahisi hasa kipindi cha mvua. Barabara ambazo zipo kwenye hali mbaya sana ni pamoja na; Haporoto – Ileya – Ishinda; Shamwengo - Us/Muungano; Irambo – Nsonyanga; Nsenga - Swaya-Nzovwe;

Mjele - Ikukwa; Ilembo – Isonso; Madugu – Ilindi – Isuto; Ilembo – Mbagala; Ilembo – Mwala; Iwowo - Igalukwa -Mlowo; Horongo – Igale; Songwe Viwandani – Jojo; Kawetere – Ikukwa; Mbalizi – Ilota; Nyalwela – Ngole; Nyalwela - Mbonile – Itala; Ilembo – Mbawi; na Igawilo - Hatwelo. Kwa bajeti ndogo ambayo ni kilometa chini ya 100 kwa mwaka, ni vigumu kutatua changamoto za barabara hizi kwa kiasi kikubwa zinabeba uchumi wa kilimo na madini kwa Mbeya na Tanzania kwa ujumla. Napendekeza Serikali iweke msukumo zaidi kwenye kuboresha miundombinu ya barabara kurahisisha usafirishaji wa mazao ya kilimo, itasaidia kuimarisha uchumi.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2022 Kamati ya TAMISEMI walifanya ziara Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya na Mheshimiwa Bashungwa aliyekuwa Waziri wa TAMISEMI, aliahidi Kamati ya TAMISEMI na kuagiza TARURA wajenge kwa dharura barabara kuu tatu ambazo zimejifunga kwa kipindi kirefu. Kwa masikitiko makubwa mpaka leo hakuna kilichofanyika kwa barabara hizo tatu za Haporoto – Ileya – Ishinda; Mjele - Ikukwa; na Madugu – Iyunga Mapinduzi – Isuto.

Mheshimiwa Spika, katika mazingira haya, wananchi wanakosa imani na viongozi wao na kupelekea hata uchumi kuporomoka ukichukulia haya ni maeneo muhimu kwa kilimo na uzalishaji wa madini. Kutokana na kupoteza fedha za kigeni kwenye madini na mazao ya kibiashara, naomba Wizara itoe fedha kwa udharura ili barabara hizo zitengenezwe.

Mheshimiwa Spika, napendekeza kuwepo na msukumo wa kuhakisha Halmashauri zinasimamia kikamilifu elimu ya kujitegemea kwenye ngazi zote za msingi na sekondari. Kwa shule za vijijini kushirikisha Maafisa Ugani wa Kilimo na Uvuvi kuanzisha mashamba darasa kwa kila shule za vijijini. Kwa shule za mijini kuna fursa pia kuweka msukumo wa elimu ya kujitegemea kulingana na mazingira ya shule ikiwemo elimu ya ufundi.

Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa mikopo kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu, napendekeza Serikali iboreshe mfumo wa mikopo hii kuendana na madhumuni ya mikopo ya kuimarisha kundi hili kiuchumi. Kama ilivyopendekezwa kwenye hotuba ya Waziri, uendeshaji wa mikopo hii uwe na misingi ya huduma za kifedha jumuishi (financial inclusion) ikiwemo elimu ya matumizi ya mikopo na usimamizi wa kitalaam wa mikopo. Kwa ukubwa wa mfuko huu kitaifa kuna umuhimu wa kuunda taasisi ya kifedha kuusimamia kwa tija.

Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri ya Mbeya kuna Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mbalizi ambao una wakazi zaidi ya 100,000 na shughuli nyingi za kiuchumi ikiwemo viwanda, madini na hata Uwanja wa Ndege wa Songwe. Pia katika Kata ya Utengule Usongwe kuna Kijiji cha Mbalizi ambacho mipaka yake haiungani na vijiji vingine vya kata hiyo. Napendekeza Serikali irekebishe mipaka ya Mbalizi na ipandishe hadhi kutoka Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mbalizi kuwa Halmashauri ya Mji wa Mbalizi.

Mheshimiwa Spika, mapendekezo ya kugawa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ni kilio cha muda mrefu, na Hayati Dkt. Magufuli mwaka 2020 aliagiza zoezi la kugawa lifanyike haraka na aliagiza kubadilisha jina la Jimbo la Mbeya Vijijini haraka iwezekanavyo. Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ina sifa zote za kugawa ikiwemo uwezo kiuchumi ni mkubwa sana, idadi kubwa ya wakazi, na pia changamoto za kijografia. Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya inapakana na Halmashauri zote za Mikoa ya Mbeya na Songwe kasoro Kyela na Tunduma na pia inapakana na hata Mkoa wa Njombe. Vikao vyote vya kisheria toka ngazi za chini mpaka ngazi ya Kamati za Ushauri vya Wilaya na Mkoa katika wakati tofauti vimepitisha mapendekezo hayo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.