Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI Angellah Kairuki na Naibu Mawaziri wake (Dkt. Festo Dugange na Deogatius Ndejembi) pamoja na wataalamu wa Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya kutatua changamoto za wananchi hapa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo la Moshi Vijijini, tuna changamoto za kimsingi zinazohusiana na uwepo wa vituo vichache vya afya. Pia kuna uhaba wa kidato cha tano katika shule zetu za kata za sekondari.

Mheshimiwa Spika, jimbo langu la Moshi Vijijini kuna uhaba mkubwa wa vituo vya afya. Katika kata 16 za Moshi Vijijini, ni kata tatu tu zina vituo vya afya vya Serikali vilivyosajiliwa. Katika mwaka wa fedha wa 2021/2022, TAMISEMI iliagiza tupendekeze maeneo matatu ya kujengewa vituo vya afya vya kimkakati. Mimi nilipendekeza nijengewe katika kata za Oldmoshi Mashariki; Kibosho Kirima; na Arusha Chini. Cha kusikitisha ni kwamba mimi sijapewa hata kituo kimoja kwenye maeneo nyeti na ya kimkakati niliyowasilisha Wizarani ambayo nimeyataja hapo juu.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Oldmoshi Mashariki ina eneo kubwa ambalo lilikuwa ni makao makuu ya Halmashauri. Majengo hayo yako wazi, kwani halmashauri imehamishiwa eneo lingine. Tunapendekeza, yafanyike maboresho katika baadhi ya majengo ili kituo cha afya kipatikane kwa gharama ndogo kutoka katika eneo hili. Vilevile Serikali inashauriwa kujenga chuo cha afya katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, kipaombele namba mbili na tatu ilikuwa ni kujengewa vituo vya afya katika Kata za Kibosho Kirima na Arusha Chini. Kwa kuwa vituo pendekezwa ni vya kimkakati, tunaiomba Serikali itekeleze azma ya kutujengea vituo hivyo.

Mheshimiwa Spika, katika kukagua miradi ya maendeleo jimboni, nilipokea maombi toka kwa wananchi ya kupandisha hadhi baadhi ya maeneo yanayotoa huduma za tiba kuwa vituo vya afya. Katika Kata ya Kibosho Kati, kuna msamaria mmoja aitwaye Barnabas Mallya amejenga zahanati ya kisasa yenye vifaa vyote muhimu; na inaitwa Zahanati ya Lima. Alikabidhi zahanati hii Serikalini, bahati mbaya sana rasilimali hii ya majitoleo haitumiki kikamilifu kwa sababu ya ukosefu wa wataalamu. Kuna haja kubwa ya kuipandisha hadhi hii zahanati na kuifanya kituo cha afya kwani imekidhi vigezo.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Kindi haina kituo cha afya, ila kuna kliniki (Mary Bennet) ambayo imeshakarabatiwa kwa msaada wa Wajerumani na kuwekwa vifaa tiba vya kisasa toka Ujerumani vya aina mbalimbali. Ninapendekeza kliniki hii ipandishwe hadhi na kuwa kituo cha afya.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Kimochi haina kituo cha afya. WDC ilikaa na kupendekeza Zahanati ya Shia iboreshwe iwe kituo cha afya kwani wana eneo la kutosha, naiomba TAMISEMI ifikirie ombi hili.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Kibosho Magharibi ina Kituo cha Afya Umbwe kilichojengwa miaka ya 1977 na kuzinduliwa na Baba wa Taifa. Kituo hiki ni kituo pekee katika Tarafa ya Kibosho yenye kata sita. Vilevile hutoa huduma kwa wananchi na Wilaya ya Hai hasa Kata ya Machame Mashariki.

Mheshimiwa Spika, pamoja na umuhimu wa kituo hiki cha afya, wanakabiliwa na changamoto zifuatazo: -

(a) Kituo cha Afya Umbwe kinahitaji kupanuliwa ili kukidhi hadhi ya kuwa kituo cha afya ikiwa ni pamoja na kuongeza majengo, wahudumu, vifaa tiba na dawa za kutosha.

(b) Kituo cha Afya Umbwe hakina gari la kubeba wagonjwa. Kuna uhitaji wa gari jipya ili liweze kuhudumia wajawazito na wagojwa wengine.

(c) Kituo cha Afya Umbwe hakina jengo la upasuaji, maabara ya kukidhi mahitaji ya sasa, jengo la mortuary na jokofu.

(d) Kituo cha Afya Umbwe hakina uzio.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru sana Serikali kwa kuboresha shule za kata katika jimbo langu la Moshi Vijijini. Ninaiomba Serikali ipandishe hadhi ya kuwa na kidato cha tano na sita shule za sekondari za kata zifuatazo: -

(i) Shule ya Sekondari Masoka iliyo Kata ya Kibosho Kirima. Shule hii ina eneo la kutosha na imekuwa inafanya vizuri sana kitaaluma.

(ii) Shule ya Sekondari Kimochi iliyoko Kata ya Kimochi.

(iii) Shule ya Sekondari Mpirani au Mabogini. Shule hizi ziko Kata ya Mabogini.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, pamoja na kuishauri Serikali, naunga mkono hoja.