Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, utangulizi; kabla ya kuanza mchango wango nimshukuru Mwenyezi Mungu anayetuwezesha kuendelea kutekeleza majukumu yetu ya kuwawakilisha wananchi wetu kwenye Bunge hili tukufu. Pia nimpongeze Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mheshimiwa Angellah Kairuki, Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu na watendaji wote wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kwa kuendelea kuisimamia ilani ya uchaguzi ya mwaka 2020 - 2025 inatekelezwa kikamilifu kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, aidha nikiri kuwa kazi kubwa imefanyika toka tulipomaliza uchaguzi wa mwaka 2020. Wananchi wanaendelea kuwa na matumaini makubwa kwa Serikali yao chini ya usimamizi mahari wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kuhusu utawala; Jimbo la Hanang lina kata 33 na vijiji 96, makao makuu yake yapo Mji Mdogo wa Katesh. Kwa kuwa maeneo mengi ya Jimbo la Hanang ni ya kilimo na ufugaji unakuta kuna maeneo ambayo ni makubwa jambo linalosababisha ugumu wa kutoka makazi ya wananchi na maeneo ya huduma. Ili kuboresha huduma kwa wananchi ninashauri yafuatayo yafanyike: -

(i) Kuundwa kwa mamlaka kamili ya Mji wa Katesh badala ya kuendelea kuwa chini ya mamlaka ya Mji Mdogo wa Katesh kwani Mji wa Katesh unakua kwa kasi na unahitaji usimamiwe vizuri ili kuharakisha zaidi maendeleo na kustawisha biashara na shughuli zingine za kiuchumi ndani ya mji.

(ii) Kugawanywa kwa kata ambazo ukubwa wake unatatiza upatikanaji wa huduma kwa wananchi hasa Kata za Measkron, Lalaji, Laghanga na kuifanya Kijiji cha Mureru ambacho ni kikubwa sana kuwa kata.

(iii) Kuundwa kwa vijiji vipya vya Nyasande, Merekwa, Marega, Gidagong na Nanyami.

Mheshimiwa Spika, kuhusu maslahi ya Madiwani, Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji; viongozi wa kuchaguliwa yaani Madiwani, Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji wanafanya kazi kubwa kwenye maeneo yao na muda wao mwingi unatumika kwenye kuhudumia wananchi kwenye maeneo yao. Kwa sasa Madiwani wanapata posho ambayo ni ndogo sana ila Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji hawapati chochote hivyo ninashauri yafuatayo yafanyike; kwanza kwa kuwa posho wanayopewa Madiwani ni ndogo sana ukilinganisha na majukumu waliyonayo, waongezewe posho.

Pia Wenyeviti wa Vijiji, Mitaa na Vitongoji watengezewe utaratibu wa kupata posho ili kufidia muda wao unaotumika kwenye shughuli za kusimamia maendeleo. Fedha za kuwalipa posho inaweza kupatikana kwa kurasimisha makusanyo yanayopatikana kwenye usimamizi wa mikataba inayofanyika ngazi za vijiji, mitaa na vitongoji kama vile kuuziana mashamba, viwanja na kukodi shamba, nyumba pia kurudisha kwa wakati sehemu ya mapato inayokusanywa na halmashaji vijijini na mitaani.

Mheshimiwa Spika, viongozi hawa wa kuchaguliwa wakishirikishwa na kutumika vizuri wataisaidi Serikali kwenye makusanyo ya kodi na mapato mengine na kuondoa ufujaji wa mapato ya Serikali inayostahili kukusanywa kw mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Spika, kuhusu maslahi ya watumishi; kumekuwa na usumbufu mkubwa kwa watumishi kufuatilia stahiki zao ikiwepo kupandishwa madaraja, hii inaathiri kwa kiasi kikubwa sana utendaji wa watumishi husika na kuwakosesha wananchi wetu huduma walizostahili. Wapo watumishi wengi ambao hawajapandishwa madaraja kwa wakati na hakuna uwazi kwenye eneo hili ambayo ingewaepusha watumishi ufuatiliaji usiokuwa na uhakika wa lini watafanikiwa hivyo kuathiri utendaji wao.

Pia watumishi wanaoelekea kustaafu mafao na taarifa zao ziandaliwe mapema ili kupunguza shida wanazopata watumishi wanapostaafu ikiwepo kuangalia upya suala la kikokotoo kwa kushirikiana na vyama vya wafanyakazi kwani kumekuwa na malalamiko makubwa ambayo nitachangia zaidi wakati wa bajeti ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Mheshimiwa Spika, suala la uhaba wa watumishi; ili kupeleka huduma kwa wananchi kwa kiwango kinachostahili ni muhimu kuwa na watumishi wa kutosha na wenye weledi. Jimbo langu la Hanang lina upungufu mkubwa wa watumishi hasa walimu wa shule za msingi na sekondari, manesi, tatibu, wataalam wa maabara za shule za sekondari na afya pia hatuna mtaalam hata mmoja wa vifaatiba.

Mheshimiwa Spika, watendaji wa kata na vijiji ambao ni muhimu sana katika usimamizi wa shughuli za maendeleo kwenye ngazi ya vijiji na kata nako kuna upungufu mkubwa, mfano katika jimbo langu la Hanang tuna upungufu wa watengaji 37 kati ya 96 wanaohitajika na watendaji wa kata wapo 25 wakati mahitaji ni 33. Hali hii ya upungufu wa watumishi inaathiri kwa kiasi kikubwa kasi ya maendeleo ya wananchi wetu.

Ninaiomba sana Serikali ifuatilie na kutatua changamoto kubwa ya ufungufu wa watumishi iliyopo Wilayani Hanang. Aidha, kwa kuhitimisha eneo hili la watumishi, Serikali itupatie Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri au imthibitishe Bwana Ibrahim Mbogo anayekaimu sasa kwani toka Bi. Jenifer Omolo ateuliwe kuwa Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha na Mipango nafasi hiyo imekuwa ikikaimiwa na inaathiri utendaji wa Halmashauri yetu ya Hanang.

Mheshimiwa Spika, miradi ya maendeleo na mgawanyo rasilimali; kwa niaba ya wananchi wa Hanang ninampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa miradi mikubwa inayotekelezwa maeneo mbalimbali nchini na hapa chini nitataja miradi inayotekelezwa kwenye jimbo langu hasa eneo la afya, elimu na miundombinu; stendi mpya ya kisasa Mji wa Katesh; ufunguzi wa barabara mpya Masqaroda-Ngalda – Lambo - Masakta, Mogitu - Gendabi, Mulbadaw- Basodesh, Hilbadaw - Mwanga, Garawja - Gijetamog, Dawar- Ziwa Chumvi, Waama – Diloda - Mureru, barabara za Mji wa Katesh iliwepo barabara za lami; madarasa ya shule shikizi, shule za msingi na sekondari; na ujenzi wa vituo vya afya Mogitu, Hilbadaw, Bassotu, Gisambalag na zahanati mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mambo makubwa yaliyofanyika kama nilivyotaja hapo juu, mimi ninaamini mambo makubwa zaidi yangeweza kufanyika iwapo mgawanyo wa rasilimili ungefanyika kwa kuzingatia ukubwa wa majimbo na mahitaji halisi ya maeneo husika. Mfano jimbo langu ina kata 33 na vijiji 96 kama nilivyoeleza hapo awali bado inapata mgao mdogo wa rasilimali ukilinganisha ukubwa wake.

Mheshimiwa Spika, ninaomba sana wakati Wizara ipanga fedha za kupeleka kwenye maeneo yetu iangalie mahitaji halisi ya maeneo husika. Wananchi wamekuwa wakijitolea kwenye shughuli mbalimbali za maendeleo ambapo mpaka sasa kuna maboma mengi ya madarasa, nyumba za walimu, mabweni, zahanati ambazo hazijakamilishwa kwa muda mrefu hii inaathiri moyo wa wananchi kuchangia shughuli za maendeleo mfano Zahanati ya Dang'ayda ambayo iliwekwa jiwe la msingi mwaka 2012 na maeneo kama hayo yapo mengi kwenye jimbo langu.

Baada ya maelezo haya Wizara izingatie yafuatayo; kuongeza fedha za TARURA ili kujenga kilometa 10 za lami Mji wa Katesh, kujenga madaraja ya Siro, Mto Basodesh inayounganisha Gijetamog na Basodesh, Mwanga na Sasemwega, Mara na Endasak, Mbuga Sanjaya inayounganisha Kata ya Simbay na Hidet, daraja la kuunganisha Hidet na Gidahababiye, Murumba na Ghambesh, Qalosendo na Merekwa; kuendelea kuimarisha na kukarabati barabara zilizofunguliwa; pia kuendelea kufungua barabara za kuunganisha vijiji na makao makuu ya kata.

Mheshimiwa Spika, pia kuihamisha barabara ya Bashnet – Luqmanda - Basodesh Hilbadaw - Zinga toka TARURA kwenda TANROADS kwani barabara hii kwa upande wa Singida ipo TANROADS pia sehemu ya Bashnet - Dareda ipo TANROADS hii ni barabara inaunganisha mkoa wa Manyara na Singida

Mheshimiwa Spika, kujengewa angalau zahanati tano kwa mwaka ili kuendana na mahitaji makubwa ya zahanati kwenye wilaya yetu na kuharakisha ujenzi wa vituo vya afya vya Endasak, Balangdalalu, Hidet, Nangwa, Masqaroda na kufanya tathmini kwenye kata zote ili kuboresha miundombinu ya huduma za afya kama Serikali ilivyoahidi kwa Dirma, Laghanga na Getanuwas.

Pia kukamilisha nyumba za walimu, madarasa, mabweni na zahanati ambayo maboma yake yalijengwa kwa nguvu za wananchi kwa mpango wa dharura na kuanzisha mkakati mahususi wa ujenzi wa mabweni kwenye shule za kata ambazo wanafunzi wanalazimika kupangisha vyumba mitaani (mageto) ambayo kwa Hanang ni karibu shule zote ili kuwaokoa watoto wetu na changamoto ya malezi kwa kukaa maeneo yasiyokuwa na usimamizi ikizingatiwa vijana wanaosoma sekondari bado ni wadogo.

Mheshimiwa Spika, pia shule za sekondari za kata za Ishponga, Gendabi, Dawar na Jorodom zijengwe haraka ili kuwaondoelea adha wanayopata watoto wa maeneo tajwa ya kufuata elimu kata za jirani na kwa shida kubwa.

Mheshimiwa Spika, nihitimishe mchango wangu kwa kumshukuru Waziri wa TAMISEMI Mheshimiwa Angellah Kairuki kwa kuanza kufanyia kazi maombi tuliyowasilisha wakati tulipokutana na Wabunge wengine wa Mkoa wa Manyara kwani fedha tayari zimeshatoka kwa ajili ya ukarabati wa shule kongwe ya Gendabi, ujenzi wa shule mpya ya Dillinghang, fedha za ujenzi wa madarasa na matundu ya vyoo Basotu, Dajameda, Diloda na Gawolol.

Mheshimiwa Spika, nawasilisha.