Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa neema ya uzima hata nikapata nafasi ya kuchangia Bajeti ya Ofisi ya Rais- TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii pia kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutufanyia makubwa sisi wananchi wa Jimbo la Kilwa Kusini. Kupitia TARURA, tumeweza kuongezewa fedha za barabara kutoka wastani wa shilingi milioni 500 kwa mwaka mpaka wastani wa shilingi bilioni 1.5 kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, kutokana na ongezeko la bajeti ya barabara tumeweza kujenga barabara kwa kiwango cha changarawe ili angalau zipitike kipindi kirefu cha mwaka. Kwa kutolea mfano wa barabara hizo ni kama vile Hoteli Tatu – Pande – Lihimalyao; Naiwanga - Likawage na Kikole - Mitole. Aidha, tumeweza kujenga barabara kwa kiwango cha lami kutoka Lumumba hadi Mnazi Mmoja kiasi cha kilometa 0.7 pale Kilwa Masoko. Napendekeza barabara hii iongezewe fedha kwa mwaka huu wa 2023/2024 ili ifike Kilwa Sekondari kwa kiwango cha lami. Napendekeza pia barabara ya Dodoma One (Dodoli) iunganishwe na barabara hii ya Sekondari.

Mheshimiwa Spika, tunaomba bajeti ya TARURA iongezwe ili kuendelea kukarabati barabara zetu ili zipitike kipindi kirefu cha mwaka.

Mheshimiwa Spika, tunashukuru kwa upande wa Hospitali yetu ya Wilaya ya Kinyonga tumeweza kupatiwa jengo la dharura na kupokea fedha shilingi milioni 900 kwa ajili ya kujenga maabara, jengo la upasuaji na x-ray. Tunaomba kuongezewa fedha kwa bajeti hii ili kujenga uzio na kukarabati wodi.

Mheshimiwa Spika, niombe kupitia bajeti hii Kata za Likawage na Lihimalyao ziweze kujengewa vituo vya afya kwani ni kata za pembezoni na ziko mbali kutoka maeneo ya vituo vya kutolea huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, tunashukuru kwa kupata Shule ya Sekondari Ngome pale Kilwa Masoko kupitia Mpango wa SEQUIP. Tunaomba Serikali ikamilishe shilingi milioni 130 zilizobaki ili kukamilisha miundombinu katika shule hii. Tunaomba mpango huu uendelee kwa kujengewa shule ya sekondari katika eneo la Singino, Kata ya Kivinje - Singino ili kupunguza mrundikano wa wanafunzi katika Shule ya Sekondari Kivinje.

Mheshimiwa Spika, katika mpango wa Serikali kupeleka magari ya kusafirisha wagonjwa ambayo TAMISEMI itapeleka angalau gari moja kwa kila halmashauri, naomba Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa ipatiwe magari mawili ili gari moja lipelekwe kwa ajili ya Kituo cha Afya Nanjirinji.

Mheshimiwa Spika, mwisho nitumie fursa hii kuipongeza Ofisi ya Rais-TAMISEMI kwa kuanzia na Waziri wa Nchi Mheshimiwa Angellah Kairuki, Naibu Mawaziri, Mheshimiwa Deo Ndejembi na Mheshimiwa Dkt. Festo Dugange. Nimpongeze pia Katibu Mkuu na Naibu wote pamoja na Wakuu wa Mikoa akiwemo RC wangu Mheshimiwa Zainabu Telak. Nipongeze pia Wakuu wa Wilaya akiwemo DC wangu Mheshimiwa Christopher Ngubiagai na Mkurugenzi wangu Bwana Ngilangwa na Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, kwa kweli wanachapa kazi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.