Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema ya afya na uzima, pili, nitumie fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kunipa imani ya kuhudumu katika dhamana hii muhimu sana ya Ofisi ya Rais – TAMISEMI, ninamhakikishia Mheshimiwa Rais kwamba nitaendelea kuchapa kazi kwa juhudi, maarifa na weledi wa hali ya juu.

Mheshimiwa Spika, tatu ninamshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Mheshimiwa Angellah Jasmine Kairuki kwa uchapakazi wake na umahiri mkubwa, pia ninakushukuru sana Mheshimiwa Spika kwa uongozi wako mahiri sana wa kuliongoza Bunge letu Tukufu na kwa kweli unalitendea haki nafasi hiyo ambayo Bunge hili limekupa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninawashukuru sana wananchi wa Jimbo la Wanging’ombe kwa imani waliyonipa na ushirikiano wanaoendelea kunipa na niwahakikishie kwamba tutaendelea kuchapa kazi kuhakikisha tunaendelea kutatua changamoto mbalimbali katika Jimbo la Wanging’ombe.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingi zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge, nianze kwa kusema kwamba hoja zote ambazo zimetolewa mapendekezo, ushauri na maoni, Ofisi ya Rais - TAMISEMI tumeyapokea na tutakwenda kuyafanyia kazi kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Spika, kuna baadhi ya hoja kwa sababu ya muda nitaomba nizipitie. Hoja ya kwanza ilikuwa ni pamoja na kuboresha mfumo wa kukaa mara kwa mara Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Wizara ya Afya kuhusu upatikanaji wa dawa, vitendanishi na vifaatiba kupitia Bohari ya Dawa - MSD. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali ilikwishaweka utaratibu wa Wizara hizi mbili kukaa kila robo mwaka na kufanya tathmini ya upatikanaji wa dawa lakini pia mfumo wa usambazaji na tutahakikisha tunaendelea kufanya hivyo ili kuondoa changamoto ya upungufu wa dawa katika vituo vyetu pia kuongeza ufanisi wa kupeleka dawa na vitendanishi katika vituo vyetu.

Mheshimiwa Spika, mfumo ambao unatumika kwa sasa ni wa electronic ambao unasaidia kituo cha afya na wahudumu kuweza kuomba dawa kutoka kwenye kituo chao moja kwa moja kwenda kwenye Bohari ya Dawa na Bohari ya Dawa kuleta dawa katika kituo husika bila kulazimika mtumishi kusafiri kwenda kwenye kituo husika. Kwa hiyo, tutaendelea kuboresha mfumo huu wa ki-electronic katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ilikuwa ni suala la kuweka michoro inayofanana katika majengo yetu ya Serikali, majengo ya Ofisi za Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya lakini wa Halmashauri na nyumba za Wakuu wa Idara. Serikali ilikwishafanya mapitio ya michoro yote ya majengo rasmi ya Serikali kuanzia ngazi ya Mikoa mpaka ngazi za Halmashauri lakini tunaenda hadi ngazi za Kata Ofisi za Watendaji wa Kata na Watendaji wa Vijiji tutakuwa na ramani moja ambayo itakuwa standard kwa nchi nzima ili kuleta uniformity lakini pia kuwa na msawazo sawa wa gharama za ujenzi.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la hospitali zetu na vituo vya huduma za Afya. Ni kweli Waheshimiwa Wabunge tulio wengi tumechangia juu ya umuhimu wa kuwa na vituo vya afya katika Kata zetu za kimkakati lakini pia katika Tarafa za kimkakati vilevile kuwa na zahanati katika vijiji. Serikali imefanya kazi kubwa sana katika kipindi cha miaka miwili cha uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan sote ni mashuhuda katika Majimbo yetu kila sehemu, zimejengwa zahanati kwa wingi, Vituo vya Afya, Hospitali za Halmashauri, majengo ya dharula EMD, ICU na Vifaatiba kwa wingi sana.

Mheshimiwa Spika, kipaumbele cha Serikali kwa sasa ni kuhakikisha yale majengo ambayo tayari yamejengwa lakini hayajakamilika, yanakamilika kwanza ili yaanze kutoa huduma za kutosha kwa maana ya uwezo wao katika vituo hivyo na baadae tuweze kwenda kwenye ujenzi wa vituo vingine. Kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge tunatambua uwepo wa Kata za Kimkakati na Tarafa za Kimkakati ambazo bado hazijapata vituo vya afya na zahanati lakini baada ya kumaliza kipaumbele cha ukamilishaji basi tutakwenda kwenye ujenzi wa vituo hivyo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Mheshimiwa Deus Sangu la hospitali ya Halmashauri. Kwa mujibu wa sera ya Wizara ya Afya hospitali ya Halmashauri inakuwa moja katika Halmashauri. Kwa kuwa, Halmashauri ya Sumbawanga tayari ina hospitali ya Halmashauri na kwa kuwa Serikali inatambua na kuthamini afya za wananchi wa Laela tunapeleka pale fedha Shilingi 500 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya Laela ili wananchi wasifuate umbali mkubwa kilometa 180 kwenda kupata huduma katika kile Kijiji cha Mto Wisa.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na hoja hii, imechangiwa na Waheshimiwa wengi ya vifaatiba. Serikali katika kipindi cha miaka hii miwili imepeleka fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba katika vituo vyetu vyote vilivyo kamilika na kazi ya usambazaji wa vifaa unaendelea na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge zoezi la kupeleka vifaatiba ni endelevu ili kuwezesha vituo vyetu hivi kutoa huduma bora za Afya kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, suala hili linaendelea na kwenye bajeti ya mwaka ujao wa fedha, fedha zimetengwa kwa ajili ya kuendelea kununua vifaatiba.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la mpango wa ukamilishaji wa vituo lakini na vifaatiba na hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Mbinga ambayo Mheshimiwa Mbunge ameisemea, ile ni moja ya hospitali kongwe 19 ambazo zimetengewa fedha lakini mwaka ujao wa fedha zimetengewa Shilingi Milioni 900 kwa ajili ya kuifanyia ukarabati na upanuzi, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge Serikali ilikwisha ainisha hospitali zote kongwe na chakavu pia vituo vya afya vyote vikongwe na chakavu kwa ajili ya kuendelea kutenga fedha kwa awamu ili viweze kuboreshwa na viendelee kutoa huduma stahiki kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Bunda ambayo changamoto yake ni kwamba majengo yale hayajakamilika, hii inafanana na hospitali nyingi za Halmashauri na ambazo zilipewa fedha kipindi cha mwaka 2018/2019, 2019/2020 lakini Serikali imeshafanya tathmini iko hatua za mwisho za ukamilishaji wa mahitaji halisi ya gharama za ukamilishaji wa vile vituo na hospitali na fedha itatafutwa kwenda kukamilisha majengo yote ambayo hayajakamilika likiwemo hili la hospitali ya Halmashauri ya Bunda Vijijini, Halmashauri ya Mlele na maeneo mengine ambayo hospitali zina sura ya aina hiyo.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na wananchi kukosa huduma kutokana na miradi kutokamilika pamoja na Serikali kupeleka fedha, Serikali imeshaweka utaratibu mzuri wa kuhakikisha kwanza wale wanaohusika na upotevu wa fedha za Serikali hatua stahiki za kinidhamu na kisheria zinachukuliwa kwao pia hatua za kisheria zinafuatwa na kuhakikisha kwamba hakuna watumishi ambao watakuwa wanatumia vibaya pesa za Serikali, lakini pili yale majengo ambayo hayajakamilika sasa ndio hayo ambayo yanatafutiwa fedha kwa ajili ya kwenda kuyakamilisha.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la wazabuni kuwa na madeni, Serikali ilishatoa maelekezo kwamba Halmashauri au taasisi yoyote ya Serikali kabla ya kutangaza zabuni lazima ijiridhishe kwamba kwanza kuna bajeti ya shughuli hiyo lakini pili fedha zipo ili zabuni ikitolewa fedha zile ziweze kuwa zinapatikana na kulipwa kwa wakati ili kuepusha usumbufu kwa wazabuni lakini pia kuepuka kutengeneza madeni ya Serikali yasiyo ya lazima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la utawala bora ambalo Waheshimiwa Wabunge wengi sana wamechangia lakini Mheshimiwa Mrisho Gambo aliongea kuhusu suala la ubadhirifu mkubwa katika Halmashauri ya Jiji la Arusha.

Mheshimiwa Spika, hatua zimeshaanza kuchukuliwa na ndiyo maana Wakuu wa Idara kadhaa tayari wameshachukuliwa hatua za kisheria na kinidhamu lakini aliyekuwa Mkurugenzi alishachukuliwa hatua za Kisheria na taratibu zinaendelea, pia tutaendelea kuchukua hatua kwa wote ambao watathibitika kuhusika kwa namna moja ama nyingine katika matumizi ambayo siyo sahihi ya fedha za Serikali. Kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge Serikali iko macho katika eneo hili na kazi inaendelea kufanyika na kuhakikisha kwamba tunatenda haki katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la upatikanaji wa dawa katika vituo vyetu. Kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa dawa umeendelea kuimarika lakini tunatambua bado kuna changamoto ya upungufu wa baadhi ya dawa muhimu na hususan dawa za matibabu kwa wazee lakini pia watoto chini ya miaka mitano na wakina mama wajawazito. Mpango wa Serikali, Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Afya tumeshaweka mkakakti wa kuainisha dawa muhimu ambazo zinatoka kwa wingi zaidi ili tuhakikishe kwamba dawa hizo zinapatikana kwa wingi kwenye vituo vyetu lakini tumeongeza orodha ya dawa zote muhimu kutoka 33 hadi 241, hii itasaidia kuhakikisha kwamba wananchi sasa wana wigo mpana wa kupata dawa katika maeneo hayo kuliko ilivyokuwa huko nyuma.

Mheshimiwa Spika, nihitimishe kwa kukushukuru sana na kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge na kuhakikishia kwamba Ofisi ya Rais, TAMISEMI tunakwenda kutekeleza haya yote kuhakikisha tunaboresha huduma kwa jamii.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)