Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema aliyetuwezesha sote kuweza kufikia hatua hii ambako hatimaye naweza kuhitimisha hoja hii ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa mwaka wa fedha 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, kipekee ninashukuru na ninakupongeza sana wewe binafsi, Naibu Spika na Wenyeviti wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri ambao umetuwezesha na umewezesha Bunge lako Tukufu kuweza kujadili hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Rais - TAMISEMI kwa weledi mkubwa sana. Aidha, nichukue nafasi hii kuweza kuwapongeza na kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote walioweza kuchangia hoja hii, takribani Wabunge 96 wameweza kupata nafasi ya kuweza kuchangia hoja hii, kwa kweli tunawashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hakika maoni na ushauri uliotolewa na Waheshimiwa Wabunge utatusaidia sana kuweza kupata mwelekeo wa kuweza kusimamia vizuri zaidi utekelezaji wa mpango wetu na bajeti kwa mafungu yetu yote 28 ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI hatimaye kuweza kuimarisha utoaji wa huduma zetu kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, nitakuwa sijatenda haki na nitakuwa mchoyo wa fadhila endapo sitaweza kuishukuru Kamati yetu ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa inayoongozwa na Mheshimiwa Dennis Lazaro Londo, Mbunge wa Jimbo la Mikumi pamoja na Makamu Mwenyekiti wake Mheshimiwa Nyamoga Mheshimiwa Mbunge wa Kilolo na Waheshimiwa Wajumbe wote wa Kamati kwa umahiri wao, kwa weledi wao na namna ambavyo wameendelea kushiriki katika kupendekeza na kutushauri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee napenda pia kuwashukuru Mawaziri wote ambao wameweza kuwa nami pamoja na wenzangu katika kuhakikisha kwamba tunaweza pia kuhitimisha hoja hii vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, kipekee pia napenda kuwashukuru Wabunge wote, lakini zaidi pongezi. Pongezi mlizozitoa, naomba sana zimrejee Mheshimiwa Rais Wetu Mpendwa, ambaye ndiye ametuwezesha sisi kwa maelekezo yake na msukumo wake kuweza kuyafikia yote haya tuliyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zaidi nashukuru kwa pongezi kwake mlizozitoa na kwa namna ambavyo nanyi pia katika mafanikio yote haya hayawezi kupatikana bila ninyi wenyewe Waheshimiwa Wabunge, Waheshimiwa Madiwani, Watendaji mbalimbali katika ngazi zote za msingi, lakini bila kuwasahau Waheshimiwa sana Wakuu wetu wa Mikoa, Wakuu wetu wa Wilaya, Wakurugenzi wetu wote wa Halmashauri, Makatibu Tawala wetu wote wa Mikoa na wa Wilaya. Kipekee nawashukuru sana Wenyeviti wetu wote wa Halmashauri pamoja na Mameya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile nitakuwa sijatenda haki endapo nitashindwa kuwashukuru Manaibu Waziri wangu kwa kazi kubwa ambayo wameifanya. Wameweza kuonesha uwezo na umahiri Mkubwa. Nampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Dugange kwa kazi kubwa ambayo amekuwa akiendelea kuifanya ikiwa ni pamoja na ufuatiliaji. Vile vile nampongeza na kumkaribisha tena Mheshimiwa Ndejembi, hata kwa leo mmeona kwa muda mfupi tu aliokaa Wizarani, namna ambavyo yuko mahiri na ana weledi mkubwa sana. Kwa kweli nawashukuru, na bila ya wao kwa hakika nisingeweza kuwasilisha hotuba hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile nitakuwa sijatenda haki nisipomshukuru Katibu Mkuu Ndg. Adolf Nduguru pamoja na Manaibu Katibu Wakuu wote, Dkt. Msonde, Dkt. Mahela pamoja na Dkt. Mtwale; Makamishina wote, Wenyeviti wote wa Bodi za taasisi zetu, na vile vile Watendaji Wakuu wa taasisi zilizoko chini ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Wakurugenzi wote, na wafanyakazi wote walioko chini ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI)na taasisi zetu. Kwa kweli nawashukuru sana kwa kazi kubwa. Kwa hakika nadhani wenyewe wamejionea maandalizi waliyoyafanya na wameweza kuona matokeo.

Mheshimiwa Spika, zaidi tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge. Endapo kuna sehemu tutakuwa tumewakwaza, tunawaomba radhi, haikuwa nia yetu, na tutaendelea mwaka hadi mwaka kuweza kuboresha ili kufikia viwango na matarajio ambayo mnayo katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, naomba nisitaje majina moja moja, maana yake nikisema yote 96 niweze kutaja, nitakuwa sijatendea haki muda wako. Napenda tu kufanya muhtasari kwa hoja takribani 16 za aina mbalimbali zilizojitokeza. Ipo hoja ya Uboreshaji wa huduma ya elimu Msingi na Sekondari; kulikuwa kuna hoja kuhusiana na kukamilishaji wa maboma ya elimu na utoaji wa huduma za afya msingi; miundombinu chakavu ya shule za msingi na uhaba wa matundu ya vyoo na madawati; uhaba wa nyumba za watumishi katika ngazi ya elimu msingi na afya msingi; uimarishaji na ubora wa huduma ya afya ngazi ya msingi; maoni mbalimbali kuhusu kuanzishwa kwa daraja jipya au kundi jipya ambapo Halmashauri 56 wamo kuhusiana na wao kuchangia kiwango cha asilimia 20 katika miradi ya maendelo kutoka mapato ya ndani yasiyolindwa; na uhitaji wa watumishi na utaratibu wa ajira.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ilihusu watumishi wanaojitolea; nyongeza ya posho ya Waheshimiwa Madiwani na Wenyeviti wa Vijiji na Mitaa; hitaji la ongezeko la bajeti kwa ajili ya wakala wetu wa wa TARURA; wingi wa miradi isiyokamilika na ubadhirifu wa fedha; kuongeza bajeti kwa ajili ya uendelezaji ya miundombinu ya barabara; utekelezaji wa ahadi za viongozi; uwezeshaji wa wananchi kiuchumi kupitia asilimia 10 ya mapato ya ndani; uimarishaji wa ukaguzi wa ndani; na ufuatiliaji wa tathmini ya miradi ya maendeleo na ufuatiliaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia hayo maeneo niliyoyabainisha, kwa uchache, napenda sasa kuchukua nafasi hii kuweza kutoa ufafanuzi wa hoja mbalimbali kama ambavyo zimetolewa na Kamati, na Waheshimiwa Wabunge katika kujadili Bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya Kamati kupitia Mheshimiwa Londo ambapo walituelekeza kuona ni namna gani tunaweka vipaumbele na hasa katika matumizi ya fedha hizi za uwajibikaji wa makampuni yenye leseni katika HakiMadini au CSR. Vile vile kabla ya kupokea kwa fedha hizo, alishauri tuangalie vipaumbele, na kuona ni kwa namna gani fedha hizi zinaweza kutumika na kufanya tathmini kuhusu maeneo yote ambayo yamenufaika na fedha hizi; na pia kuwa na mwongozo mzuri wa matumizi ya fedha hizi za CSR.

Mheshimiwa Spika, napenda tu kusema tunapokea ushauri na tunashukuru. Kwa kweli ni hoja ambayo wamekuwa wakiisemea kwa uzito wa kipekee na kwa kweli tumewaelewa na tunaiona hoja yao.

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa utoaji wa fedha hizi za uwajibikaji wa Makampuni ya Madini katika jamii, unaongozwa na sheria kupitia kifungu cha 105 cha Sheria yetu ya Madini na hasa kifungu kile kidogo cha (2) ambacho kinaelekeza kabisa, kampuni ambayo itakuwa na HakiMadini inatakiwa iandae Mpango wa Mwaka wa Uwajibikaji wa Kampuni katika Jamii. Pia inatakiwa iandae kwa pamoja na Halmashauri husika ambako shughuli zile za madini zinafanyika. Baada ya hapo, wanatakiwa wawasilishe kwa kushauriana na Waziri anayesimamia masuala ya TAMISEMI pamoja na Waziri wa Fedha na hatimaye kwa baadaye inaweza kuidhinishwa kwa utaribu mahususi.

Mheshimiwa Spika, napenda tu kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba tunaendelea, na wiki mbili zilizopita tumepokea Mpango wa Mwaka kwa upande wa GGM kwa Halmashauri ya Geita Mji na Geita yenyewe. Tunaendelea kusimamia hilo kwa karibu, na niwahakikishie kwamba Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Wizara ya Fedha na Wizara ya Madini tutaendelea kulisimamia suala hili kwa karibu sana.

Mheshimiwa Spika, tayari Wizara ya Madini imeanza kuandaa kanuni zinazosimamia suala zima la CSR, na vilevile sisi kama TAMISEMI tunaandaa Mwongozo mahususi utakaosimamia utekelezejai huu na lengo letu kubwa ni kuhakikisha kwamba tunaongeza tija katika miradi inayotekelezwa tukitambua kwamba CSR hii haitakuwepo milele, na kwamba shughuli za madini hazitakuwepo pale milele. Kwa hiyo, ni lazima pia miradi inayoibuliwa kama vipaumbele na Halmashauri husika iwe kweli ni miradi mizito na miradi yenye tija ambayo kweli itaweza kuacha alama na itakayokuwa na manufaa.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja nyingine ya Kamati katika upande wa mradi wetu wa Kuimarisha Elimu ya Sekondari (SEQUIP). Kwenye eneo hili tumekuwa tukitoa Shilingi milioni 470 kwa kuanzia kama awamu ya kwanza na awamu ya pili tunatoa Shilingi milioni 130 na tayari tumeshafanya ujenzi wa shule hizi katika maeneo mbalimbali na Majimbo yote mmeweza kupata, na tumeweza kujenga takribani Shule 231.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo tumeelekezwa na Kamati kuona ni kwa namna gani tunaweza kutafuta fedha zitakazoweza kuongezea kukamilisha majengo ambayo yatakuwa yalijengwa na hayajakamilika. Napenda tu kuwahakikishia Kamati na Waheshimiwa Wabunge kwamba Ofisi ya Rais, TAMISEMI tunaendelea kukamilisha tathmini ya kina ya gharama halisi zinazohitajika kukamilisha ujenzi wa shule hizo na pia kuweza kutafuta fedha zitakazoweza kukamilisha ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja pia ya gharama za vifaa vya ujenzi au gharama elekezi. Tumeanza. Tulianza na darasa moja kwa Shilingi milioni 20. Maeneo mengine ilikuwa katika ujenzi wa vyoo ni Shilingi milionI 1.1, tumeiboresha sasa hivi ni Shilingi milioni 2.1. Katika madarasa, tumeboresha kikanda. Katika kanda saba tumefanya mapitio. Ukiangalia kuna maeneo mengine kutoka Shilingi milioni 20 tumepeleka Shilingi milioni 22 mpaka Shilingi milioni 26.

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa hoja ya Mheshimiwa Mkundi, Mbunge wa Ukerewe, lakini pia maeneo mengine kama ya Mafia, visiwa vya Goziba, Muleba na kwingineko.

Inawezekana pia bado kwenye moja, kwa mfano, Dar es Salaam ni kanda kweli ya Pwani, lakini ukiangalia Dar es Salaam na Pwani yenyewe inaweza ikatofautiana gharama. Pwani yenyewe pia, ukiangali Kibaha, Bagamoyo haiwezi pia kufanana na Mafia wala Rufiji kwa upande wa Delta. Kwa hiyo, pia na Ukerewe tunaipokea na tutaendelea kuifanyia kazi vizuri, lakini walau tumetoka katika hiyo 20 tunakwenda katika hiyo 22 mpaka 26 katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, yote hii ni michango yenu Waheshimiwa Wabunge, ndiyo imetuwezesha pia kuweza kufanya mapitio na marejeo ya gharama hizi. Tunawashukuru.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja nyingine ya suala zima la umuhimu wa upembuzi yakinifu. Tunaliona na hasa hufanywa kabla ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo. Ni kweli Kamati ilienda Mwanza kuangalia soko. Ukiangalia katika aina ya udongo ni lazima ufanye due technical investigations, tunaona na tunambua na tunashukuru kwa maoni yale. Vile vile tunaendelea kuweka umuhimu wa kuwa na hitaji la kufanya upembuzi yakinifu kabla ya kuweza kutekeleza miradi hii ili kuhakikisha kwamba miradi inavyotekelezwa inakuwa ni miradi ambayo haina changamoto mbalimbali na inakuwa kweli imezingatia maeneo husika lakini pia imeweza kuzingatia vigezo vyote vya kiutalaamu na kuhakikisha kwamba kweli tunawajengea timu zetu za Halmashauri uwezo na utaalamu mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya matumizi au uwepo wa fedha ya bakaa. Mwaka wa fedha unaisha, lakini bado unajikuta miradi haijakamilika na fedha nyingine hazijatumika. Kwa mujibu wa Waraka Namba (1) wa Hazina, ukiangalia katika kipengele cha 4.3 kimeelekeza vizuri zaidi ni namna gani mwaka wa fedha unapoanza, mara tu baada ya bajeti kukamilika, inatakiwa wale ambao wamenufaika au wameelekezewa fedha za miradi wanatakiwa waziombe.

Mheshimiwa Spika, fedha za miradi ya maendeleo haziji tu. Baada ya kupitisha hapa kwenye Bunge. Mamlaka zote za Serikali za Mitaa hazitakiwi kukaa, zinatakiwa zipeleke maombi. Mikoa yetu haitakiwi kukaa, inatakiwa ipeleke maombi, na vile vile Ofisi ya Rais, TAMISEMI kama walivyo wanufaika wengine wa bajeti, hawatikiwi kukaa, ni lazima waziombe Hazina. Hazina hawawezi kukuletea fedha bila wewe kuziomba.

Mheshimiwa Spika, sasa tumezielekeza Ofisi zetu za Mikoa kuhakikisha wanaunganisha maombi yote kutoka katika Mamlaka zetu za Serikali za Mitaa kupitia kila Halmashauri. Tunapoanza Julai mosi, tunaziwasilisha kwa Katibu Tawala wa Mkoa ambaye atapeleka kwa Wizara yetu ya Fedha akiwa na maombi na mchanganuo wote wa fedha wa Mkoa husika na Halmashauri zake ili kuhakikisha kwamba Hazina wanapata nafasi ya kufanya uchambuzi wa kina na makini. Lengo ni kuhakikisha kwamba Hazina wanatuletea fedha mapema na kwa wakati, na ziweze kutoa muda wa kutosha pia na nafasi, ili kuwa na utekelezaji mzuri na wenye ubora wa miradi yetu. Badala ya kuletewa fedha mwezi wa Nne, mwezi wa Tano, na hapo una mradi wa maendeleo, mwingine ni wa ujenzi, kwa hakika ni lazima hela itabaki na utakuwa na bakaa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kuanzia Julai mosi, na niliwambia mikoani tutaendelea kuwapima na hiki kitakuwa ni kigezo, nani amewasilisha, nani hajawasilisha? Ulipata lini? Endapo ulipata mapema na hujaweza kukamilisha mradi kwa wakati, kwa hakika ni lazima watakwenda na maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa pia kuna hoja ya kufanyia maboresho Sheria ya Matumizi ya Fedha za Umma ambazo kwa mfumo na muundo na hasa katika majukumu ya Serikali za Mitaa ni lazima Sheria hii ya Fedha iangalie kwa majukumu yake. Serikali kuu namna ambavyo wanatumia fedha na muundo wake hauwezi kufanana na Serikali zetu za Mitaa. Kwa hiyo, na yenyewe pia tutawasilisha Wizara ya Fedha. Tunapokea ushauri huu mzuri ili kuweza kuona ni kwa namna gani suala hili pia linaweza kutatuliwa.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya kumalizia maboma yaliyoanzishwa kwa nguvu za wananchi ili kuondoa hasara inayoweza kupatika. Kwa kweli kwenye hili nawashukuru sana wananchi wa maeneo mbalimbali kwa namna ambavyo wamejitolea. Zaidi nawashukuru pia Waheshimiwa Wabunge kupitia Mifuko yenu ya Majimbo, mmeweza kuunga mkono na kuweza kupeleka fedha kuhakikisha kwamba majengo haya yanamalizika na kuwa na ubora. Siyo hivyo tu, mmetoa hata fedha zenu binafsi na wadau wengine mbalimbali. Kwa hakika kwa niaba ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, nawashukuru wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha uliopita, miaka miwli 2020/2021 na 2021/2022 tuliweza kutenga kama Serikali takribani Shilingi bilioni 280.35 ambazo zimetumika kumalizia maboma ya madarasa, mabweni, mabwalo na vituo vya afya kama 52 pamoja na zahanati zaidi ya 1,419. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba, kwa mwaka huu wa 2023/2024 tumeweza pia kutengewa fedha takribani Shilingi bilioni 20.56 ambapo tutaweza kukamilisha maboma ya zahanati zaidi ya 376, mabweni 10 pamoja na miundombinu mingine mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kushirikiana na mikoa yetu na Halmashauri tumefanya tathmini ya mahitaji halisi ya maboma ambayo hayajakamilishwa pamoja na yale yanayoendelea kujengwa kwa upande wa afya na elimu ili kuweza kuyawekea mkakati wa kuyakamilisha.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna hoja ya Kamati pia kuona kuna umuhimu wa watendaji wetu wa kata kuweza kupata mafunzo ya awali kuhusiana na utumishi wa umma, masuala ya usalama, masuala ya huduma za kijamii ni namna gani wanatakiwa waenende na wawe taswira katika jamii zetu ili kuhakikisha kwamba wanakuwa na uwajibikaji mzuri zaidi katika ngazi zetu za vijiji na kata. Napenda kuihakikishia Kamati na Waheshimiwa Wabunge kwamba katika Bajeti hii 2022/2023 inayomalizika Juni, tumetenga fedha na tutahakikisha kwa kuanzia, tutaanza na mafunzo kwa Watendaji wa Kata 1,936 na tutaendelea kutoa mafunzo hayo pia kwa awamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna hoja kuhusiana na mradi wa KKK wa Kupima, Kupanga na Kumilikisha ambapo Halmashauri zetu zilitengewa takribani Shilingi bilioni 49.47.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, napenda tu kuwaambia kwamba fedha nyingi zilielekezwa katika kupima viwanja na tuliweza kufanikisha upimaji kwa takribani ya asilimia 91.37. Hadi kufikia mwezi Februari mwaka 2023 tumeweza kurejesha takribani shilingi bilioni 16.75, kati ya fedha iliyotolewa ambayo ni asilimia 33.85. Pia tumetoa ukomo kwamba ifikapo tarehe 31/10/2023 ni lazima fedha hizi zote ziwe zimerejeshwa Serikalini, na vile vile kuhakikisha kwamba zinazopatikana basi haziwi sehemu ya mapato ya ndani ya Halmashauri na badala yake ziwe ni sehemu ya fedha za mradi unaojitegemea, na zirejeshwe katika utekelezaji na uendelezaji wa mradi huo wa Kupima, Kupanga na Kumilikisha.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja pia ya kuendelea kuzijengea uwezo Halmashauri zetu katika kuandaa maandiko ya miradi ya kimkakati ya kuona ni kwa namna gani tunafanya tathmini ya marejeo ya mapitio ya mwongozo wa miradi ya kimkakati ili kuona sasa katika mwongozo tulionao sasa tunautatua vipi?

Mheshimiwa Spika, napenda kuliarifu Bunge lako kwamba tumeendelea kufanya zoezi hili, tunashirikiana na Wizara yetu ya Fedha na Mipango pamoja na taasisi ya UNCDF na tayari tunayo tume au timu ya kitaalamu ya kitaifa kwa ajili ya kujenga uwezo wa Mikoa yetu na Halmashauri na hasa katika suala zima la uandishi wa miradi ya kimkakati. Tayari tumeanza kutoa mafunzo katika timu zetu za kitaifa, ambayo yameshirikisha watendaji wa Mikoa na Halmashauri, na tayari takribani Mafisa zaidi ya 281 wameshapatiwa mafunzio hayo katika Mikoa na Mamlaka zetu za Serikali za Mitaa, wakiwemo Makatibu Tawala Wasaidizi wa sehemu ya Mipango na Uratibu katika mikoa yote 26.

Mheshimiwa Spika, vile vile, tunaendelea kutekeleza maelekezo ya Kamati ya kufanya marejeo ya vigezo vya Mwongozo wa Miradi ya Kimkakati ili kuona ni kwa namna gani tunahuisha vigezo hivyo na kuziwezesha pia Halmashauri zetu nyingi zaidi kuweza kukidhi vigezo hivyo kwa ajili ya kutekeleza Miradi ya Kimkakati.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya TARURA kutokuwa na ofisi za kutosha. Ni kweli; tayari wameshaanza mkakati wa kujiandaa kuendelea kupata viwanja katika Halmashauri zetu, na vile vile mkakati wa ujenzi kuhakikisha kwamba Ofisi zote za TARURA zinamilikiwa na TARURA yenyewe.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya upungufu au changamoto ya ukosefu wa magari. Mpaka sasa TARURA ina magari takribani 282 na kati ya hayo tumeendelea kununua 245 tayari tumeshayapokea na mengine tumeshaanza kuyagawa. Hadi sasa upungu wa magari tulionao ni takribani magari 177. Kama Serikali tumeendelea kuyapangia bajeti. Nimhakikishie Mheshimiwa Shangazi, TARURA Wilaya ya Lushoto itapewa kipaumbele katika magari ambayo tunayasubiri, lakini vile vile tutaangalia na Wizara nyingine.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya kaka yangu Mheshimiwa Deo Sanga Mzee wa Mabii na Matrilioni. Kwa upande wa soko lao la Kituo cha Mabasi ya Makambako, nimhakikishie kwamba Halmashauri yetu ya Makambako ni moja ya Halmashauri ambazo zitanufaika na Mradi wa TACTIC ambao unanufaisha Miji, Majiji na Manispaa 45. Kwa upande wetu wa Makambako, tumeitenga katika awamu ya tatu ya TEA III lakini kubwa niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge wote, kabla ya 2025 mradi huu utakuwa umekwishaanza kwa hatua mbalimbali kwa namna moja au nyingine.

Mheshimiwa Spika, nami pia ni mwanasiasa ndugu zangu, siwezi kukubali suala hili likapita kipindi hicho ukikaribia uchaguzi, halafu miradi hii haijaanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kubwa niwatoe hofu, lazima hili litaanza. Iwe iwe mvua, iwe jua, iwe nini tutahakikisha hili inatekelezeka. Lakini pia Mheshimiwa Rais amenielekeza kulisimamia suala hili kwa karibu zaidi, na tarehe 15 mei tunaanza kutangaza kuna baadhi ya zabuni kwa ajili ya usanifu zitaanza kufanyika, na tunaamini ndani ya muda mfupi sana mtaweza kuona mambo mengi zaidi yakifanyika kwenye mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya Mheshimiwa Rashid Shangazi na wengine, kwamba fedha zinazotolewa na Mfuko wa Barabara zinachelewa kutolewa na matokeo yake imesababisha baadhi ya wakandarasi kutoomba zabuni za utekelezaji wa barabara. Nipende tu kumwambia Mheshimiwa Shangazi na Waheshimiwa wengine, kwamba Ofisi ya Rais TAMISEMI tunapokea ushauri na tutafuatilia ili kuhakikisha kwamba fedha hizi zinatolewa mapema zaidi na kwa wakati. Wizara ya Fedha imekuwa ikijitahidi kuweza kuzitoa mapema. Tutaendelea kuona ni kwa namna gani wataongeza kasi zaidi.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya DMDP; Mheshimiwa Bonnah Mheshimiwa Chaurembo Mheshimiwa Jerry Silaa na wengine wote wa Dar es Salaam. Ni kweli tunatambua Dar es salaam bado kwa kiasi kikubwa ina miundombinu mibovu, lakini nipende kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge na wenzake, kwamba Ofisi ya Rais, TAMISEMI tunatarajia kuanza utekelezaji wa BMDP awamu ya pili, na halmashauri zote tutaanza Dar es salaam zitanufaika na mradi huo ambao utajumlisha ujenzi wa miundombinu ya barabara, mifereji mikubwa ya barabara, ya maji ya mvua, madaraja na miundombinu ya usimamizi wa taka ngumu. Hadi sasa mradi uko katika hatua za mwisho za kupata wataalamu washauri wa usanifu wa miundombinu ya kipaumbele; lakini pia kuweza kuandaa nyaraka muhimu zikiwepo za masuala ya kijamii, mazingira pamoja na mengine.

Mheshimiwa Spika, tunaendelea kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha kufanya mashauriano na majadiliano ya mwisho na Benki ya Dunia, lakini hiyo haizuii hatua zingine kuendela. Kama tulivyoeleza zaidi ya asilimia 36 ya miradi ambayo imekusudiwa usanifu wake unaanza na tayari tunakusudia gharama yake itahusisha kama takribani kilomita 174 katika utekelezaji wa mradi.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya Mheshimiwa Chaurembo ya kuunganisha barabara nyingi za Dar es salaam kutoka eneo moja na lingine ili kuona ni kwa namna gani tunapunguza msongamano. Nimshukuru kwa hoja hiyo na nimhakikishie kwamba tunapokea ushauri na tutatumia vyanzo mbalimbali vya fedha ili kujenga barabara za kuunganisha sehemu mbalimbali za mkoa wa Dar es salaam na kupunguza msongamano. Tumefanya hivi kupitia mradi wa DMDP wa awamu ya kwanza na tuatafanya hivyo na DMDP wa awamu ya pili na DART katika halmashauri zote za Mkoa wa Dar es salaam na katika miradi ya ujenzi wa barabara zinazotumia fedha za ndani.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya Mheshimiwa Chumi kuhusuiana na kuona ni namna gagi tunasaidia haswa wakandarasi wa ndani kwa kuwajengea uwezo au pia hata kuona namna au umuhimu wa kuwapa udhamini ili waweze kupata mikopo ya mitambo; lakini pia kuona ni kwa namna gani TARURA kila kanda itakuwa na mitambo yake ambayo itakuwa inakodishwa kwa wakandarasi na baadaye wakandarasi wetu hawa wazawa waweze kukatwa kutokana na malipo. Nipende kusema tu kwamba tunapokea ushauri huu, Serikali itafanya tathmini ya pendekezo hili kabla ya kuanza kulitekeleza.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya hospitali kongwe katika mamlaka zetu za Serikali za Mitaa na kwamba zimechakaa, sana na zinahitaji kufanyiwa ukarabati. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tayari kwa mwaka huu tnaoumalizia tulitenga zaidi ya shilingi bilioni 16.65 na tumeweza kukarabati zaidi ya hospitali 19. Lakini katika mwaka ujao wa fedha tutakarabati takribani hospitali kongwe 31, na tumeshazitengea takribani shilingi bilioni 27.9.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya magari ya wagonjwa. Niwape habari njema Waheshimiwa Wabunge wetu; tuliagiza magari 527; na nipende kusema ilikuwa yawe ni magari 407 lakini kwa uzarendo na kwa kushirikiana na Wizara yetu ya Afya na UNICEF, badala ya kupata magari 407 kwa mbinu tulizozitumia tutapata magari 528. Kwa hiyo tumeokoa zaidi ya magari 121 ambayo endapo tusingetumia utaratibu huu hayo magari yasingepatikana. Kwenye hili Waheshimiwa Wabunge kila halmashauri itapata magari mawili ya kubebea wagonjwa na itapata gari moja kwa ajili ya suala zima la usimamizi na uratibu wa miradi ya afya katika halmashauri zao. Kwa hiyo kwenye hili naulizwa na Mheshimiwa Hawa Mwaifunga hapa ni lini; nimpe habari njema nafuatilia kwenye simu bill of lobing tangu tarehe saba magari yameshafika bandarini. Yako yaliyofika tarehe 14 na yako yanayoingia tarehe 21, na vivyo hivyo mpaka tumalize magari 528. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa yaliyo katika ukomboaji ni magari 55, hardtop kadhaa taktiban 30 na ambulance 25 tayari zimeshaanza kukombolewa; lakini kubwa kuliko yote kila mmoja atapata kwa ajili ya kuhudumia wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya suala la hospitali mbalimbali; kwa Muleba, Mbulu na kwingineko. Niwahakikishie Mheshimiwa Mwijage, Mheshimiwa Massay na wengine wote, kwa zile fedha za vituo vya afya ambazo zilikuwa hazijapelekwa tutahakikisha fedha hizo zinapelekwa kwa wakati ili kuendeleza miradi iliyoanza lakini vilevile kwa ile ambayo ilikuwa haijaanza; yote tuliyoahidi fedha hizo zitapelekwa.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya shule za msingi kuchakaa hali ambayo hata imepelekea mdondoko wa wanafunzi wetu na kupunguza ufaulu. Nipende kuwahakikishia kuwa tayari kupitia mradi wetu wa kuimarisha elimu ya awali na msingi kupitia BOOST tumetenga shilingi bilioni 230 kupitia maelekezo ya Mheshimiwa Rais kati ya sasa, Aprili na Juni bilioni 230, hapo vipi? Na mmeona wenyewe barua, si maneno, na tayari wiki hii fedha hizo tutaziwasilisha katika halmashauri zenu. Kubwa ninalowaomba Waheshimiwa Wabunge na viongozi wengine, nawaomba; kwa kuwa mradi huu wa bust ni wa lipa kwa matokeo, itakapofika tarehe 30 juni ni lazima fedha hizo bilini 30 kila mmoja kwenye jimbo kadri alivyopangiwa basi ni lazima ziwe zimekamilika na ujenzi uwe umekemilika na matokeo yaweze kuonekana. Tukija mwezi julai baada ya kufanya mapitio na tathmini kadri utakavyokuwa ume-deliver fedha nyingine zaidi zitaweza kujitokeza katika mwaka ujao wa fedha.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya walimu waliomaliza vyuo wapewe mwaka mmoja wa kujitolea kabla ya kuajiriwa, tunapokea ushauri. Serikali inaendelea kufanyia kazi suala hili ili kuweza kupata mwongozo wa utekelezaji wake.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya Mheshimiwa Mussa Sima lakini vilevile illikuwa ni hoja ya Ndugu yangu Mheshimiwa Sekiboko, na nitaomba kidogo hii niisemee. Jukumu la Wizara ya Elimu ni pamoja na kutengeneza Sera ya Elimu Mitaala, Sheria ya Elimu na mitaala yetu iweje pamoja na Mihutasari jukumu la Ofisi ya Rais TAMISEMI kama mtekelezaji ni kusimamia utekelezaji ili umahiri wa watoto wanotarajiaa waupate waweze kuupata. Lengo letu ni kumtengeneza mwanafunzi awe na ile sura kama ambavyo wizara ya imetuelekeza.

Mheshimiwa Spika, na Sera yetu ya Ugatuaji wa Madaraka iko wazi kabisa; Wizara ya Elimu inafanya nini mpaka wapi, Ofisi ya Rais TAMISEMI inafanya nini mpaka wapi hatuwezi kuwa na shule tukazisimamia halafu tukasema sisi tuna majengo tukaacha, hilo halitawezekana na liko wazi kabisa. Kwa hiyo nipende kusema tu kwa lugha nyepesi sana Wizara ya Elimu ni msanifu halafu Ofisi ya Rais TAMISEMI sisi sasa tunajenga kile tulichoelekezwa kusanifu mtoto wa Kitanzania.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja katika mkataba wa utendaji kazi au performance contract, kwamba zimewasumbua walimu na mambo mengine kadhaa wa kadhaa. Nipende kusema, kwamba tulijipangia makataba wa kuboresha elimu nchini ambao umepitishwa mwezi wa nane mwaka jana ambao ulizinduliwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu; na Katibu Mkuu Naibu Katibu Mkuu wa Elimu ambaye kwa sasa ndio Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu pia alishiriki kama Mgeni Rasmi katika hatua moja wapo wakati mkutano huu.

Mheshimiwa Spika, tulichokifanya katika mkataba wa utendaji kazi ni kutafsiri ule mkakati wetu wa kuboresha elimu Tanzania. Kwamba tunataka elimu ya aina gani katika msingi na sekondari. Yako majukumu ambayo tumewapatia walimu wetu. Mwalimu ana jukumu la kujenga umahiri na stadi mbalimbali kwa ajili ya watoto wetu, hawezi akaachwa hivi hivi, kwa hiyo hakuna kipya kilichofanyika. Tumeangalia mdondoko wa ufaulu, tumeutafsiri, ni lazima na sisi kama Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu tuje na mkakati; na ndio maana tukaja na ule mkakati.

Mheshimiwa Spika, kwenye hili mtaona maafisa wetu wa elimu wilaya na mkoa pia hawakai ofisini, wanatoka huku na ule kuhakikisha kwamba kila wiki wanaenda kukagua katika shule zetu ili kujiridhisha na kile ambacho kinafundishwa katika shule zetu. Lengo kubwa ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na uimara katika stadi ambazo tunataka kweli wanafunzi wetu wapate; na kubwa tuliangalia zile changamoto, tuliangalia dosari mbalimbali zilizopo nza kuhakikisha kwamba tunaqweza kuzirekebisha.

Mheshimiwa Spika, moja ya mafanikio ya haya, huku nyuma kulikuwa kuna changamoto pia hata katika kiwango cha uandikishwaji, lakini kwa sasa kupitia mkataba huohuo wa utendaji kazi unaosemwa na mkakati wa uboreshaji wa elimu walau katika elimu ya awali tumeweza kufikia uandikishwaji wa awali asilimia 109, na hata tumeweza kuvuka hata lengo lilokuwa limepangwa.

Mheshimiwa Spika, kwa darasa la kwanza uandikishwaji ni asilimia 108 na kwa upande wa kidato cha kwanza tumeweza kufikia asilimia 93. Mkakati huu pamoja na mkataba huo wa utendaji kazi ndio umetewesha kuweza kufikia mafanikio hayo ndani ya muda mfupi sana. Kwa hiyo nipende tu kusema kwamba hakuna kikubwa katika mkataba huo wa utendaji kazi. Wadau wote wa elimu wana majukumu; kama wazizi wana majukumu yao kama wanafunzi wana majukumu yao, walimu wana majukumu yao, jamii ina majukumu yake; lakini na mwalimu naye jukumu lake kubwa ni kujenga umahiri katika mazingira ya watoto wetu. Kwenye eneo hilo niliona niliwekee mkazo kidogo ili kuonesha kwamba kwanza hakuna kitu kipya. Lengo letu kubwa ni kuhakikisha tu kwamba tunaborsha kiwango chetu cha elimu.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya ajira watendaji wa vijiji, kwamba haitoshi. Nipende tu kuwakikishia Wabunge wetu kwamba tutaendela kuajiri. Kwa sasa tuna upungufu wa watendaji wa kata 262, kwa upande wa mtaa tuna upungufu wa watendaji wa mtaa 2,864, lakini vilevile kwa upande wa vijiji nako kuna upungufu wa watendaji wa vijiji 1,773. Kama Serikali tutaendelea kuajiri watendaji wa kata vijiji na mtaa kulingana na namna Serikali itakavyoendelea kupata fedha.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya halmashauri nyingi kukosa wahandisi ambao wamekuwa hawapo kwa ajili ya kusimamia miradi. Nipende kuwaambia Waheshimiwa Wabunge kwamba tayari Mheshimiwa Rais ameshaelekeza tupate kibali cha watumishi takribani 250 wahandisi 100 wakadiriaji majengo 100 na vilevile maafisa manunuzi 50. Lengo letu kubwa ni kuona ni namna gani watumushi hawa wapya wataweza kusimamia shughuli za ujenzi wa miradi inayotekelezwa ili kuimairisha tawala zetu za mikoa lakini pia kuhakikisha tunakuwa miradi ya maendeleo ambayo ina kidhi vigezo.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ambayo ilikuwa ina wachangiaji wengi sana, kuhusiana na walimu wanaojitolea wapewe kipaumbele katika ajira. Kwenye hili naomba unilinde kidogo endapo dakika zitakata basi walau kuna hoja kama mbili na nyingine moja ikikupendeza basi walau kidogo kunipa upendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye hoja hii kwanza niwashukuru Wabunge kwa kulileta, lakini la pili niseme kwamba tunatambua uwepo wa walimu wanaojitolea kufundisha katika shule za msingi na sekondari katika mamlaka zetu za Serikali za mitaa. Uwepo wa walimu hawa umesaidia sana kuweza kupunguza changamoto ya uhaba wa walimu katika baadhi ya shule za msingi na sekondari nchini.

Mheshimiwa Spika, nipende tu kuwatahadharisha au kuwajulisha Waheshimiwa Wabunge kwamba hadi sasa hatuna mfumo ulio rasmi unaotumika kuwatambua na kuwa na taarifa za walimu wanaojitolea. Hivyo basi kwa sababu hii baadhi ya walimu na hata kwa upande wa sekta ya afya wamekuwa wakipata nafsi ya kujitolea kweli lakini wapo wengine ambao walitamani wazipate pia lakini hawajawahi kuzipata nafasi hizi. Wamekuwa wakikosa nafasi katika shule lakini vilevile katika vituo vya kutolea huduma za afya ambako kuna mahitaji hayo. Kukosekana kwa mfumo au utaratibu huo ulio rasmi na uliowazi bado unaweka ombwe kati ya walimu na watumishi wengine wa sekta ya afya waliohitajika kujitolea kupitia uongozi wa shule au kupitia uongozi wa kituo cha kutolea huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, hivyo basi tunaandaa utaratibu mahususi na maalumu wa kuweza kutumia mifumo yetu ya kielektroniki kupitia Wizara yetu ya Afya, tunashirikiana pia na Wizara ya Elimu; tuone ni namna gani, kwa mfano upande wa sekta ya elimu; hivi waombaji wataomba vipi, kanzidata itakuwa vipi, hawa walimu wanaojitolea katika shule zetu watakuwa na utendaji wa aina gani na watafuatiliwaje, na taratibu zingine kadhaa wa kadhaa. Nipende tu kusema baadhi ya mnaeneo unaweza ukaangalia, labda Kinondoni, waombaji ambao wameomba katika sekta ya afya 150 lakini unakuta wengine pia haukuwa wazi labda wamepata 50 tu au 100.

Mheshimiwa Spika, kwenye hili tuwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, kwamba katika mchakato huu tulionao sasa kwanza tutaanza na ajira za 2015 waliomaliza shule mwaka 2015; na tunaangalia maeneo matatu tu vigezo vyetu vikubwa. Kwanza mwaka wa kuhitimu, la pili kwa elimu ni masomo, na kwenye hili labda niliweke wazi ni masomo ya aina gani inawezekana wengine hawayajui, ni masomo ya sayansi, ukiangalia fizikia, chemistry, biology lugha ya kiingereza lakini pia English in literature na wale wataalamu wetu wa ufundi katika maabara zetu za sayansi.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hilo tutaanza kwanza na mwaka wa kuhitimu. Na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, na kwenye hili kwa kweli niwaondolee lawama zote Waheshimiwa Wabunge, wala wananchi wenu wasiwahukumu kwamba labda hukumsaidia mtu au lolote. Mimi niwape comfort, binafsi hata katika vigezo vyote mpaka kufika hapa tulipofika na mimi mwenyewe na Manaibu wangu na uongozi mzima wa wizara tumekuwa karibu hatua kwa hatua. Lakini sisi pia ni viongozi, hatutataka kuharibu au kuchafua majina yetu; tutahakikisha kwa nguvu zetu zote tunasimamia kuhakikisha kwamba zoezi hili linafanyika kwa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mtakubaliana na mimi hata wengine wakinitumia zingine meseji hata sizijibu. Wako hata viongozi ambao wamenipigia simu na nimesema siangaliii kiongozi siangalii nani ni nani, tunatenda haki. Kwa sababu tusipofanya hivyo ndugu zangu mtu asiyemjua mtu tutajenga taifa ambalo huko mbele tutapata shida sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi mwenyewe binafsi nami ni mwanasisasa yako maeneo ninakotoka wako wengine ni ndugu zangu nimewaambia nenda kwenye mfumo na wala sihitaji hata kupata cheti chako; nenda kwenye mfumo. Kwa hiyo nataka kutoa comfort leo hii jioni tarehe 18 haki itatendeka. Na hata juzi na jana nimerejea tena kwa watendaji Ofisi ya Rais TAMISEMI, kama hata kulikuwa kuna chembe ya aina yoyote ya kutoaminika kwa mtu kwenye eneo hili kuna watu watakwenda na maji, kwenye eneo hili kuna watu watapata mashtaka ya jinai, na ndiyo maana kila hatua unavyoona nikitangaza matangazo nawaambia jamani watu wasitapeliwe watu, wasiahidiwe fedha kwa sababu atakayestahili ndiye atakayepata lipo jopo linalopitia na hata mimi mwenyewe nimewaambia tunafunga matangazo tarehe 25, tarehe 27 baada tu ya muungano mimi mwenyewe nitaenda pia kwenye mfumo kuona mchakato ulivyofanyika na jina kwa jina.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungmzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri dakika mbili malizia.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwenye hili nimeona nieleze kwa kina na ni vivyo hivyo kwa watendaji wengine wa afya katika suala zima la ajira hizi.

Mheshimiwa Spika, kwa dakika nikuombe kwenye ile hoja ya makundi ya zile halmashauri 56 ambazo zimewekwa katika halmashauri kundi la asilimia 20. Walikuwa wanatakiwa kutoa asilimia 40 ya mapato ya ndani yasiyolindwa lakini sasa wamewekwa katika asilimia 20.

Mheshimiwa Spika, niwashukuru Wabunge waliochangia hoja hii na wamechangia kwa hoja nzito. Ninipende kuwatoa hofu, lengo la Serikali limekuwa ni zuri. Tuliwaweka kwenye asilimia 20 kutokana kwamba uwezo wa halmashauri haulingani. Ziko halmashauri ambazo zingine hazikuweza kupeleka hata yale mapato ya mikopo ya asilimia 10, wamepeleka asilimia saba, hawakufikia asilimia kumi. Wako ambao katika miradi ya maendeleo badala ya asilimia 40 wamepeleka asilimia 33 na hata pungufu.

Mheshimiwa Spika, pia wako ambao hata walipelekea kuto kulipa stahiki sahihi za madiwani. Lakini si hilo tu wakati wa hitimisho la kazi na Waheshimiwa Madiwani kwa mwaka 2020 ziko halmashauri zaidi ya 20 bado kuna deni la shilingi bilioni 3.05 ambazo madiwani walikopa walikuwa wnatakiwa kukatwa na halmashauri lakini halmashauri hazikuweza kuwakata zingine kwa sababu ya madeni mbalimbali na hatimaye sasa hivi tunajikuta TAMISEMI na Serikali tunaubeba mzigo huu, na tumeshindwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, lengo letu ilikuwa ni kuwapunguzia mzigo halmashauri zile 56 ili walau waweze kuapata unafuu lakini tumewasikia wamelisema kwa hisia za kipekee suala hili. Sisi tuwaombe wabaki kwenye hiyo 20 lakini endapo bado wanaona kuna haja basi tutaendelea kushauriana ndani ya Serikali na Wizara ya Fedha na Serikali kwa ujumla wake. Ili kuweza kuona sasa ni nini kifanyike warudi tena kwenye asilimia 40 au wawekwe katika kundi la asilimia ngapi.

Mheshimiwa Spika, lengo letu lilikuwa ni kuhakikisha kwamba tunawapunguzia mzigo ili shughuli mbalimbali za kuendesha halmashauri ziweze kwenda vizuri. Stahiki mbalimbali za viongozi wa kisiasa katika halmashauri zao na watumishi wa umma ziweze kwenda vizuri lakini na wao pia waweze kutekeleza majukumu mengine kama ambavyo wamekasimiwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nikushukuru kwa nafasi lakini zaidi niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa namna walivyochangia hoja yetu na kwa kuzingatia maeneo hayo, niwashukuru sana na nipende kuseme naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, naafiki.