Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Kwanza niungane na wenzangu wote kumshukuru Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote niipongeze Serikali kuna kazi nyingi sana zimefanyika katika Jimbo la Mbulu Mjini, kazi kubwa ambayo ilikuwa imeshindikana kwa muda mrefu. Aidha nichukue nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa sababu kabla ya wakati huu kulikuwa na miradi ambayo ilishindikana kwa muda mrefu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue pia nafasi hii kuiopongeza Serikali kwa kazi kubwa iliyofanyika na naomba nichukue nafasi hii kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii. Kwanza Jimbo la Mbulu Mji Manyara kule lina sura mbili, kuna Vijiji na Mji. Eneo la vijiji ni Kata 10 eneo la Mji ni Kata Sita, katika hali kama hiyo kuna changamoto kubwa sana hasa kwenye upande wa watumishi. Wakati tunagawanyika mwaka 2015 Halmashauri ya Mbulu Mji ilipokea asilimia 40 ya watumishi, hadi tunapoongea sasa hivi hatujapata hata kujaza zile asilimia ambazo zilipungua kulingana na Mji kupokea asilimia 40 kwa 60. Kwa hiyo, tumeomba mara nyingi ajira za ujazaji ukiacha hizi ajira mpya.

Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu ni mkubwa sana. Kwa mfano, kwenye eneo la Watumishi wa Kilimo wako Watatu badala ya 54. Katika hizo Kata za Vijijini kuna Vijiji 34. Katika Vijiji 34 vilivyoko watumishi hawa wa kilimo na mifugo walikuwa muhimu sana, kuna upungufu wa watumishi 54 wa kilimo na watumishi 52 wa mifugo, ukijumlisha ni watumishi 100.

Mheshimiwa Naibu Spika, kilio changu ni kwamba nimeenda Wizara ya Utumishi mara nyingi, bahati mbaya

Mawaziri wamebadilika lakini ofisi ni ile ile. Nikitetea walau hizi nafasi za ujazaji zijazwe ili wananchi wangu wapate huduma bora kulingana na upungufu huu wa watumishi. Hizi ni kada mbili tu zina upungufu wa watumishi 100 sijaenda kwenye kada zingine. Mfano mwingine ni Vijiji na Mitaa tulizogawiwa 2014, kulikuwa na mahitaji ya Watendaji wa Vijiji na Mitaa zaidi ya 94 hadi sasa wamejaza nafasi za 30 tu na kila unapoenda unaahidiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu au hoja ya msingi zaidi ni kwamba hata yule aliyestaafu mshahara wake anapokea nani? Mheshimiwa Waziri kama alistaafu yuko kwenye mshahara na mshahara wake pengine ulikuwa unaweza kuajiri hata watumishi watatu, wanne, kwa maana ya yeye anaweza akawa anapokea zaidi ya Milioni Moja na watumishi wapya wanaoajiliwa kwa kada tofauti tofauti wanaweza kuajiliwa mpaka Watatu kwenye nafasi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu hapo ni kwamba hatuangalii data zetu kwa umakini na maeneo gani yanaathirika sana. Ukizungumza Maafisa hawa ambao ni ngazi za Kata na Vijiji wakakosekana moja kwa moja uwezo wa utendaji wa Serikali na utoaji wa huduma kwa Serikali unapungua kwa asilimia kubwa sana. Kwa hiyo, nilikuwa naona wakati fulani kibali hiki siyo hisani unapoona mtumishi wako amestaafu na kinaombwa mwezi wa Machi kila mwaka kwenye bajeti lakini hakuna kinachotokea. Ninaomba Mheshimiwa Waziri eneo kama hili linahitaji kibali cha ajira mbadala na kama Halmashauri ina Kata 17 ina Vijiji 34 ina Mitaa 58 wananchi wa eneo la Mbulu Mji, eneo la Mji ni ndogo. Eneo hilo la Mji lilichanganywa pamoja na eneo la vijiji, lengo kubwa lilikuwa kwamba kutokana na jiografia ilivyo, na kwa kuwa Halmashauri iligawanywa kwa lengo la kupeleka huduma karibu na wananchi, basi tusiwapeleke wananchi wale wa upande wa Vijijini waende Jimbo la Mbulu Vijijini ili wapokee huduma. Kwa hiyo naomba sana chonde chonde, nendeni kwenye data muangalie Halmashauri ya Mbulu Mji imeomba nafasi ngapi za ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo jingine naomba nichangie kwa upande huu wa wenzetu ambao wako katika eneo la TAKUKURU. TAKUKURU Wilaya ya Mbulu ina miaka zaidi ya 15 inapangisha jingo, TAKUKURU Wilaya ya Mbulu pia ina upungufu wa watumishi. Kwa hiyo kuna hoja nyingi za TAKUKURU katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu na Wilaya ya Mbulu hazifanyiwi kazi kwa wakati kulingana na wale watumishi walivyo wachache. Kama inawezekana hoja nyingi zinazokwama kwa ajili ya utekelezaji wa Maafisa, basi ngazi za Mkoa na ngazi zingine ziangalie namna ya kutatua tatizo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye ndege za Serikali. Duniani kote hakuna Serikali inaweza ikafanya biashara ika – perform au ikafanya ufanisi zaidi, ushauri wangu kwenye eneo hili la ndege za Serikali hasa za ATCL kwa maana zile zinazokodishwa kwenda ATCL basi Serikali ibinafsishe ili yenyewe ipewe gawio ama ipewe sehemu ya hisa, kwa sababu ni eneo ambalo limelalamikiwa sana na taarifa za CAG, kwamba zinaonesha zinaipa Serikali gharama kubwa na hakuna mafanikio zaidi. Kwa nini nazungumza hivi? Ninazungumza hivi kwa sababu ukiacha ndege za Viongozi wa Serikali hizi ndege zingine zote kwa kukodisha huwezi kupata mrejesho wa mafanikio ya mapato na ufanisi wa kiuchumi kwa maana ya uzalishaji. Kwa hiyo, eneo hili linahitaji zaidi sana lipate utaratibu wa kukodishwa ama wa kubinafsishwa kwa utaratibu wa wazi wa Serikali kusubiri gawio ama sehemu ya faida iliyotarajia kutoka mwanzo.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni eneo la ajira. Vijana wengi wanatoka vijijini, wanakuja huku Makao Makuu ya Nchi kufanya usaili, kule wanakotoka wanakopa, wanapokuja huku wanapata gharama kubwa, ushauri wangu katika eneo hili Serikali iangalie utaratibu wa kuwezesha Sekretarieti ya Ajira kufanya usaili kikanda ili kupunguza gharama kubwa ambayo watoto wa wananchi na vijana wetu hawa wanapata gharama kubwa na kadri wananvyokuja huwa wanakosa kwa sababu nafasi tunazopata ni chache na hizo nafasi chache wanapokuja wengi baadae inageuka kuwa kilio. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna wakati tulipitisha hapa Bungeni kikokotoo kwa Watumishi wa Umma. Wastaafu wamelalamikia sana eneo hili. Hata kama hatusikii, tuliona kuwa ni muhimu, Maazimio ya Bunge siyo Msahafu. Tutazame upya kilio cha wale wengi ambao ni Watumishi wa Umma, walishaitumikia nchi hii, na sasa wanalia kule. Hawa ni watumishi, waliitumikia nchi hii kwa uzalendo mkubwa sana, wanacholalamikia ni umri wa Mtanzania umeshuka. Kwa kuwa umri wa Mtanzania unashuka, na kikokotoo kile kinakuwa kidogo. Nadhani tuna jukumu kubwa la kutazama kama Bunge na kama Serikali, ili tuone hao watumishi na wastaafu wanachokizungumza katika ile hali ya uhalisia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na muda, naomba nizungumzie pia eneo lingine la TASAF.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)