Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Michael Mwita Kembaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Kwanza kabisa ningependa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kutoa pongezi kwa Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya ya kuongoza Wizara hii muhimu katika Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa niseme kidogo kuhusiana na kazi kubwa ambayo inafanywa na viongozi wetu wa kitaifa. Wakati nikiwa mdogo mama ndiye alikuwa tegemeo kubwa katika familia, alikuwa akienda kusenya kuni akiuza ndipo tunapata riziki ya kula. Familia ilikuwa inategemea jitihada za mama, kusomesha, kula na kila kitu. Leo hii wana Tarime tunaona jitihada kubwa za mama yetu mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaifanya katika kulijenga Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapozungumza tayari soko ambalo lilikuwa ni tatizo kubwa katika mji wetu wa Tarime tayari limejengwa liko katika asilimia 75 ili liweze kukamilika wapate sehemu ya kufanyia biashara. Vilevile kubwa zaidi ni ule mradi mkubwa wa maji kutoka Ziwa Victoria. Mji wetu tulikuwa tunapata shida kubwa sana. Maji tuliyokuwa tunatumia yamechanganyikana na tope, magonjwa ya bilharzia na Magonjwa ya kuhara yalikuwa ni sehemu ya Maisha yetu. Sasa mradi huu wa maji utakuwa ni ukombozi wa wana Tarime. Kwa hiyo nichukue nafasi hii kumpongeza Rais wetu kwa kutupa fedha za kutosha kwa ajili ya kuleta maji katika mji wetu wa Tarime.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuwapongeza mawaziri wote kwa kazi nzuri wanazozifanya, lakini niwaombe wasiwe wanakwenda kwenye majimbo yetu kimya kimya, na wakati mwingine wanakwenda bila kutoa hata taarifa kwa Wabunge. Ni matarajio ya wananchi kuona Mawaziri wakizungumza nao na kueleza mambo makubwa ambayo Serikali imefanya kupitia kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine Mawaziri wanaenda pale kinyemela kinyemela, unashtukia tu anaenda kwenye ofisi ya Mkuu wa Wilaya, wananchi wanaambulia kuona misafara na vimuli muli vinapita. Tungependa waweze kufanya mikutano, waweze kuzungumza matendo makubwa ambayo yanafanyika kupitia Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanya kazi kubwa sana kwa upande wa madarasa, vituo vya afya na kujenga hospitali. Kwa mfano, kwa kipindi cha kuanzia 2021 mpaka sasa hivi kumejengwa hospitali zaidi ya kumi za rufaa za mikoa. Vile vile hospitali 102, vituo vya afya 487 na Zahanati 1,198. Upanuzi wa vituo hivi, na madarasa unahitaji wafanya kazi ambao wanahitajika kufanya kazi katika vituo hivyo, zahanati hizi pamoja na shule ambazo zimejengwa mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini takribani wafanyakazi watumishi waliopo katika Serikali yetu ni takribani laki saba ambayo kwa ujumla kila Mbunge anayesimama anaongelea kuhusu upungufu wa watumishi katika majimbo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kushauri jambo moja. Kila mwaka wahitimu wanahitimu katika vyuo vyetu, na wahitimu hao wanapotoka katika vyuo vyetu wanaenda kufanya shughuli ambazo haziendani na kazi walizosomea. Kwa mfano mtu amesomea udaktari ameenda kufanya kazi ya kupiga debe stendi; sasa amefanya kazi ya kupiga debe ndani ya miaka sita mfululizo. Kwa mfano ajira zilizotoka hivi juzi akaajiriwa mpiga debe ambaye amefanya kazi kwa miaka sita akaenda kutibu mgonjwa. Kama tunavyojua mtu akikaa muda mrefu bila kuendeleza taaluma yake kile anachokifanya kinaingia kichwani mwake na anaendelea kukifanya. Ni nini tunategemea basi? Hatima yake ni kwamba hatutegemei atoe huduma iliyo bora, hata kauli atakayokuwa anatoa haitakuwa kauli ya taaluma aliyoisomea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile ningependa kusema hili. Ukiangalia sasa hivi wale wanao ajiriwa loan board inaenda kuwadai walipe mikopo, na ukiangalia mishahara yao especially wale wanao ajiriwa katika sekta binafsi unakuta mtu anapata mshahara wa laki tatu, mshahara wa laki nne, anadaiwa alipe makato yote pamoja na mkopo huu wa loan board. Hii inapelekea apate kitu kidogo sana ambacho hakiwezi kustahimilisha maisha yake ya kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa nishauri kuwepo utaratibu, sera madhubuti iandaliwe, ambayo itaruhusu wahitimu wote walio hitimu waweze kwenda kujitolea katika sehemu zao walikotoka. Kama ni madaktari waende kwenye hospitali, zahanati na vituo vya afya vilivyo katika maeneo yao. Hii itapunguza gharama za maisha kwa sababu atakuwa anatoka nyumbani anaenda kufanya kazi. Lakini vile vile wakati anajitolea Serikali ipange utaratibu mzuri waweze kuwalipia mikopo hiyo kidogo kidogo kwa sababu wanafanya kazi, ili atakapokuwa wameajiriwa at least ipunguze makali ya makato ambayo huwa wanakatwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kujitolea kunajenga mtu aweze kupata uzoefu, ajenge na kuwa na uzalendo wa nchi yake na pia kujitolea ni tendo la upendo. Kwa hiyo tutakuwa tumejenga uzalendo katika nchi yetu, kwamba watu wakimaliza elimu yao vyuoni watakwenda kujitolea, kwa hivyo tutakuwa na watumishi wengi, jambo ambalo litapunguza uhaba wa madaktari, walimu na watumishi katika idara zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba, hili nilishalisema, lakini ninarudia kusema kwa sababu ninaona kwanza huduma zinazotolewa katika taasisi na idara zetu za Serikali wakati mwingine zinakuwa ni chini ya kiwango kwa sababu watu waliotoka pale ni wametoka direct kutoka kupiga debe, kuendesha boda boda, wakulima na ile fani ambayo waliisomea hata imesha yeyuko kutoka kwenye akili zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa Serikali ichukue hili kwa u-serious ili iweze kulifanyia kazi na tuondokane na tatizo la upungufu wa watumishi katika idara zetu. Lakini vile vile itasaidia kujenga uzalendo na vijana wetu kupata ujuzi wa kufanya shughuli zao kikamilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti,ukiangalia katika Sekta ya elimu, kwa mfano kwa mwaka 2020, utafiti uliofanywa na taasisi isiyo ya kiserikali ya BEST ilibainisha kwamba kuna upungufu wa watumishi katika idara ya elimu zaidi ya 50,993, hiyo ni miaka hiyo kabla ya madarasa hayo kujengwa na shule kupanuliwa. Kwa hiyo sasa hivi kutakuwa na uhitaji mkubwa wa watumishi katika sekta ya elimu pamoja na sekta ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kuondokana na tatizo hili, ambalo ni kubwa na ni sugu katika nchi yetu. Najua kwamba si Tanzania peke yake, ni nchi nyingi, ningependa sana Serikali kupitia Wizara hii wafanye mchakato wa kuandaa sera ya kuhakikisha kwamba wale wahitimu wanaotoka katika Vyuo vyetu wanapata nafasi ya kujitolea katika maeneo yao. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.