Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii nyeti. Kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kuendelea kuaminiwa na Mheshimiwa Rais na Naibu wake. Najua ni wachapa kazi, kwa hiyo niwapongeze sana. Vile vile niwapongeze wataalam ambao wako katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze pia Mheshimiwa Rais. Mheshimiwa Rais mwaka jana alirudisha furaha kwa watumishi waliokuwa wameondolewa kazini kwa kusema ile asilimia tano irejeshwe kwa watumishi ambao awali ilionekana hawana haki ya kulipwa chochote. Jambo hili limerudisha furaha kubwa kwa watumishi ndani ya Tanzania hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watumishi wale wameanza kulipwa, baadhi yao wamelipwa, lakini bado kuna watumishi hawajalipwa. Kwa hiyo niiombe Serikali ifanye jambo hili haraka kama agizo lilivyotolewa ili ile furaha ambayo watumishi walianza kuwa nayo iendelee na iwepo, isije sasa ikaonekana jambo hili limesemwa halafu watumishi wanaendelea kusononeka, wanarudisha masikitiko na masononeko kwa Serikali yao ambayo inawapenda sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, nizungumzie suala la ajira. Amezungumza vizuri sana mwenzangu Mheshimiwa Ezra hapa. Ikumbukwe na ifahamike sisi hapa hatusemi maneno yetu wenyewe, yale yote tunayoyazungumza ni maneno ya wale waliotutuma kuja hapa Bungeni. Kule kwenye maeneo yetu ndiko wanakoenda hao watumishi wanaoajiriwa kwa mtindo ule ambao Waziri wa TAMISEMI jana alizungumza hapa. Ni utaratibu mzuri, lakini ule utaratibu una manung’uniko huko kwenye majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, manung’uniko ni mengi sana. Baadhi ya wananchi wanasema ajira hizi zinatolewa upande fulani na wanataja. Naogopa tu kusema hapa, kwa sababu wanawaona mtu fulani kwa jina na majina yanafahamika. Unaona Walimu wameletwa labda 10, katika 10 wale nane majina yanafanana ni ya maeneo fulani. Kwa hiyo, wananchi wanasema kwamba ajira hizi zinatolewa kwa ukanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maneno yale wanatupatia sisi kama wawakilishi wao. Sasa kwa sababu tunakuwa hatuna takwimu, hatuna data pale za kusema kwenye jimbo langu mimi hapa, kwenye halmashauri yangu hii mimi wametoka watumishi wa ngapi? Kwa hiyo, hapa ndio namuunga mkono Mheshimiwa Ezra kwamba idadi ile ikigawanywa kwa halmashauri zote pengine sisi tutakuwa na majibu mazuri kwa wale wananchi tofauti na ilivyo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana jambo hili watusikilize, hatuna nia mbaya na Serikali yetu, tunaipenda sana, najua Serikali zinaongea, Serikali inazungumza, wafanye mawasiliano watusikilize. Kwanza, watoe kwa wale waliokuwa wanajitolea, lakini pili kwa kila jimbo, kwa kila halmashauri basi kuwe na idadi fulani ambayo mimi Mbunge nikienda kuongea nasema hapa bwana kuna orodha ya watu hawa ametoka katika halmashauri hii, itakuwa imekaa vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nilikuwa nataka niongelee suala la ujibuji wa barua. Watumishi wetu hawa wanaandika barua pengine wanakuwa na vikwazo na matatizo fulani kwenye idara husika au eneo fulani analofanyia kazi. Anakuwa amesimamishwa au ana jambo tatizo fulani anaambiwa aandike barua. Anaandika barua, mwisho wa siku anakata rufaa, ipo kwenye Wizara ya Mheshimiwa Waziri, majibu yale hayarudi, inachukua muda mrefu sana watu kujibiwa majibu. Sasa sijajua hiki kitengo hakina watu wa kutosha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama shida ni hiyo, basi waongezewe watu. Mpaka leo nina watu 18 wamepeleka barua toka mwaka 2022. Wale walioondoshwa kwa vyeti fake wamepeleka barua katika Ofisi ya Mheshimiwa Waziri, lakini mpaka leo hawajajibiwa. Sasa kutojibiwa inakuwa kero kwa Serikali, inakuwa kero kwa Mbunge, inakuwa kero kwa Serikali iliyoko pale eneo husika kwa maana ya wilaya na halmashauri, kila siku watu wanahudhuria ofisini hapo. Niombe sana Mheshimiwa Waziri aimarishe hiki kitengo, kijibu zile barua, kama ndio iwe ndio, kama hapana iwe hapana ili lile suala liwe limefungwa. Tofauti na ilivyo sasa kila leo simu, kila leo message, kila leo ofisini, tunakuwa hatujaimarisha utawala bora katika nchi yetu. Naomba sana hili tulifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la wastaafu na pensheni; wastaafu wetu hawa wamelihudumia Taifa hili kwa uadilifu mkubwa sana. Wanafika sehemu wanastaafu, wengine wanalipwa kwa muda, lakini watu wengine wanapata shida sana kupata mafao yao. Hata hivyo, wanaweza kuwa wamepata mafao, kuja kupata yale mafao ya mwezi hawapati. Vilevile hawapati saa nyingine si kwa sababu yake yeye kuna kitu kinaitwa tozo. Sasa hii tozo mimi nimeifuatilia, haimhusu yule mtumishi aliyefanya kazi akamaliza muda wake, amekwenda pale ale pensheni yake anaambiwa bwana Serikali, sijui taasisi fulani haikulipa hii tozo. Sasa hii tozo inamhusu nini huyu mtumishi? Jambo hili linaumiza sana, jambo hili halikubaliki.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Matiko, taarifa.

TAARIFA

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka tu kumpa taarifa msemaji anayechangia kuhusiana na kadhia wanayoipata wastaafu. Ni kweli alivyosema yaani imekuwa kero. Kwa mfano, mstaafu amepandishwa cheo, alikuwa na cheo fulani amepanda kwenda ngazi fulani ambayo mshahara umepanda, lakini anapostaafu analipwa kikokotoo cha mshahara wa awali sio ambao amepanda cheo. Akiuliza anaambiwa Serikali haikuleta hayo makato. Inatakiwa ulipe kwanza yaani achukue hela pembeni alipe hiyo tozo ya Serikali ili aweze kupewa mafao yakeo. Kwa hiyo, imekuwa ni kero wastaafu wanateseka sana, wengine mpaka wanaweza kufa kabla hawajapata mafao yao.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Benaya Kapinga unapokea taarifa?

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hii tena kwa mikono miwili na ndio ilikuwa hoja yangu ya pili kwamba pamoja na ile ya tozo ambayo nilikuwa naisemea kwamba, hii tozo ni ama taasisi aliyokuwa anaifanyia kazi ama Serikali ilichelewa kupeleka kwenye Mfuko husika. Huyu mtumishi yeye makato yake yalishakwenda, lakini Serikali au taasisi fulani imechelewa kupeleka ile tozo, gharama yake sasa inamrudia mtumishi. Hili jambo si sawa wala sio haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako watumishi sasa hivi katika halmashauri yangu wanahangaika na hilo, hawalipwi mafao yao wana miaka mitano. Hawalipwi pensheni yao ya mwezi kwa sababu tu halmashauri haikupeleka tozo, kwa sababu tu Idara ya Elimu wakati huo haikupeleka tozo. Sasa hii tozo jamani, Serikali si wanaongea? Kwa nini wasizungumze huyu mwananchi raia wa kawaida apate haki yake, aendelee kula. Ameshafika miaka 60, miaka yenyewe ya kuishi mwisho 70, sasa atapata lini hela yake? Kwa kweli jambo hili si zuri na si sawa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ndilo hilo alilosema Mheshimiwa Esther kwamba tunachelewa kuwapandisha vyeo hawa watumishi au anapata barua halafu mshahara hauingii miezi mitano au mitatu. Mwisho wa siku anakuja kupata mshahara wa mwezi mmoja, calculation inayokuja kufanyika inafanyika ile ya kule nyuma sio ile stahiki yake na analipwa hicho, mtumishi huyo anaendelea kuhangaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri, najua yeye ni mchapakazi kweli kweli na ndio maana Mheshimiwa Rais anamwamini na anaendelea kumwamini, naomba hili jambo wakati huu yupo liishe. Vile vile na watumishi kama wananisikia wawasaidie Waheshimiwa Mawaziri hapa, wasikae tu sisi tunasema hapa, tunawasema hawa, wao kule wanafurahia wanafanya mambo yao kama inavyofanyika siku zote. Si jambo jema, wafanyeni kazi kizalendo, waisaidie nchi hii, wamsaidie Mheshimiwa Rais wa Nchi hii kuondoa kero katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kulisemea ni suala la Sekretarieti ya Ajira. Tulianza vizuri ilikuwa inaenda vizuri na ilikuwa inafanya kazi vizuri. Najua lengo la Serikali ni kuleta umoja ndani ya nchi yetu. Haya mambo tunayosema ukanda fulani ili yasijitokeze, lakini sasa hivi zimeibuka baadhi ya tasisi zinataka zenyewe sasa ziajiri zenyewe. Jambo hili sio jema tutarudi kule kule ambako tunafikiri sasa ukanda ule ndio utaendelea zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yalikuwepo maneno TRA wamejaa watu wa ukanda fulani, Bandari wamejaa watu wa ukanda fulani wakati fulani, lakini hapa katikati yalipungua sana. Kwa hiyo, niombe tuiboreshe Sekretarieti ya Ajira, badala ya kufikiri kurudisha tena kule hizi taasisi zikawa zinaajiri zenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)