Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa kunipatia nafasi ya kuchangia bajeti ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma. Nikianza kwa kumpongeza mwenye Ofisi yake kwa maana ya Mheshimiwa Rais. Pia, niwapongeze wanaomsaidia kwa maana ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Kaka yangu Mheshimiwa Simbachawene, tuna imani kubwa naye, Waziri senior na mjomba wangu Ridhiwani Kikwete tuna imani naye, ni mweledi katika eneo ambalo Mheshimiwa Rais amekupa majukumu hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile, nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipompongeza mtangulizi wa Mheshimiwa Simbachawene, Dada yangu Jenista Mhagama amefanya kazi ambayo imeacha legacy katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na wenzangu ambao kwa kweli tunaikumbusha Serikali kuwafikiria wale ambao waliondolewa katika Utumishi wa Umma kwa sababu zisizokuwa na ulazima wowote, Mheshimiwa Jenista Mhagama amefanya kazi kubwa asilimia kubwa wamerudi, kwa sababu kauli ya Mheshimiwa Rais anasema kazi iendelee ninaomba Mheshimiwa Simbachawene endeleza pale ambapo Mheshimiwa Jenista ameachia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo wachache ambao wamebaki wakiwemo wale ambao walikuwa na qualification za Darasa la Saba naomba Mheshimiwa Waziri shughulikia warudi katika Utumishi wa Umma kwa sababu ilikuwa ni haki yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo mimi nianze na ajira. Wachangiaji wengi wamezungumzia katika mfumo ule wa Central Government kwa maana ya ajira ambazo zinafanywa na Sekretariati ya Ajira katika Utumishi wa Umma. Nianze na ajira ambazo zinafanywa na Mamlaka za Serikali za Mitaa ambazo kimsingi zimekasimiwa na Sekretariati ya Ajira katika Utumishi wa Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ajira ambazo zinafanywa na Mamlaka za Serikali za Mitaa ni za kisheria lakini sheria hiyo inawataka watu wa Sekretariati ya Ajira wasimamie mchakato wa mwenendo huu, lakini mimi nieleze masikitiko yangu kwamba usimamizi wa mchakato wa ajira unaofanywa katika Mamlaka za Serikali za Mitaa unatuondolea imani sisi tunaotoka katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, bado tunahisi kwamba kuna viashiria vya ubaguzi, kuna viashiria vya upendeleo na kuna viashiria vya kuonea watu wa Mamlaka za Serikali husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na case study kutoka katika Halmashauri yangu ya Wilaya ya Kilwa, michakato kadhaa ya ajira imefanyika, karibu mitatu nyuma kutoka sasa lakini hata wale wenye sifa za msingi wanaotoka katika Halmashauri za Wilaya ya Kilwa wamekosa kupata ajira kwa kisingoizio tu kwamba hawakufaulu mtihani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kuna jambo la kufanyia kazi Serikali na nitoe wito au ushauri kwa Serikali kwamba hebu tukachunguze ajira tatu zilizofanywa kwa mfululizo katika Halmashauri ya Kilwa kama zili-base on merit, kama sheria zilizingatiwa na kama weredi ulitumika katika mchakato wa ajira huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kusikitisha zaidi ni kwamba watumishi wale ambao ni wakazi na wazawa wa Halmashauri wanapokuja katika mitihani ya practical wanafanya vizuri lakini inapokuja katika theory wanaonekana wamefeli, watumishi wanotoka nje ya Kilwa wanapokuja kwenye theory wanafanya vizuri kulikoni? Hii kama ni bahati mbaya kwa nini iwe ni bahati mbaya au by accident wa ajira tatu mfululizo hata mmoja hapati, hata wale watumishi ambao wamekuwa wakijitolea pale kwa mfano, hata kada ya madereva tu wanakosa ajira sifa za msingi wanazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo la kufanyia kazi Serikali. Nimetoa ushauri kwamba likafanyiwe kazi kabla sisi Mamlaka ya Serikali za Mitaa kwa maana mimi Diwani mmojawapo wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa na Madiwani wenzangu hatujachukua hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo nije katika stahiki za Watumishi. Hapa nitazumzia watumishi waliopo katika Utumishi wa Umma na Wastaafu. Pamoja na juhudi ambazo Serikali imeendelea kuzifanya lakini bado katika eneo la matibabu, masomo likizo malimbikizo ya mishahara na disturbance allowance kwa wastaafu bado imekuwa ni kizungumkuti katika kuhakikisha kwamba watumishi hawa wanapata stahiki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano kwa kadhia ambayo imekuwa ikiwakumba wastaafu. Ninayo orodha ya wastaafu waliostaafu katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa tangu mwaka 2018 mpaka leo, ninasikitika kusema kwamba hawajalipwa mafao yao ya kustaafu kulikoni? Nikiwataja kwa uchache wao hapa angalau kwa mfano tu, kuna Mwalimu Mstaafu Omari Mcheula kuna Mwalimu Mstaafu Khadija Bungurumo kuna Mwalimu Mstaafu Salma Kaisi tangu 2018 mpaka leo hawajalipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha wakati wengine hebu tuuvae uhusika, just imagine kwamba ni wewe ndiyo umetumikia nchi hii kwa weledi kwa mapenzi makubwa tangu 2018 umestaafu mpaka leo hujalipwa, hii ni kadhia lazima Serikali ifanye jambo hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo niseme tu kwamba Mifuko ya Pensheni na hapo kwa upeke yake nauzungumzia mfuko wa PSSSF umekuwa ukichelewesha mafao ya watumishi wastaafu, hebu Serikali ichukue hatua katika eneo hili. Mstaafu anastaafu miaka mitano nyuma anakaa tu anahangaikia tu, hili kwa kweli ni jambo ambalo linasikitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo nije katika suala la madaraja. Ninashukuru Serikali ya Awamu ya Sita imeweza kupandisha madaraja watumishi lakini kitu ambacho ninaomba kuikumbusha Serikali ni kwamba zoezi hili halikufanyika kwa umakini tulioutarajia. Kilichofanyika ni kwamba watumishi ambao pengine kwa miaka mitano na kidogo hivi hawakupandishwa vyeo wakapandishwa kwa mkupuo, tafsiri yake ni kwamba kwenye eneo la utumishi wa umma tunakosa ile dhana ya seniority, mtumishi ambaye alikuwa wa kwanza kuajiriwa anajikuta yuko daraja moja na aliyefuatia kuajiriwa, hii itakuja kuleta athari kwenye utaratibu wa kustaafu na kwenye taratibu za mafao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe ushauri pamoja na kwamba Serikali imefanyia kazi eneo hili, ushauri wangu ni kwamba ikafanye review ya taratibu zote za upandishaji wa madaraja ili kila mtumishi akae kwenye daraja lake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nizungumie suala la motisha kwa Walimu. Huko nyuma tulikuwa na kitu ambacho kwa Walimu kilikuwa kinaitwa teaching allowance haitolewi kwa nini Serikali imeondoa teaching allowance, nadhani Serikali ambayo ilikuwepo wakati huo iliweka teaching allowance kwa Walimu kwa kuzingatia uzito wa jukumu la kazi ya ualimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nikumbushe tu kwamba mwalimu pamoja na kufundisha, ambapo watu wengi tunadhani kwamba kazi yake ni kufundisha tu, ana kazi kubwa ya kuandaa mpango mzima wa ufundishaji wa mwaka au muhula mzima ambao kiualimu unaitwa scheme of work, lakini mwalimu anajukumu la kuandaa lesson plan, mwalimu ana jukumu la kuandaa teaching aid, utaona walimu kama watatu hivi wanacheza wanaandaa midoli, midoli hivi ndiyo kazi ya Mwalimu na anaifanya nje ya muda wa kazi. Walimu wana kazi ya kuandaa lesson plan na sasa hivi wameongezewa kitu kinachoitwa KPI. Hii load kubwa yote kwa nini Mwalimu asilipwe teaching allowance wakati watumishi wengine wanalipwa kitu kinachoitwa responsibility allowance, ration allowance, on call allowance kwa nini Mwalimu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalizungumza hili kwa masikitiko makubw,a tutunze heshima ya Walimu katika nchi hii, viongozi wengi wakubwa katika nchi hili wamekuwa ni walimu, kwanini hatumheshimu Mwalimu? (Makofi)

MBUNGE FULANI: Taarifa.

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, viongozi wengi wakubwa katika nchi hii wamekuwa ni walimu, Baba wa Taifa ni Mwalimu, Mzee Alli Hassan Mwinyi ni Mwalimu, Hayati Magufuli ni Mwalimu, Waziri Mkuu wa sasa hivi Kassim Majaliwa ni Mwalimu, kwa nini hatutunzi heshima ya Walimu? Spika wa Bunge ni Mwalimu, tutunze heshima ya walimu kwa kuhakikisha kwamba walimu tunawatendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbushwa hapa kwamba Waziri wa nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu ni Mwalimu, pia nakumbushwa kwamba Waziri wa Elimu ni Mwalimu, nakumbushwa pia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu mwingine ni mwalimu, sasa Ndugu zangu ni kwa nini hatuwatendei haki walimu, rudisheni teaching allowance kwa walimu. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya masuala ya kwamba performance na nini na nini hayana mpango wowote, muwezeshe mwalimu, toa motisha kwa walimu, elimu itapanda katika nchi hii. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumza haya kwa masikitiko makubwa, nimesahau hata Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, ndugu yangu Mheshimiwa Jumanne Abdallah Sagini ni mwalimu. (Kicheko/Makofi)

MBUNGE FULANI: Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ally Kassinge muda wako ulikuwa umekwisha lakini kwa mamlaka niliyonayo nakuongeza dakika nyingine moja ili uweze kumalizia na pengine ufahamu pia na Kiongozi wa Muhimili huu pia ni mwalimu. (Makofi)

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe ushauri wa bure na wa nia njema, hatuzungumzi kwa namna ya kufurahisha Bunge lakini ni ushauri wa bure na wa nia njema, hebu tutunze hali ya mwalimu katika nchi hii, turudishe teaching allowance kwa walimu. Ufaulu utaongezeka kwa kumwezesha na kumpa motisha Mwalimu na siyo vinginevyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kuniongezea muda na wewe utawekwa katika alama ya kumbukumbu kwamba ulimwongezea muda Mbunge anayechangia hotuba hii kwa kuhakikisha kwamba walimu wanapewa fursa ya kusikilizwa na haya yakifanyika tutakuweka katika kumbukumbu, wekeni alama Mheshimiwa Simbachawene, Mheshimiwa Waziri wa Elimu wekeni alama kwa kuhakikisha kwamba mnarudisha motisha kwa kwa Walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi/Vigelegele)