Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika bajeti hii ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Kwanza, napende kumpongeza Mheshimiwa Rais pamoja na Wizara yetu hii kwa kazi kubwa ambayo wameifanya katika kipindi cha siku hizi za karibuni, kwa kuzingatia utawala bora katika nchi yetu, hasa kwenye ile misingi ya utawala bora ambayo ni haki na usawa, ukweli na uwazi, ushirikishwaji, uhuru na misingi ya kidemokrasia, kufuata sheria pamoja na kusimamia maslahi ya wengi hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuanza kuchangia kwenye suala la mafunzo kwa Maafisa Utumishi. Maafisa Utumishi wetu wengi wamekariri Standing Orders au zile Kanuni za Utumishi wa Umma. Wengi ni mambumbumbu katika Sheria Mama katika Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini. [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta Maafisa Utumishi wengi wanashindwa ku-cope na mazingira na wakati mwingine wanajikuta wanakosea na kuwanyima baadhi ya watumishi wetu haki zao kwa sababu wamekariri tu mambo fulani ambayo yapo kwenye Kanuni za Utumishi wa Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukimpelekea Afisa Utumishi kwenye sheria mama, Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini, unakuta hajui. Kwa hiyo, napenda kusisitiza, naiomba Serikali iwekeze kwenye kutoa mafunzo kwa hawa Maafisa Utumishi ili waweze kutenda haki kwa watumishi wetu ambao wanatumikia Taifa letu katika ngazi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika hili, unakuta kuna baadhi ya Halmashauri, Mkurugenzi anajiamulia tu. Unaweza ukakuta Mkurugenzi kila baada ya miezi sita anahamisha watendaji kata bila ya kuzingatia taratibu na haki zao ambazo wanazostahili. Unakuta Mtendaji Kata leo amehamishiwa kata hii, baada ya miezi sita anahamishiwa kata nyingine, halipwi disturbance allowance, halipwi haki yake yoyote. Shida ni kwamba kanuni na sheria na taratibu, hawa Maafisa Utumishi wanashindwa kuwaelekeza hawa Maafisa Masuuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala la upungufu wa watumishi. Bado kumekuwa na upungufu mkubwa wa watumishi, japokuwa Serikali imejitahidi kwa miaka ya hivi karibuni, na hivi karibuni wametangaza hizo ajira 21,200, lakini bado tatizo ni kubwa. Tatizo limekuwa kubwa zaidi hasa kwa Halmashauri zetu za Wilaya. Watumishi wengi wakiajiriwa, unakuta wakishapata tu uthibitisho kazini, wanahama kutoka kwenye Halmashauri zetu za Wilaya zenye vijiji vingi, kwenda Halmashauri za Miji, Manispaa na Majiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali katika eneo hili ijitahidi kudhibiti taratibu za uhamisho ili wakishaajiriwa waendelee kubaki kule kwenye vijiji vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukienda kwenye zahanati na shule, utakuta walimu ni wachache; manesi, utakuta ni mmoja tu, na ndio huyo huyo, hakuna Clinical Officer, hakuna daktari. Kwa hiyo, ni shida juu ya shida. Pamoja na kwamba tumeongeza miundombinu ya madarasa, maabara na zahanati, lakini unakuta zahanati hizo zimebaki zikiwa hazina watumishi wa kutosha, na mwisho wa siku wananchi wanakosa huduma muhimu katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niseme, Mbunge mwenzangu, Mheshimiwa Ally Kassinge, Mbunge wa Kilwa amezungumza hapa kwa uchungu kabisa na kwa hisia kubwa. Naye alikuwa Mwalimu siku zilizopita. Anajua vizuri katika masuala ya ualimu. Upungufu wa Walimu umesababisha hasa kwenye masomo ya sayansi, walimu wamefikia hatua wanapangiwa vipindi kati ya 35 mpaka 64 kule kwenye Halmashauri yetu ya Wilaya ya Kilwa, lakini standard ni vipindi 24 mpaka 30. Kwa hiyo, unaweza ukaona hali halisi ilivyo. Kwa hiyo, Walimu wanafanya kazi katika mazingira magumu na mwisho wa siku maisha yao yamekuwa magumu vile vile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna madai mbalimbali ya walimu. Yamekuwa aidha yakichelewa kulipwa na wakati mwingine hayalipwi kabisa na wanapigwa danadana tu. Unakuta madai ya tangu mwaka 2015 mpaka leo bado hayajalipwa. Hata yakilipwa, mtu anadai Shilingi 500,000/= analipwa Sh. 180,000/=, anaambiwa hii utalipwa baadaye na ndiyo imetoka hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba kwa watumishi nayo ni changamoto kubwa. Hii imelazimu sasa watumishi wengi wanaolazimika kukaa maeneo ya mbali yenye nyumba zinazostahili ambazo ziko mbali na vituo vyao vya ajira. Kwa hiyo, naomba Serikali iliangalie jambo hilo ili kuboresha hasa kwenye sSekta hii ya elimu na sekta ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuzungumzia suala la wathibiti ubora. Mwaka 2022 nilizungumza juu ya changamoto iliyopo kwa watumishi hawa muhimu wathibiti ubora, wamekuwa wakifanya kazi kubwa katika mazingira magumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mwaka 2014 nilishawahi kusema, ulitoka waraka ambao unahusu viwango vya mishahara pamoja na viwango vya posho za madaraka kwa viongozi wa elimu, lakini yale mabadiliko ambayo yalitolewa kulingana na waraka ule wa mwaka 2014, yameweza kutumika tu kwa wale ambao wako kwenye kada ya elimu yenyewe; walimu wakuu, waratibu wa elimu, Maafisa Elimu wa Wilaya na Mikoa, lakini hawa Wathibiti Ubora wa Wilaya na wa Kanda hawajaweza kubadilishiwa. Pamoja na kuzungumza mwaka 2022 mpaka leo hii, hawajabadilishiwa miundo yao, hawajabadilishiwa posho zao, hawalipwi stahiki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naishauri Serikali kwamba iwalipe stahiki zao pamoja na arrears zake ili waweze kufanya kazi kwa bidii na kwa umahiri ili tuweze
kupata elimu iliyo bora. Kwa sababu unaweza ukafundisha darasani, lakini kama hakuna assurance kwenye elimu, ni kazi bure. Utakuta hiyo elimu haifuatiliwi, kama kuna uzembe haufatiliwi, au kuna kulegalega katika kufuatilia mambo kama hayo. Kwa hiyo, kwa ujumla napenda hilo nalo lizangatiwe ili basi hawa wathibiti ubora nao waweze kusaidiwa na kuweza kupata haki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala la wastaafu. Wenzangu wamezungumza sana kwa kirefu, nami labda nizungumze kwa kifupi tu. Wastaafu wamekuwa wakichelewa sana kupewa haki zao. Naomba hao wazee wetu wapewe kipaumbele. Katika mwaka wa fedha unaokuja watengewe bajeti inayotosha kulipa haki zao za mizigo na haki nyingine ili hatimaye pale wanapostaafu, walipwe mara moja na waweze kwenda kurudi katika maeneo yao ambayo wanatokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)