Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, naomba kuchukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali nzima ya Awamu ya Sita kwa jinsi walivyosimamia utekelezaji wa Ilani ya CCM 2020/2025. Kwa kweli kwa niaba ya wananchi wa jimbo langu la Mbulu Mjini napenda kuchukua nafasi hii kwa jinsi tulivyotatua changamoto nyingi zilizoshindikana kwa zaidi ya miaka 20 kwa kupatikana fedha za miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, mifano hiyo ni ujenzi wa Bwawa la Umwagiliaji la Endayaya Tlawi ambayo usanifu wake ulikamilika toka mwaka 2003 na sasa linajengwa kwa shilingi bilioni saba.

Pili, ujenzi wa barabara ya lami Karatu – Mbulu - Haydom ambayo ni ahadi ya Serikali ya Awamu ya Nne inayotekelezwa; tatu, ujenzi wa sekondari mpya katika Kata ambazo haziko, ujenzi wa vituo vya afya kikata; na nne, kupatikana kwa fedha za mfuko wa jimbo kwa ajili ya matengenezo ya barabara TARURA na fedha zingine nyingi.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba kutoa mchango wangu kupitia mpango huu wa mapendekezo ya Bajeti ya Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora; kwanza Serikali itazame upya mfumo wake wa kujaza nafasi wazi za watumishi wanaostaafu, kwa mfano halmashauri yangu ya Mbulu Mjini kuna watumishi wengi waliostaafu toka mwaka 2015; mpaka sasa hakuna kibali cha ajira mbadala iliyotolewa hali inayopelekea halmashauri kubakiwa na maafisa kilimo watatu badala ya 54 na maafisa mifugo, uvuvi na ushirika kubakiwa watano badala ya 52. Mbaya zaidi hivi karibuni kuna mtumishi wa ajira mpya aliyepangwa mpaka leo hajaripoti, kwa hiyo, halmashauri yetu ina upungufu mkubwa sana wa watumishi, Serikali ichukue hatua za haraka.

Mheshimiwa Spika, pili, Serikali iangalie upya utaratibu wa kuwaingiza walengwa wa TASAF hasa wale walioko kwenye maombi ya rufaa; tatu, Serikali iangalie uwezekano wa kuingiza somo la uzalendo kuanzia elimu ya msingi hali itakayowaandaa kizazi cha Watanzania kitakachokuwa na uzalendo mkubwa kwa nchi yao. Nasema hayo kwa sababu ukipitia taarifa nyingi za CAG ni wazi kuwa kizazi chetu kinazidi kupoteza maadili na uzalendo; nan ne, Serikali ijaze nafasi zinazokaimiwa katika Mamlaka za Serikali za Mitaa na sekta zingine zijazwe au kuthibitisha wale wanaokaimu nafasi hizo haraka ili kuboresha utendaji na uwajibikaji kwa watumishi wetu.

Mheshimiwa Spika, tano, Serikali iangalie uwezekano wa muda mzuri wa Bunge kujadili taarifa ya CAG mara itakapokabidhiwa kwa Mheshimiwa Rais ili kuondoa hisia nyingi za wananchi kama ilivyo sasa kujadiliwa mwezi Novemba kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, tunamshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia baraka zake kwetu nyanja mbalimbali za ustawi wa kijamii, kiuchumi, kisiasa kidiplomasia na kutuepusha na majanga mengine mengi. Pia tunampongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa mambo mengi sana katika kuiongoza nchi yetu na utekelezaji wa Ilani ya CCM 2025, kwa kweli sisi kama Wabunge wa CCM tuna mengi ya kujivunia kupitia Rais wetu, tunamwombea kwa Mwenyezi Mungu amjalie ulinzi, baraka na mafanikio katika utume wake kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Sekretarieti ya Ajira nchini ndiyo chombo pekee cha kufanya usaili wa ajira nchini ambapo nchi ina wahitimu wengi sana wanaotuma maombi ya nafasi ya ajira pindi tangazo litakapotolewa, Serikali iangalie uwezekano wa kuijengea uwezo wa fedha, magari na vitendea kazi mbalimbali ili usaili wa nafasi za kazi ufanyike kikanda hapa nchini kwa kuwa wanaofanikiwa ni wachache.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa niongeze sehemu ya mchango wangu kupitia hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Mbulu ni Wilaya kongwe hapa nchini, kwa sasa inakabiliwa na upungufu mkubwa wa miundombinu ya huduma hususan majengo ya taasisi mbalimbali, kwa hiyo toka mwaka 2005 serikali ilifungua ofisi ya TAKUKURU Wilaya ya Mbulu, toka muda huo mpaka leo taasisi hiyo haina jengo la ofisi kwani walipangisha nyumba ya mtu binafsi ambayo ni ndogo sana na iliyojengwa kwa ramani ya makazi. Hivyo ninaiomba sana Serikali itujengee ofisi ya taasisi hiyo muhimu kwa maendeleo na ustawi wa jamii na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, Serikali iangalie upya utaratibu wa kuongeza malipo ya pensheni ya kila mwezi kwa watumishi wastaafu wa miaka ya nyuma kwa kuwa kiasi kinacholipwa kidogo sana ambayo haiwezi kumpatia hata bima kubwa, sote tunafahamu kundi hili linakabiliwa na maradhi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia moa moja.