Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mheshimiwa George Simbachawene na Naibu wake Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete pamoja na watendaji wa Serikali katika Wizara hii kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utajikita kwenye utaratibu uliotumika mwaka 2020 kuhitimisha ajira na kusimamisha mishahara kwa watumishi wa Serikali Watanzania waliogombea nafasi za kisiasa (Ubunge) na madhara yake; na umuhimu wa Serikali kupitia upya sheria inayowafanya maprofesa kustaafu wakiwa na miaka 65 na kutokupata mikataba maalumu ya kuendelea kufundisha.

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kuhitimisha utumishi wa umma kwa kugombea nafasi za kisiasa umeanishwa kwenye Waraka wa Mkuu wa Utumishi wa Umma Na. 1 wa tarehe 2 Januari, 2015 unaohusu utaratibu kwa watumishi wa umma wanaogombea nyadhifa za kisiasa nchini. Waraka huo umefafanua utaratibu wa watumishi wote wa umma wenye nia ya kugombea nyadhifa za kisiasa kama ifuatavyo: -

Kwanza, mtumishi wa umma atakayeamua kugombea nafasi ya Ubunge wa kuchaguliwa, Viti Maalumu vya Ubunge au nyadhifa nyingine za kisiasa ataruhusiwa kufanya hivyo, baada ya Tume ya Uchaguzi kumtangaza kuwa mgombea wa Ubunge na atalazimika kuacha kazi na kulipwa mafao yake.

Mheshimiwa Spika, utaratibu uliotumika ulikuwa tofauti na waraka ulivyoelekeza hapo juu. Serikali iliiagiza Hazina kutowalipa mshahara wa kuanzia mwezi Julai watumishi wake wote waliochukua fomu ya kugombea nafasi ya uongozi wa kisiasa kupitia vyama vya siasa. Siyo tu kuwa mishahara ilisimamishwa, bali baadhi ya waajiri walichukua hatua ya kuwaondoa kazini watumishi waliochukua fomu za kugombea uongozi wa kisiasa mara walipobainika kuchukua fomu za kugombea Ubunge.

Mheshimiwa Spika, watumishi wengi sana wenye uwezo walichukua fomu za kugombea Ubunge, na baada ya kunyimwa mishahara kwa kipindi cha kuchakata majina ya wagombea, hii ilisababisha hofu na usumbufu mkubwa. Watumishi wengi walichukua fomu wakijua kuwa kisheria hakuna shida kutia nia. Kitendo hiki kitatia hofu watumishi wa Serikali (hasa vijana) wenye uwezo wa kugombea katika chaguzi zijazo.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyochangia kwa maandishi katika bajeti ya mwaka 2022/2023, katika vyuo vyetu vikuu vya Serikali, kuna changamoto kubwa ya tatizo la rasilimali watu likiwa limesababishwa kwa kiasi kikubwa na kitendo cha Serikali kubadilisha utaratibu wa maprofesa kuendelea kufundisha kwa mikataba maalumu hadi wanapofikisha umri wa miaka 70.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, kwa miaka michache iliyopita, maprofesa wengi katika vyuo vya Serikali wamestaafu katika umri wa miaka 65 kwa mujibu wa sheria. Katika vyuo vikuu vya Serikali kuna uhaba mkubwa wa walimu katika ngazi ya maprofesa na kwenye soko la ajira si rahisi kuwapata wataalamu wenye vipaji hivi.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya rasilimali watu vyuo vikuu Tanzania inasababishwa pia na masharti magumu ya kuajiri wataalamu kutoka nje ya Tanzania. Kuajiri wataalamu kutoka nje kwenye maeneo ya kimkakati ni muhimu ili kutusaidia kwenye kukuza rasilimali yetu, na kutuunganisha na mifumo ya kimataifa. Upatikanaji wa vibali huchukua muda mrefu na husababisha walengwa kutoka nje kubadili mawazo na kuacha kuja kufanya kazi Tanzania.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuelezea changamoto za hapo juu, naishauri Wizara yafuatayo: -

Kwanza, Serikali ifuate sheria na kanuni za kiutumishi kwenye masuala mbalimbali. Naishauri Serikali iwalipe mishahara iliyosimamishwa watumishi wote wa Serikali waliotia nia ya kugombea kama ilivyoainishwa kwenye Waraka wa Mkuu wa Utumishi wa Umma Na. 1 wa tarehe 2 Januari, 2015 unaohusu utaratibu kwa watumishi wa umma wanaogombea nyadhifa za kisiasa nchini kwani hawakuvunja sheria wala kanuni kutia nia.

Pili, Wizara ya Utumishi na Utawala Bora itoe vibali vya kuajiri wanataaluma wa kutosha kuendana na idadi ya wanafunzi wanaodahiliwa. Hii ni pamoja na kuajiri wataalamu kutoka nje katika maeneo ya kimkakati kama yale ya sayansi, uhandisi na hesabu.

Tatu, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora wapitie sheria na kuongeza umri wa maprofesa kutumika kwa mikataba uanzie pale wanapostaafu wakiwa na miaka miaka 65 na waendelee hadi wanapofikisha miaka 75 au watakapokuwa hawana uwezo wa kufanya majukumu yao.

Hii haina hasara kwa Serikali kwani wanapostaafu mishahara yao inakuwa bado iko kwenye ikama.

Mheshimiwa Spika, kuwaandaa hawa wataalamu, Serikali hutumia gharama kubwa sana. Tunapositisha huduma zao, vyuo binafsi huwachukua bila gharama na kuwatumia kuwajengea sifa, ilhali vile vya Serikali vinadorora.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.