Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS. MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nami ninaomba awali ya yote naomba nianze kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kutujalia afya njema. Kwa kipekee kabisa nikushukuru wewe kwa jinsi ambavyo unaongoza Bunge letu hili, lakini kwa kweli pamoja na wote wanaokusaidia ikiwa ni pamoja na Mheshimiwa Naibu Spika, na Wenyeviti wetu, kwa hakika tunaendelea kumwomba Mwenyezi Mungu awajalie heri ili mambo yaendelee kuwa mazuri kama yalivyo sasa.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo niruhusu nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kama ambavyo nilimshukuru siku ya kwanza niliposimama baada ya kupata uteuzi wa kuja kuwa Naibu Waziri katika Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Ninaendelea tena kumshukuru yeye kwa kuniamini pia naendelea kumwahidi kwamba nitachapa kazi kwa maarifa yangu yote na vipawa vyangu vyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niruhusu nimpongeze na kumshukuru sana Comrade wangu Waziri wangu Mheshimiwa George Simbachawene, Mbunge, kwa ushirikiano mzuri anaonipa mimi na wenzangu wote ndani ya wizara lakini kwa hakika uongozi wake, miongozo yake na michango yake kwa kweli inatufanya sisi ndani ya wizara kwenda katika direction nzuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa kipekee kabisa niruhusu niwashukuru sana Makatibu wangu Wakuu wawili na Naibu Katibu Mkuu mmoja; hapa nakusudia kuzungumzia Ndugu Maendeka wa Katibu Mkuu Ikulu na Ndugu Juma Mkomi Katibu Mkuu Utumishi wa Umma na Ndugu Xavier Daudi ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara yetu. Kwa hakika ushirikiano wao umekuwa ni nguzo ya mafanikio katika Wizara yetu.

Mheshimiwa Spika, sio mwisho kwa umuhimu niruhusu nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mke wangu Mama Aziza na watoto wangu wote. Kwa hakika upendo wao na kunivumilia kwao nikiwa nachapa kazi za umma ndio jambo moja ambalo linanisukuma kwenda mbele zaidi, pia bila kuwasahau wananchi wa Jimbo la Chalinze kwa ushirikiano wao mkubwa ambao wananipa. Nataka niwahakikishie kwamba Mbunge wao nipo kazini na sijawasahau naendelea kuchapa kazi nikiendelea kuwapa heshima wana-Chalinze. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba uniruhusu niingie kwenye hoja ambazo zimetajwa au zimeelezwa na Wabunge. Kwa kipekee kabisa nianze na hoja ambazo zimeelezwa na Kamati yako ya Bunge inayosimamia Wizara yetu.

Mheshimiwa Spika, katika moja ya hoja ambayo imeelezwa na kamati lakini pia na michango ya Wabunge ni hoja inayohusu eneo la TASAF. Ni hakika na ukweli kabisa maneno yote mazuri, michango yote mizuri iliyotolewa na Wabunge sisi kama Wizara kwanza nataka niwahakikishie Wabunge tunayachukua. Kwa sababu katika maelezo waliyoyatoa Waheshimiwa Wabunge yako baadhi ya maeneo ni kweli kwamba Wizara inakiri yanatakiwa yafanyike marekebisho, lakini pia yako baadhi ya maeneo wizara inakiri kwamba huenda kuna tatizo la taarifa au uaminifu wa watu wetu ambao tunawatuma kwenda kufanya kazi. Kwa hiyo nataka niwahakikishie Bunge lako, kwamba sisi kama Wizara yale maeneo yenye mapungufu tunakwenda kuyafanyia kazi pia yale maeneo ambayo yanatakiwa yaendelee kusisitizwa ni lazima tuendelee kuyafanya.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, liko eneo la utambuzi ambalo limelalamikiwa sana na mimi binafsi yangu nimshukuru sana Mheshimiwa Aida Khenani ambaye alichokoza hoja asubuhi wakati wa maswali ya msingi ndani ya Bunge lako.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba eneo hili limekuwa na changamoto, lakini Serikali yako imekuwa kila mara inafanya utaratibu wa kuhakikisha kwamba jambo hili linabadilika au linaboreka ili kuweza kuhakikisha wafaidika wa TASAF wanapata faida ya mradi huu. Katika miaka hii ya karibuni nataka nilihakikishie Bunge lako na nitoe taarifa kwamba Serikali imekuja na utaratibu wa kuelekeza Serikali zetu za Vijiji kuhakikisha kwamba mikutano ya vijiji inawakusanya watu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesikia yapo baadhi ya malalamiko juu ya siasa kuingizwa katika taratibu hizi. Nataka niwahakikishie Wabunge na hasa kwako, sisi kama Wizara tunalibeba hili jambo la mwingiliano au mgongano wa maslahi ya kisiasa na tutakwenda kulifanyia kazi ili kuondoa vilio vya Bunge lako. Pamoja na hilo pia baadhi ya Wabunge wamezungumza juu ya malipo madogo ya wafaidikaji wa TASAF. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie wananchi hawa kwamba, Serikali imefanya juhudi kubwa sana. Mwaka 2022 wakati tulipoanza mchakato wa mjadala wa kupitia tena mafanikio ya TASAF, hili jambo lilionekana na tulifanikiwa kupeleka ile pesa wanaolipwa wafaidikaji mpaka Sh.3,000, lakini ni kweli hali za maisha zimebadilika na hitajio la kuongeza linafanyika. Sasa ninapozungumza mchakato wa kujadili taarifa na kuthamini utekelezaji wa Mradi wa TASAF, awamu ya tatu, kipande cha pili unaendelea.

Mheshimiwa Spika, tutakapofanikiwa kumaliza uchambuzi huo, nataka nilihakikishie Bunge lako na Watanzania na wafaidikaji wa TASAF kwamba changamoto kama hizi ambazo zinaonekana ni moja ya jambo ambalo tunakwenda kulishughulikia na tutakuja kuleta mrejesho hapa ili wananchi na Wabunge wapate kuelewa kwamba Serikali yao ni sikivu na Mheshimiwa Rais, anaendelea kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka vilevile niwatoe wasiwasi ndugu zangu Watanzania, Mradi wa TASAF huu kwa kutegemea pesa zetu za ndani, siyo rahisi kuweza kuwafikia watu wote. Nchi yetu haiishi katika kisiwa, nchi yetu inashirikiana na nchi mbalimbali, wahisani mbalimbali ili kuhakikisha kwamba programu za maendeleo ya nchi na watu wake zinakwenda mbele. Hivyo, hawa watu wote au wadau wote tuliyowataja katika taarifa yetu ya mwanzo ni wazi kwamba wanatusaidia sana Watanzania ili tuweze kufikia miradi vizuri.

Mheshimiwa Spika, katika kufanya hilo, moja ya mafanikio makubwa tuliyoyapata ni sasa Mradi wa TASAF umeweza kufikia kaya zisizopungua 2,300 ambayo ndani yake ina wafaidikaji wasiopungua 5,200,000 ambao wao ni Watanzania wenye uhitaji ambao Serikali yao inaendelea kuwaangalia.

Mheshimiwa Spika, nataka nikuhakikishie kwamba, changamoto nyingine zote ikiwepo changamoto ya NIDA tutaendelea kuifanyia kazi na sisi tunaendelea na mazungumzo na wenzetu wa Wizara ya Mambo ya Ndani na Idara husika inayohusika na Vitambulisho vya Taifa ili kuweza kuwafikia wananchi ilimradi waweze kufaidika na programu hii ya TASAF. Kwa wale ambao hawana vitambulisho vya NIDA, maelekezo yamekwishatolewa kwamba waende kwa sababu utambuzi wa kwanza ni katika ngazi yao ya kijiji tutawatambua na kuwaingiza katika mfumo ili waweze kuendelea kufaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo pia limezungumzwa jambo la ajira katika maeneo ya vyuo vikuu, aliyezungumza ni Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo na nataka nikiri mbele ya Bunge lako kwamba, maelezo aliyotoa Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo yana ukweli kabisa, nini kimefanyika na nini kimetufikisha hapo, kwa muda nisingependa nirudi huko, lakini Serikali ilishakutana na Uongozi wa Vyuo Vikuu vya Umma wakiongozwa na Dean wao ambaye ni Vice Chancellor wa Chuo cha Ardhi kilichopo Dar es Salaam. Mazungumzo yamefanyika nimwombe Mheshimiwa Kitila Mkumbo na wenzake katika eneo la chuo kikuu watupe nafasi Serikali tupate kuangalia, nini zilikuwa sababu za kufika hapa tulipofika na nini kifanyike ili tuweze kuondoka hapa tulipofika twende mbele kwa kasi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nikuhakikishie na Bunge lako kwamba si nia ya Serikali kuchukua mamlaka ya vyuo vikuu na kuyafanya ya kwake, lakini zipo kada mbalimbali, zipo kada za administrations au eneo la kiutawala, lakini pia zipo kada za Walimu au kwa maana ya Wakufunzi wetu. Kada hizi mbili treatment zake ni tofauti ndugu Watanzania. Kada ya Administrations imeendelea kubaki chini ya utumishi, lakini pia kada ya wale wenzetu ambao ni wakufunzi imeendelea kuratibiwa katika jicho la mbali, lakini mambo yote yanaendelea kufanyika ndani ya vyuo vikuu vyenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, liko jambo limezungumzwa na walio wengi juu ya malipo ya madai ya malimbikizo ya mishahara. Ni kweli zipo kazi na juhudi kubwa ambazo Mheshimiwa Rais wetu anazifanya katika kipindi cha miaka miwili zaidi ya Shilingi Bilioni 2.4 zimelipwa kwa wale ambao walikuwa wanadai malimbikizo. Hata hivyo ni kweli kama walivyosema, kwenye Taarifa ya CAG inaonyesha kwamba bado ile ada ya malipo imeendelea kupanda juu. Nataka nilihakikishie Bunge lako, katika kipindi cha miaka miwili Mheshimiwa Rais, ameweza kulipa nusu ya yale ambayo anayodaiwa.

Mheshimiwa Spika, lingine kubwa, nataka niliambie Bunge lako, Serikali hii imechaguliwa kawa kipindi cha miaka mitano. Tumpe nafasi Mheshimiwa Rais aweze kufanya, kama ndani ya miaka miwili ameweza kulipa nusu ya madeni yanayodaiwa, iweje ashindwe katika miaka mitatu iliyobakia! Nataka niwahakikishie kuwa, tunaye Rais ambaye anawapenda na kuwajali watumishi wa umma, tunaye Rais ambaye anawapenda na kuwajali Watanzania katika hali zote. Tumpe nafasi Mheshimiwa Rais na sisi wasaidizi wake, nataka niwahakikishie kwamba madeni na malimbikizo yote wanayodai watumishi wa umma katika Tanzania tunakwenda kuyamaliza na kwenda kuyafikia yote katika maeneo yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile pamoja na hilo nataka nizungumzie juu ya uwiano wa watumishi wa umma katika vijiji na mijiā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA. Dakika tatu malizia muda wako, kengele mbili zilishagonga.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, kupitia watalam tulionao wa TEHAMA mfumo kwa ajili ya kuchakata na kujua idadi ya watumishi katika maeneo yote ikiwemo mijini na vijijini umekamilika na unafanya kazi. Mfumo huo unatambulika kama HR Assessment, mfumo huu unawezesha siyo tu Serikali lakini pia hata Serikali za Mitaa kujua idadi ya wafanyakazi katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kupitia mfumo huu, inatuwezesha sisi kuweza kupanga pia ikama za wafanyakazi katika maeneo hayo. Nataka niwahakikishie Watanzania na Bunge lako kwamba Serikali imejizatiti kimifumo kuhakikisha kwamba changamoto zote zilizopo katika maeneo haya tunazikabili na kuzitatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako mengi ya kuzungumza, lakini naomba kwa ruhusa yako sasa nimkaribishe Mheshimiwa Waziri ili aweze kuendelea hapa palipobakia. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)