Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, Dkt. Tulia Ackson, Waheshimiwa Wabunge, awali ya yote napenda kuchukua nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha na kutuongoza katika kusimamia mjadala wa Bunge wakati wa hoja ya Bajeti Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango yao na hasa Kamati ambayo inaongozwa na watu mahiri sana Dkt. Mhagama pamoja na Makamu wake. Kwa kweli Kamati hii imetusimamia vizuri na hata kufikia hatua kwa kweli Kamati inastahili sifa kwa sababu tumetumia nao muda mwingi lakini pia wamekuwa watu wema sana katika kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya yote yamefanyika kwa sababu wachangiaji wote wamejikita katika kutuwezesha kutekeleza majukumu tuliyokasimiwa na Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania sambamba na kutatua changamoto za waajiri, watumishi wa umma na hatimaye kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, sote tunafahamu na tumesikia katika michango ya Waheshimiwa Wabunge waliyowengi hakuna ambaye hakumpongeza Mheshimiwa Rais. Tunawashukuru sana kwa pongezi zenu kwa Mheshimiwa Rais na tutazifikisha salamu hizi ingawa alikuwa anasikia. Bila shaka sote tunafahamu dunia ipo katika mazingira magumu sana kutokana na majanga mbalimbali, lakini nchi yetu iko salama salimini. Iko salama kiuchumi, kijamii, kiulinzi na iko salama kidemokrasia na ndiyo maana nchi imetulia chini ya Uongozi wa Mama yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, michango iliyosemwa hapa mingi pamoja na Kamati kuwa imekuwa na mchango wa uongozi, lakini ni kama imejirudia kwenye maeneo yaleyale yaliyosemwa na Kamati, tukiichukua michango yote. Wachangiaji waliyochangia kwa kuongea ni 25 na waliyochangia kwa kuandika ni wawili uki–group michango hiyo yote unaikuta imejikita katika maeneo takribani 15.

Mheshimiwa Spika, maeneo haya 15 ni haya yafuatayo na kwa sababu ya muda pengine nisipate fursa ya kuweza kuyamaliza lakini michango hii ilikuwa ni mizito, ni muhimu kwa Taifa letu, ni muhimu kwa umoja wa Taifa, ni muhimu kwa maendeleo ya Taifa letu, lakini pia ni muhimu kwa ustawi wa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa maneno ya dakika 20 sidhani kama naweza nikatosheleza sana, lakini nitajaribu hata hivyo kupitia baadhi ya maeneo kwa haraka ili angalau iweze kuwasaidia Waheshimiwa Wabunge kuweza kutupitishia bajeti. Tukishapitisha bajeti maana yake siyo kwamba tumefika mwisho wa kuwasikiliza, tutaendelea kuwasikiliza na kuboresha eneo hili.

Mheshimiwa Spika, kama mnavyofahamu masuala ya ajira kwa utumishi wa umma ni mhimili muhimu sana katika usalama wa nchi. Watumishi wa UMMA NA UTUMISHI WA UMMA kwa ujumla ni rasilimali muhimu sana katika maendeleo na mshikamano na umoja wa Taifa lolote lile. Mathalani ili kuweza kuajiri watu wanaotosha, ili kuweza kuwalipa mishahara watumishi wakaridhika kabisa, kabisa, hakuna nchi imefikia kiwango cha asilimia 100. Katika kila nchi yako madai, watu wanadai kwa viwango tofauti na pengine nchi yetu inaweza ikawa imefikia hatua nzuri sana katika kuutunza na kuusimamia utumishi wa umma tofauti hata na nchi nyingi zinazotuzunguka. (MakofI)

Mheshimiwa Spika, mnasikia wenyewe baadhi ya nchi sasa hivi hata kulipa mishahara ni tatizo, lakini sisi wananchi wetu wanalipwa mishahara. Kama mishahara kulipa ni tatizo utazungumzia ajira mpya? Siyo rahisi kuzungumzia ajira mpya. Kama kulipa mishahara ya watumishi siyo rahisi, utasimamia utendaji wa kazi? Siyo rahisi kuusimamia utendaji wa kazi. Kwa hiyo, tujivunie na tujipongeze kwamba mpaka sasa pamoja na changamoto za kidunia na majanga mbalimbali, Taifa letu na nchi yetu iko salama na tunaenda vizuri. (MakofI)

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema nitoe mfano tu, mishahara lazima iendane na pato la Taifa, haipangwi tu, lazima unapoipanga mishahara iendane na mapato ya ndani ya nchi yetu na uwezo wa uchumi. Tunaweza tukalipana tunavyotaka, liko Taifa moja duniani siwezi kulisema hapa, limewahi kuamua kupanga mishahara kadri ya maneno, wakaachana na uhalisia, Taifa lilianguka na mpaka leo Taifa hilo halijawahi kusimama, liko America huko. Halijawahi kusimama pamoja na u–giant wake kwa sababu walikosea tu kwa kipindi cha makubaliano ya hela, baadaye kutoka kule ikawa ni ngumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mathalani kwa mwaka 2020/2021, Bajeti ya Mishahara ilikuwa ni trilioni 7.7, wakati mapato ya ndani yalikuwa ni trilioni 24, hii ni sawa sawa na asilimia 32. Mwaka 2021/2022, Mishahara ilikuwa ni trilioni 8.1, wakati mapato ya ndani yalikuwa ni trilioni 26.3. Mwaka 2022 Mishahara ilikuwa ni trilioni 9.8 na pato la Taifa lilikuwa ni trilioni 28, sawa sawa na asilimia 34. Sasa hivi kwa Bajeti ya 2023/2024 tutakwenda trilioni 10.8 wakati mapato ya ndani ni trilioni 31, tayari asilimia 35.

Mheshimiwa Spika, kuna standards za Kimataifa, uki – break hiyo ni lazima utaingia kwenye crisis ya uchumi. Maslahi haya tunayopigia kelele, walipwe vizuri, wafanywe nini watu hawa hawazidi milioni moja, ni laki tano na sitini plus. Sasa tukitaka hawa wapate sana maana yake tusimamishe miradi mikubwa ya maendeleo. Tunazungumzia idadi ya watu chini ya milioni moja, chini ya Watanzania walio sasa karibu milioni 62. Sasa hapa tunazungumza maslahi ya watu hawa tu, ingawa wanafamilia zao, lakini tunazungumzia maslahi ya hawa watumishi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tuwe makini tunapotaka kuzungumzia maslahi, tuangalie pia na miradi na mambo mengine ambayo yatabeba uchumi huu ili kujenga uchumi na baadaye tuje tumalize haya yabebe na maslahi ya watumishi. Kwa hiyo hatuwezi kwenda kwenye perfections a hundred percent, lakini tumejitahidi na tuko vizuri kama Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niliona nianze hapa ili tuwekana vizuri, tunaweza tukadai chochote kile tukasema chochote kile, lakini tufahamu kwamba lazima tuendane na uwezo wa uchumi wetu katika kuweka maslahi ya watumishi wetu.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili lililozungumzwa ni nafasi za kazi kugawanywa katika halmashauri ili kuwe na usawa katika kuajiri watumishi wa umma. Sera ya Menejimenti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, Toleo la Pili la Mwaka 2008, kifungu cha 4(2) inatamka kuwa ajira zinatakiwa kuwa za ushindani na zifanyike kwa kuzingingatia miundo ya kiutumishi (Schemes of Services).

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge hapa wamezungumza kwa hisia kubwa sana kwamba tugawane kwa sababu hatuoni uhalisia, hazigawanywi sawasawa. Hata hivyo, nataka niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge, kwamba huko nyuma hatukuwa na Sekretarieti ya Ajira na tatizo lilikuwa kubwa kuliko hili la leo. Ni bora leo tumeweka Sekretarieti ya Utumishi wa Ajira na kuweka ajira zetu ziwe centralized, tunaweza tukaona hata hayo mapungufu.

Mheshimiwa Spika, huko nyuma tulikokuwa hata hayo mapungufu kuyaona ilikuwa ni vigumu. Tunafahamu zilikuwepo baadhi ya taasisi ambazo ulikuwa unakuta watu wa ukanda fulani, watu wa maeneo fulani ndiyo wameajiriwa pale, leo kuna hata afadhali unaweza ukasema Hapana, mbona kwangu sijaona, mbona kwangu sijaona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo msukumo wa haya yote na tulipofika pamoja na pengine mapungufu ya mfumo ulioko sasa, lakini tumefika hapa kwa sababu wanaomaliza katika vyuo na kutegemea kuajiriwa na Serikali ni wengi kuliko nafasi zilizopo. Nilikuwa naongea na Waziri wa Elimu tunavyo Vyuo vya Ualimu mathani 35 vya Serikali, weka na vya binafsi tuchukulie kila chuo wakamaliza wanafunzi 200 tu katika hivyo vyuo 35, tutakuwa na wahitimu wangapi? Watakuwa karibu 7,000.

Mheshimiwa Spika, hapa hatujaweka na vyuo binafsi, so in average tuna wahitimu wa nafasi za Ualimu kwa ngazi tofauti tofauti karibu 15,000 kila mwaka. Ajira za Walimu zinazotoka mathalani zilizotoka kwa mwaka 2022/2023 ni 13,000, tayari wahitimu wamezidi idadi ya nafasi zilizopo. Kwa hiyo kumbe kuna makosa ambayo tuli–over plan na mkumbuke kwa nini Walimu?

Mheshimiwa Spika, Walimu wamekuwa wengi kwa sababu tulikuwa na uhaba wa Walimu wakati tulifungua shule nyingi, shule za kata ambazo zikahitaji Walimu, tukakosa Walimu, ndiyo tukaja na vodafasta, we had no Teachers. Tuliposema hivyo vyuo vikafunguka, kila mtu anajua huku ndiyo kwenye mikopo, kwenye nini? Ndiyo sababu tukapeleka wanafunzi wengi na fursa zikafunguka pale, sasa tumewa–over training Walimu. Kwa hiyo kuna haja ya kufanya u–turn na kupunguza. Sasa hili ni jambo ambalo sekta na yenyewe watatusaidia katika kufanya hayo.

Mheshimiwa Spika, sasa hili siyo jambo la kiutumishi peke yake, lakini jambo ni kwamba tuna walimu wengi lakini nafasi ni kidogo, kwa hiyo ugomvi huu wote na mivutano hii yote inatokana na sababu hiyo. Niseme tu kwa sababu ya nafasi ndogo tutajitahidi, ni bora tukabaki katika mfumo uliopo tukauboresha kwa kutumia mawazo haya mlioyasema, kuliko tukazichukua hizi nafasi mkasema tugawane. Nilikuwa naangalia kwenye group letu la party caucus tukigawana tutapata kila mmoja 112, haya nipeni mimi nichukue 112 niende nazo kwenye Jimbo langu la Kibakwe, nikifika nazo tu pale Kibakwe kila mmoja anajua Mbunge ndiyo anaetoa hizi ajira, wanakuja kujaa kwangu. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nikishapewa hizo ajira 112 ambazo mmenigawia za Jimbo la Kibakwe, Mfuko wa Jimbo wenyewe mnajua Madiwani tunavyohangaishana nao, kwa hiyo Madiwani na wenyewe watasema tugawane, kama ni 112, unapata 20 haya tugawane kila mmoja kila Diwani anapata Watatu, ikifika kule Diwani nae ataambiwa Mwenyekiti wa Kijiji atasema tugawane, automatically zitakuwa hazitoshi na tutaleta crisis na ugomvi zaidi, isipokuwa tunachoweza kufanya ambacho tunafikiria kwenda kufanya ni kutumia mawazo haya ya kuhakikisha kwamba waajiriwa wa nchi hii wanatoka maeneo yote kwa sababu utumishi huu ni utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mnakumbuka Waheshimiwa Wabunge, tunayo Majimbo yetu na tumekuwa tukiomba vibali vya Halmashauri kupata ajira na tumekuwa tukipewa zile ajira 15, 16 za wale Watendaji wa Vijiji na nini na nini. Niambieni nani, zimebaki katika Jimbo lake zote? Zikifika kule Mkuu wa Wilaya anataka Ndugu yake awepo, Mkuu wa Wilaya anatoka Kibakwe? Afisa Utumishi hatoki Kibakwe, anataka ndugu yake awemo, DSO anataka ndugu yake awemo, Mkurugenzi anataka ndugu yake awemo, Afisa Mipango anataka ndugu yake awemo. Hawa wote hawatakuwa wametoka Nkasi, hawa wote watakuwa wamekuja na vyeo vyao na wao watakuwa ndiyo wanakaa kwenye ile panel na ndiyo wenye nguvu, wanazichukua zile zote matokeo yake wa pale Nkasi, wa pale sijui Peramiho hapati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hilo lenyewe tuko kule sisi limetushinda. Tukisema tuchukue zile ndiyo kabisa! Kwa hiyo, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge wazo ni zuri, acheni tukae tutulie. Suala la Utumishi wa Umma ni suala la usalama wa nchi. Nchi hii imewekwa katika misingi mizuri sana na haya mambo yanayochipuka ni ya mtu mmoja mmoja lakini kuna ukweli kwa maneno haya mnayosema ninyi Viongozi mnaowakilisha watu kwamba kuna upendeleo tunaona kuna harufu, hawezi akawa mtu mzima hapa nikasema haupo haiwezekani! Yako maeneo upendeleo upo na yapo maeneo yako vizuri, lakini lazima turekebishe na kurekebisha kwenyewe hatuwezi kuvunja kitu ambacho kipo kizuri, tukaanzisha ambacho hatukijui hatma yake.

Mheshimiwa Spika, nakubaliana tutachukua mawazo haya, will make a system ambayo hata katika uombaji tu pale tuta–control. Hebu waombe wenye address inayojulikana kama anatoka Dodoma Mjini au maeneo haya hatuzungumzii makabila sisi tunazungumzia originality ya mtu alikosomea na wazazi wake na alikozaliwa, hilo linawezekana kufanyika na zikapatikana katika mtandao na msambazo ambao upo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumetengeneza mifumo, bajeti hii ya safari hii ni bajeti ya mifumo. Tunataka kuimarisha nguvu ya mifumo. Kuna mifumo mipya iliyojengwa zaidi ya 15. Mifumo hii itatusaidia sana katika kudhibiti. Nimpongeze sana Mheshimiwa Jenista Mhagama kwa kusimamia na kuanzisha mifumo hii ambayo mingi yake bado hatujaanza kuitekeleza kwa asilimia 100, lakini ipo mifumo mipya.

Mheshimiwa Spika, ipo mifumo ambayo itatusaidia katika kusimamia utendaji kazi wa watumishi, iko mifumo itakayotusaidia katika kuhakikisha mtumishi mmoja mmoja yuko wapi na anafanya nini, iko mifumo ambayo itatusaidia suala la ulipaji wa mishahara na taarifa za kila mtumishi na uki-press mimi nilifanyiwa majaribio na nimeweza kuona just press in real time you get wherever you want, wapi kuna upungufu wapi kunaongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii tunaupungufu wa walimu wa hesabu, masomo ya sayansi 11,336. Ajira zilizotoka za Walimu ni 13,000. Ukitaka hapa ugombane hapa na Waheshimiwa Wabunge useme tunaajiri walimu wa masomo ya sayansi tu, hapa watu wao wana masomo ya arts, nini na nini utasikia vurugu, hata huko kwenye maofisi ni vurugu. Wanaanza tuweke kidogo, lakini kimsingi tunao walimu wa masomo ya arts wengi wamepitiliza hatuna hata pa kuwaweka. Tulio na shida nao ni hawa wa masomo ya sayansi, Chemistry, Physics, Biology na Hesabu.

Mheshimiwa Spika, tuchukue basi haya tuamue hapa, tuchukue zote hizi tuseme tunawapa walimu wa hesabu kupunguza gap, utasikia tu. Kwa hiyo, nasema Waheshimiwa Wabunge tuachieni tutafakari Serikali hii ni Serikali yenu. Ushauri wa Waheshimiwa Wabunge na Bunge hili hauishii kwenye kupitisha mafungu tu ya bajeti hii, uendelee hata nje ya hapa na nina wakaribisha na Mheshimiwa Spika nimechukua maoni yako, lazima tulete semina, kwa sababu moja kati ya misingi ya utawala bora ni uwazi. Moja kati ya misingi muhimu ya utawala bora ni uwazi. Hatutaficha chochote tutaleta hata mifumo ambayo bado hatujaimalizia kwa ajili ya majaribio tuje tufanye semina na Waheshimiwa Wabunge waone hali halisi ilivyo ili wakitushauri tushauriane vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mambo ni mengi lakini muda ni mdogo hata hivyo yamesemwa maeneo mengi sana. Ucheleweshaji wa uwasilishwaji wa michango ya katika Mifuko ya Jamii wastaafu, hili tutaendelea kulisimamia. Tumetengeneza mifumo ambayo itahakikisha ina - link na PSSSF na mishahara ambapo mfumo huo wenyewe ukiubonyeza tu hivi hakuna mtu anayeweza akafanya chochote hata yule wa PSSSF anaweza asifanye chochote mpaka mwajiri atoe mchango wake na muajiriwa naye atoe mchango wake iingie kwa pamoja. Haipokewi tofauti tofauti. Kwa hiyo, hiyo itafanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Spika, eneo jingine lililozungumzwa ni watumishi wa umma kukaimu nafasi za uongozi kwa muda mrefu. Hili tatizo linawezekanika ni la kiutendaji tu, ni very administrative tutaliwekea utaratibu ambao tutahakikisha kwamba na lenyewe hili linakwisha. Watu wanakaimu muda mrefu na wakati wengine wana sifa. Watu wanakaimishwa wakati hawana sifa na watu wanazulumiwa wenye sifa kuingia. Kwa hiyo, kote kuna matatizo. Mtu anakaimu na sheria inasema kukaimu mwisho ni miezi Sita, lakini mtu anakaimu miaka 10. Sasa huyo ni Kaimu huyo si tayari tu na wakati huo ukimleta mwingine unaleta ugomvi na conflicts kubwa sana ambazo zinapelekea. Kwa hiyo, nakubaliana na Waheshimiwa Wabunge kuhakikisha kwamba eneo hili tunalifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, matumizi ya kanzidata katika kuajili watumishi wapya ili kupunguza gharama za Serikali. Yes, haya mawazo yalikuwa ni ya Waheshimiwa Wabunge ya bajeti iliyopita na Mheshimiwa Jenista Mhagama aliyachukua na wamekwenda kutekeleza, kanzidata ipo hawarudii tena kufanya interview na sasa tukaongeza mpaka na muda wa kukaa kwenye kanzidata kufika mwaka mmoja, ile system inafanya kazi.

Mheshimiwa Spika, mimi niliambiwa na Waheshimiwa Wabunge nisaidie kuna kijana wangu alifanya interview na nini na nini, nimeshangaa jana ananishukuru. Ananishukuru nini? Anasema amepata ajira, kumbe wali- upload jana, walitoa jana, wametoa. Sikufanya mimi ila nashangaa nashukuriwa na Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi na ninyi kuna watu wanawashukuru lakini hamkufanya chochote. Ni system ya Sekretarieti ya Ajira inafanya kazi katika merits kwa uwazi na kwa ukweli. Kwa hiyo, hili jambo limefanikiwa ni mawazo yenu. Amini Serikali, muamini kwamba kuna watu wakweli, ingawa kama kuna wazembe ni wachache wanaotupotosha.

Mheshimiwa Spika, eneo jingine lilikuwa ni usaili unaoendeshwa kufanyika ngazi ya Kanda badala ya Dodoma ikijumuisha matumizi ya TEHAMA. Mfumo upo tayari, tumetengeneza mfumo unaitwa online aptitude testing system ambao huu mfumo sasa watafanya usaili hukohuko kwenye Kanda wala hakuna sababu ya kuja Dodoma. Watafanya kwenye Mikoa watafanya kwenye Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo jingine ni kuajiri kwa kigezo cha miaka, kwa Jeshi USU, hili tutajaribu kuwasiliana na Wizara ya Kisekta, tuweze kuona changamoto inatokana na nini je, ni lazima kweli kuangalia umri kwa sababu miaka ya 28 mtu akifanya kazi miaka 30 atakuwa na miaka mingapi? Tuangalie tutawasiliana na Wizara ya Kisekta.

Mheshimiwa Spika, pia kuhusu ajira za kujitolea. Ni kweli kulikuwa hakujawekwa utaratibu mahsusi kwa ajili ya ajira za kujitolea. Ziko nchi ambazo ajira za kujitolea volunteers ndizo zinazoendesha na zinazosaidia na ku – supplement gap ya Watumishi wa Umma. Kwa nini sisi tukiwa tuna watu wengi na tume-train sisi wenyewe kwa hela za Serikali, watu wana ujuzi badala ya kumkuta mtu anafundisha na anapenda kufundisha unamkuta anaendesha bodaboda. This is not right!

Mheshimiwa Spika, nadhani tukubaliane Waheshimiwa Wabunge na sisi Serikali tunachukua mawazo haya ni lazima tukatengeneze mfumo mahsusi utakao angalia pia hata wanachostahili hicho kidogo, kwa sababu huyu mtu hawezi kujitolea asipate kitu kabisa hataweza kwenda. Anahitaji kufua, anahitaji usafiri. Lazima kuwe kuna utaratibu ambao tuuweke ikibidi hata kutenga bajeti kidogo tutenge tuseme tunahitaji wangapi wa afya, wangapi wa elimu halafu waweze kupata na wafanye kazi huku wakingojea kuajiriwa. Unakuta hawa walioajiriwa pengine hata siyo wazuri sana kuliko hawa wanaojitolea. Inauma wakati mwingine unapokuta haya yanatokea, hili tumelichukua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, urejeshaji wa michango ya watumishi walioondolewa kazini wa kubainisha kuwa na vyeti vya kugushi. Mpaka sasa hivi madai 11,896 yenye jumla ya Shilingi Bilioni 35.02 yamelipwa kati ya madai 12,662. Waheshimiwa Viongozi wenzangu, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Serikali hii inaongozwa na Mama huyu ana huruma sana, jambo hili lilikuwa limekwisha, kukubali kutoa Bilioni 35 ni huruma ya Mheshimiwa Rais. Alisema wapeni fedha zao kwa sababu walifanya kazi lakini jambo lilikuwa limeisha.

Mheshimiwa Spika, katika muda wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu, mambo mengi ya kiutumishi yaliyokuwa yanapigiwa kelele yametatuliwa. Kwa upande wa Watumishi na Vyama vyao vya Watumishi wenyewe huko wanaimba tu ‘iyena iyena’ ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu, haya mengine tunayoyasema huku wala huko hayapo kwa sababu wamefanyiwa mambo ambayo hawakuyatarajia. Kweli kabisa tuwe wakweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ni nyongeza ya mishahara imefanyika, kama ni malimbikizo yamelipwa, hakuna ambacho hakijaguswa niwaambie ukweli Waheshimiwa. Sasa nyingine ni kurudisha posho ya kufundisha teaching allowance. Teaching allowance hii iliingizwa kwenye mishahara kwa sababu ilikuwa haina impact katika mafao. Kwa hiyo, ikaamuliwa na wahusika wenyewe Walimu kwamba hii posho mnayotupa hai - effect positively mafao yetu. Kwa hiyo, utaratibu ikaonekana basi kuwasaidia angalau wawe na kitita angalau kizuri iingizwe kule kenye mshahara. Imeingizwa tushasahau sasa tunakuja kudai tena. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sasa mimi niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge wacha tukatafakari, tuwaulize na wenyewe maana hapa kuna walimu mliostaafu, Walimu wenyewe wako kule nje, ninyi mmekuja kuwasemea. Tumewasikia mmewasemea, lakini tukawaulize na wao mnasemaje tunyofoe huku tuwaletee huku au tuiache huku isaidie kwenye mafao? Watasema wao kwa sababu wana vyama vyao.

Mheshimiwa Spika, waraka wa mwaka 2014 kuhusu viwango vya mshahara, posho wa viongozi wa elimu unaotekelezwa kwa Wakuu wa Shule lakini hautekelezwi kwa Wadhibiti Ubora. Wadhibiti Ubora kulikuwa kuna mkanganyiko wa viwango, mkanganyiko wa viwango ikaonekana huu waraka ukasitishwa na Wizara ya Elimu tutawasiliana na Wizara ya kisekta ambao hawa wadhibiti ubora wako kwao, kwamba baada ya kusitisha wamekuja na solution gani na kwenye hotuba yao wanaweza wakaja kuisema vizuri.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni kuhamisha umiliki wa ndege za Wakala wa Serikali TGFA kwenda Kampuni ya Ndege ya Tanzania. Waheshimiwa Wabunge na Waheshimiwa Viongozi wenzangu kulikuwa kuna sababu za msingi sana za kiusalama pia usalama wa rasilimali hizi za Watanzania. Pengine mawazo yale na sababu zile zinaweza zikawa zimepitwa na wakati na pengine wazo hili la kuzifanya ndege hizi zimilikiwe sasa na ATCL kwa sababu ni shirika la Kiserikali, TGFA ni wakala wa Serikali, ATCL ni Wakala wa Serikali. Mimi sioni kama kuna tatizo just give us time. Tuje tuangalie zile sababu ambazo siyo rahisi kuzisema, tukaangalie tuweze kufanya hilo kwa sababu limesemwa bajeti iliyopita na limesemwa na bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhakikisha kwamba vyuo vinatoa kozi ambazo zinaendana na soko la ajira hili nimelisema, Wizara ya Elimu sasa hivi ipo kwenye mchakato wa kubadilisha mitaala na nini, lazima tuangalie pia na demands yetu. Waheshimiwa Wabunge haya yataisha tukiwa na Tume ya Mipango. Waheshimiwa Wabunge Tume ya Mipango inakuja waraka umeshatayarishwa mimi nimekwishapitisha nangojea kwenda Baraza la Mawaziri likipitishwa wakati wowote naingia nao pale kwenda kuleta iwepo hapa na ipitishwe ndani ya Bunge hili kama Spika ataruhusu na kutoa nafasi.

Mheshimiwa Spika, tuwe na Tume ya Mipango that is why are training teachers bila kujua mahitaji yetu na hata tukijua mahitaji hatuweki conditions za kujua tunahitaji nini na nini, lakini pia hata katika sekta nyingine na ndiyo maana human capital is a very basic resource katika nchi, bado inakuwa hatuijui sawa sawa kwamba tunataka nini hatutaki nini, ndiyo maana tunahitaji reform kubwa na reform basically itafanywa na mifumo ya kidigitali na artificial intelligence, lazima tufike hatua hata usaili na nini tuweke maswali pale mtu afanye asahishiwe siyo na binadamu na awe selected na artificial intelligence, badala ya kufanywa na binadamu kwa sababu huku tunatuhumiana. Kwa hiyo hili wala halina tatizo, tutahakikisha kwamba vyuo vinatoa kozi ambazo kwa kweli zina uhitaji wa watu na vile ambavyo vimehama kwenye malengo yake ya msingi vinarudi katika malengo ya msingi.

Mheshimiwa Spika, eneo la 15 ni Sera, Sheria na Taratibu na Nyaraka za Utumishi wa Umma kupitiwa kwa wakati. Mapitio yanafanyika, tutaendelea kupitia maeneo haya na kuhakikisha kwamba tunaleta mabadiliko ili reforms hizi ziendane kwanza tubadilishe sera, tubadilishe sheria na mimi nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge katika muda ambao kama Mheshimiwa Rais ataendelea kuniacha nikabaki katika Wizara hii, ambacho na mimi ninachotaka kuacha kama legacy ni kuhakikisha kabisa tunaubadilisha mfumo wa utumishi wa umma, njia pekee tayari msingi umekwishawekwa na Waziri aliyenitangulia kuhusu mifumo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la 16 na la mwisho ni kusimamia na kutoa mafunzo maalum kwa Watumishi wa Umma ili kuwezesha utendaji kazi unaozingatia weledi na ustadi. Mafunzo yanatolewa sana lakini tunaotoa mafunzo tunaelewana? Mafunzo yanatolewa sana, kila bajeti hapo kila mliyopitisha kwenye mafungu yenu kuna mafunzo, kuna kujenga uwezo, kuna kufanya nini, lakini tufike hatua sasa tuwe na a committed public service, a committed one na mtu ajue miiko na vitu ambavyo haviruhusiwi katika utumishi wa umma. Tusichanganye utumishi wa umma. Kama unataka kuwa tajiri nenda kafanye kazi kwenye private sector. Kwenye utumishi wa umma hauji kutafuta utajiri unakuja kutoa service ni wito. Tusichanganye kabisa (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mawazo mengine ya kufikiria tunaweza tukaufanya utumishi wa umma ukawa kama udalali wa kuuza vitu fulani fulani sokoni, haiwezekani! Lazima utumishi wa umma uwe na miiko na mtu ajiulize niingie au nisiingie? Lazima uwekwe ugumu fulani wa utumishi wa umma. Huwezi ukamfanya kila mtu akawa Sheikh, huwezi ukamfanya kila mtu akawa Mchungaji. Ni lazima kuwe kuna sababu ambayo inakufanya wewe uwe mtumishi wa umma. Sasa hizo ndiyo lazima tufike huko, siyo kila mtu ni mtumishi tu wa umma.

Mheshimiwa Spika, yapo maeneo ambayo lazima tulazimishe watu kuyasomea. Leo hii kuna baadhi ya maeneo tumekosa watumishi kabisa, hili siyo jambo la ajabu hata Marekani best brain huwa wanazi- retain siyo kwamba wao hawana watu ila wanajua this is the best brain na hapa kwenye eneo hili ni gumu. Ndiyo maana nendeni Marekani, nendeni wapi, nendeni kokote huko mtakuta Watanzania Wabobezi ndiyo wanaofundisha kwenye Vyuo Vikuu, ndiyo wanaoendeha taasisi muhimu kule, ni kwa sababu watu wana retain best brain, kwa sababu duniani kuzidiana akili ni kitu cha kawaida.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tutasimama na hayo na tuta-train watu wetu, wako watu wengine watasoma hata kama hawataki. Tukijua una akili utasomeshwa hiki ili uje ufanye kwa lazima, wamekuwa wakifanya hivyo hata Awamu zilizopita. Mwalimu Nyerere alifanya hivyo, Awamu ya Pili ya Ali Hassan Mwinyi imefanya hivyo, Awamu ya Tatu imefanya hivyo, Awamu ya Nne ya Kikwete imefanya hivyo. Kuna watu lazima walazimishwe kusoma! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Chamuriho huyu alilazimishwa kusoma, tena hayo masomo aliyoyasomea hayakuwa yake, akaambiwa utasoma hiki unachoambiwa kusoma, leo hii kwenye nchi ukitafuta watu walio na ubobezi katika eneo la usimamizi wa miradi ya kiinjinia huwezi kumuacha Mheshimiwa Chamuriho, lakini do we have them in the University of Dar es Salaam or other Universities? Will you find other genius? Bado tunatakiwa kulazimisha watu wetu katika kujenga mfumo mzuri wa kuhakikisha kwamba tunakuwa na watu ambao wanaweza ku-deliver na kusimamia kama nchi ili tuweze kupata maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nirudie tu kusema nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwa kusema kwa kuandika na wale ambao hawakusema kwa sababu niliziona hisia zao, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge yote mliyoyasema hapa, yote kabisa tunayachukua kwa uzito mkubwa sana na tuhakikishe kwamba nchi yetu inapata maendeleo na ustawi, kwa sababu rasilimali muhimu ni watu, kuhakikisha wanafanya kazi na uaminifu na uadilifu.

Mheshimiwa Spika, suala la utawala bora hakuna champion wa utawala bora kama Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Nimekusikia Mheshimiwa Aida Khenani hayo ni mambo madogo, makubwa yamekwisha tatuliwa, haya madogo tunawaachia watu wa chini huku watayafanya lakini nataka nikuhakikishie Rais wetu hana ubaguzi kwa misingi ya Vyama, Rais wetu hana ubaguzi kwa misingi ya dini, wala kwa misingi ya makabila wala ukanda. Ameamua kujenga nchi moja, ameamua kujenga nchi yenye mshikamano, tuendelee kumuunga mkono na nikuhakikishie jambo hilo tutalishughulikia ili tuweze kuacha kuwa na manung’uniko ya mtu mmoja mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika baada ya maneno haya, naomba sasa kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naafiki.