Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Simai Hassan Sadiki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami kuwa mchangiaji. Awali ya yote, nitumie nafasi hii kuwapongeza sana Marais wetu; Rais wa Zanzibar na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa wanazozifanya katika kuwaletea maendeleo wananchi wa Taifa hili. Baada ya utangulizi huo, napenda nianze kwa kusema kwamba, vitu vyote duniani vina mipaka, lakini hakuna kitu kinachoweza kuunganisha dunia, mataifa, mabara na nchi kwa ujumla isipokuwa mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, athari za kimazingira hazitegemei wapi uharibifu wa mazingira umefanywa. Uharibifu wa mazingira unaofanywa na wanadamu ndio unaosababisha athari za mabadiliko ya tabianchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, dunia iko busy katika kupambana zaidi na masuala haya ya mabadiliko ya taibanchi. Kwa kuzingatia hivyo, jambo hili linatupa picha wazi kwamba, issue ya mazingira ni issue ya world, cross cutting issue, siyo suala la Taifa moja, wala siyo suala la sekta moja katika nchi ambayo inastahiki kuchukua hatua. Ni lazima sisi kama nchi kila Wizara ichukue nafasi katika kukabiliana na masuala haya, kama tulivyo. Kwa sababu kila Wizara inachukua jitihada kwa njia moja au njia nyingine bila kuhusika katika uharibifu wa mazingira. Kwa nini tushindwe kuchukua jitihada za msingi kwa kila Wizara katika Serikali hii kuweza kupambana na kuweza ku-control masuala ya uharibifu wa mazingira?

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati dunia ipo katika kupambana na uharibifu wa hali ya hewa na athari zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi sisi tukiwa kama Taifa, bado sioni haja na kujigamba kwamba tunachukua jitihada za kutosha katika kukabiliana na hali hii. Kwa sababu, sisi kama Taifa kupitia chombo hiki kitukufu, Bunge, leo hii tunajadili suala la mazingira na Muungano kwa kuchanganya vitu viwili kwa pamoja, wakati vitu hivi ukiviangalia, concept ta mazingira ndiyo inayobeba agenda ya dunia nzima sasa hivi. Concept ya Muungano maana yake ni masuala ya nchi mbili. Leo hii tunajadili kwa kutumia kutwa moja, sijui kama kweli tunachukua jitihada za kutosheleza kukabiliana na hizi effects. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kwenda kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, miradi yake haitakiwi kutekelezwa kwa kutumia bahati katika majimbo. Tunatakiwa tuangalie ule uhalisia, wapi effects zinaonekana waziwazi na kwa muda gani? Sisi kama Taifa hatuwezi kwenda kumshughulikia mgonjwa aliyekuja hospitali aliyejikata wembe wakati anakata kucha, kisa kaja mwanzo, tukamwacha mama mjamzito ambaye amefika hospitali muda huu akiwa anagaragara kutokana na uchungu wa kutaka kujifungua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina maana gani? Sisi Nungwi hali ni mbaya. Mkoa wa Kaskazini kiujumla athari za mabadiliko ya tabianchi siyo jambo la kufumbia macho. Bahari, upepo, visima kujaa maji ya chumvi vinaangamiza sana Jimbo la Nungwi, Kijini na hata maeneo ya jirani. Nakumbuka mwaka jana niliuliza swali dogo la nyongeza kuhusiana na hatua mtakazoweza kuchukua kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, maeneo ya Nungwi, Mheshimiwa Naibu Waziri, Muungano na Mazingira alijibu kwamba, katika bajeti ile ya 2021/2022 watatenga fungu la kwenda kujenga kuta pale, lakini cha kusikitisha, bajeti ilipita na hakuna hata moja lililofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri alikuja Jimboni kwangu Nungwi, kaka yangu Mheshimiwa Jafo. Baada ya kuja tukaenda kukagua, lakini nasikitika mpaka leo hii bado sijaona jitihada zilizochukuliwa. Nimwambie kitu, ziara yake ilitupa matumaini sana, lakini ilikuwa aniambie tu ukweli kwamba alikuja zaidi kama ni holiday. Nikamwandalia life jacket angalau aende kuogelea na makasa na makobe kule, kama wanavyofanya watalii wengine. Kwa sababu, tulitegemea ziara ile itazaa matunda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kila siku watu wanaohusika na suala la Muungano na mazingira wanakuja eneo la Nungwi, wanapima kwa kamba, wameshakuja kupima kwa GPS, kwa tape, kila aina ya vipimo wanakuja, lakini hakuna kimoja kinachofanyika. Sasa bora tuambizane kwamba eneo lile tulihifadhi kwa ajili ya utafiti wa athari za mabadiliko ya tabianchi, ili wale wananchi tuwaondoe, tuwape ardhi sehemu nyingine kama Mwanza, Kagera, tuwatafutie sehemu ya kuishi ili pale tukatumie kwa rasilimali hiyo. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kaka yangu, Mheshimiwa Selemani Jafo, na ninafikiria watu wa Muungano na Mazingira kwa upande wa Zanzibar wananisikia; chonde chonde, umesoma bajeti lakini bado halijakuwemo. Maeneo yale yanatuathiri vibaya sana, yanatudhalilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, upo, wewe ni msikivu sana. Shauriana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Zanzibar ni Visiwa ambavyo vinaathirika kwa asilimia kubwa kutokana na staili ya mabadiliko ya tabia nchi kwa sababu tumezungukwa na bahari. Misaada inayokuja, uhisani unaokuja, ni vizuri tukaelekeza nguvu zetu kule kwa sababu athari zake zinaonekana waziwazi, hususan Nungwi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, chonde chonde kaka yangu, nakuomba kupitia Serikali hizi Tukufu, Serikali sikivu. Twende tukatekeleze ujenzi wa ukuta kuzuia bahari isiendelee kutuathiri maeneo ya Nungwi na vitongoji vyake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kaka yangu, Mheshimiwa Jafo, nakumbuka katika bajeti iliyopita vilevile kuna suala la mfuko wa jimbo. Kuna fedha za mfuko wa jimbo tulipitisha hapa kama sote majimbo ya Tanzania kwa kuongezewa. Lakini kinachosikitisha ni kwamba mpaka leo hii majimbo ya Tanzania Visiwani tunapiga zogo. Bado hatujaongezewa chochote. Fedha zile zipo kwa ajili ya kwenda kuipa support miradi ambayo haikupata fungu katika bajeti. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Haikupata fungu…

NAIBU SPIKA: Taarifa, taarifa Mheshimiwa Simai.

TAARIFA

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaelewa sana tatizo analolizungumza Mheshimiwa Simai la fedha za mfuko wa jimbo. Naomba tu nimpe taarifa na kumhakikishia kwamba Serikali imeshalifanyia kazi na muda si mrefu kadhia hiyo itakuwa imeshatatuliwa kupitia Wizara ya Fedha, na Waheshimiwa Wabunge wote wa Zanzibar watapatiwa fedha hiyo. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante; Mheshimiwa Simai, taarifa hiyo.

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa hiyo, ahsante sana. Lakini fedha hizi tukumbuke kwamba zipo kwa ajili ya kuchochea maendelea ambayo ni miradi ya wananchi ambayo haikuwa kipaumbele katika miradi iliyotengewa fedha kwa ajili ya bajeti. Sasa niiombe Serikali tuharakishe mchakato huu wa mfuko wa jimbo na sisi Wazanzibari tupate hiyo haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana.