Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii nami nichangie Wizara hii muhimu, hasa kwa uchumi wetu. Nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais pamoja na Waziri wa Madini kwa kazi nzuri waliyoifanya kuisimamia hii sekta ya madini ambayo imeonesha mwelekeo mzuri. Ukiangalia hata kwenye pato la Taifa sekta ya madini imekuwa ikichangia kwa wastani mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Tanzania siyo kisiwa, ni sehemu ya dunia na tunaona mabadiliko makubwa ya kiuchumi duniani. Nasi rasilimali zetu tulizonazo inabidi tuzitumie vizuri na rasilimali mojawapo ambayo inaweza kuibadilisha Tanzania kwa haraka ni hii sekta ya madini. Speed tuliyonayo pamoja na hayo mafanikio, inabidi iongezwe kidogo kwa sababu, ukiangalia mtangulizi wangu hapa amezungumzia kuhusu mradi wa Mchuchuma au Liganga na Mchuchuma. Angalia muda mrefu ulivyopita, lakini kuna miradi mingi ambayo inaendana pamoja na hiyo, kwa sababu, hizi rasilimali tusipozitumia leo baadaye zinaweza kugeuka zisiwe na thamani tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Wizara iangalie namna gani kwa kushirikiana na Wizara nyingine Serikalini kuvutia wawekezaji ili kuhakikisha hizi rasilimali zinabadilishwa na zinatafsiri kuongeza uchumi wa nchi yetu. Kwa hiyo, napendekeza Serikali ichukue hatua za haraka kuhakikisha kuwa miradi kama Liganga na Mchuchuma inaenda kwa speed ya haraka ili tupate pesa za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi mingine ambayo enaendana sawa na Liganga na Mchuchuma, kuna mradi wa Niobium hapa. Nafikiri Mheshimiwa Waziri nisingesema hili neno angenishangaa. Nitaendelea kulisemea hilo kwa sababu inaelekea wenzetu bado hawaoni zile fursa tulizonazo kama Tanzania. Kuleta kiwanda cha uchenjuaji Niobium cha kwanza Afrika, cha nne duniani na mahitaji ya ferroniobium ni makubwa mno duniani. Kwa kweli ni jambo ambalo linabidi lichukuliwe kwa haraka ili Tanzania ibadilike hapa tulipo. Tumekuwa tukifanya vizuri kwenye uchumi wa nchi yetu, lakini hatujafanya vizuri sana kama tungeweza kutumia rasilimali hizi tulizonazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ferroniobium ninayoizungumzia ambayo inapatikana Mbeya, yale madini ndiyo yangetumiwa kwenye ujenzi wa madaraja yetu, ujenzi wa reli yetu tunayoijenga sasa hivi, na vilevile haya madini yanahitajika zaidi huko nje. Ukiwa na hiki kiwanda ina maana hata nchi Jirani, haya madini yao yatakuja kutengenezwa au kuongezwa thamani hapa nchini kwetu. Kwa hiyo, naona kabisa ya tunaitaka Tanzania ya viwanda. Kwa hiyo, ukiwa na kiwanda cha namna hii, ndiyo unafikia yale malengo ambayo yamo kwenye millennium goals. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, baada ya kulisema hilo, kwa ajili ya muda, mwenzangu amezungumzia kuhusu umuhimu wa dhahabu kuwa sehemu ya fedha za kigeni ambayo itatunzwa na Benki Kuu. Dunia imebadilika sana. Mataifa makubwa leo hii yanaachana na kutumia zile fedha za kigeni tulizozizoea kama Dola, Sterling Pounds au Euro kama sehemu ya kuwekeza, yamekuwa sasa hivi yananunua dhahabu na kuwekeza kwenye hizo benki na kuwa sehemu ya pesa zao za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili umuhimu wake mkubwa kwa sababu, dhahabu thamani yake mara nyingi inaongezeka kwa haraka zaidi wakati Dola inapungua. Kwa hiyo, ukiangalia huo mtazamo kwa muda mrefu, nilikuwa naangalia takwimu za mwaka 2022 Desemba, ukilinganisha na leo, miezi minne tu, bei ya dhahabu imepanda kwa asilimia 11 ambayo hiyo ni asilimia kubwa sana. Ina maana nchi yetu ingeweza kuwekeza kwenye dhahabu, hiyo thamani kubwa tungeweza kuipata badala ya kuendelea kuwekeza pesa zetu kwenye pesa za wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwekeza pesa za kigeni kwenye benki za wenzetu inawezekana hata wengi hawajui, ni sawa na kuwakopesha. Kwa hiyo, zile thamani ya pesa tulizonazo sisi kule, ina maana tumewakopesa, lakini ukiwa na dhahabu ambayo umeinunua Tanzania hapa hapa na tunazalisha Tanzania hapa hapa, utakuwa umetumia shilingi yetu kununua hiyo dhahabu na ukaibadilisha ikawa pesa ya kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapozungumzia urari wa biashara ambao sasa hivi tuliona kwa kiasi kikubwa ulikuwa hauendi vizuri sana, kwa hiyo, kwa kununua dhahabu, Benki Kuu ikianza huo mpango itawezesha nchi yetu kuwa na urari wa biashara ambao ni mzuri. Labda ni kuchukua tu tahadhari ya kwamba huko nyuma hawakufanya vizuri, kwa hiyo, sasa hivi kinachohitajika, wajifunze kutokana na upungufu uliokuwepo, ili tuweze kurekebisha taratibu zetu tuhakikishe kuwa kile tutakachonunua kitatuletea faida badala ya kutuletea hasara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uzuri wake, sasa hivi kuna mashirika makubwa sana ambayo yanalisimamia hilo. Kwa hiyo, hutanunua dhahabu kama dhahabu, utanunua dhahabu ambayo itaongezwa thamani kufikia mpaka asilimia 99.95 mpaka 99.99 ambayo inasimamiwa na mashirika makubwa kama lile la London Bullion Market Association. Ninashauri kuwa Benki Kuu waanzishe haraka hiyo ili tuepukane na kuweka fedha zetu kwenye Dola ambayo mpaka leo hatuoni kama itaendelea kutuletea faida hasa kulingana na mitikisiko ya kiuchumi na hii mivutano iliyoko hapa duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo tungelitumia vizuri kwa Wizara ya Madini; tumeona bei za mbolea zikipanda kwa haraka mno. Hizi mbolea zinatengenezwa kwa madini ambayo yanapatikana Tanzania. Calcium tunayo, phosphate tunayo, lime tunayo, natural gas tunayo, hatuna sababu ya kuendelea kutegemea mbolea za kutoka nje. Kwa hiyo, tujipange vizuri tuangalie ni namna gani nchi yetu ianze kutumia hizi rasilimali zetu tuweze kupeleka mbolea nje badala ya sisi kuwa waagizaji wa mbolea kutoka nje. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)