Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hotuba ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Utawala Bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo pia nianze kwa kuwapa pole wananchi wangu wa Jimbo la Chalinze na Halmashauri ya Chalinze kwa mafuriko makubwa yaliyowapata. Wajue tu kwamba Mbunge wao niko nao pamoja sana. Nitakwenda weekend hii ili kushirikiana nao pale panapoonekana Mbunge natakiwa nifanye kazi yangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba hii ni nzuri na imejikita katika mambo mazuri. Mimi sina wasiwasi sana na Waheshimiwa hawa wawili katika utekelezaji wa majukumu yao. Hata hivyo, yapo maeneo ambayo yanahitaji tuzungumze ili kuweka nguvu lakini pia kuendelea kukumbushana katika mambo ya msingi ambayo nafikiri kwamba wangeweza kuyasimamia basi mambo ya Chalinze na Tanzania yangekwenda vizuri zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na jambo la usimamizi wa maendeleo ya miji na halmashauri zetu. Pamoja na mambo mazuri ambayo yameainishwa lakini jambo la kupanga miji ili iweze kufanana na sura ambayo kila mtu angeitaraji iwepo ni jambo la msingi sana. Kwa mfano, nimeona katika maelezo ya mipango ya kibajeti kwamba ziko Halmashauri ambazo zimeshapanga maendeleo yao na Serikali imepanga kupeleka fedha. Nataka nikumbushe kwamba katika bajeti iliyopita Halmashauri ya Chalinze ilikuwa imetengewa fedha kwa ajili ya kupanga mji wake. Kwa bahati mbaya zile fedha zilipokuja zilitumika katika kipande kidogo sana cha kufanya tathmini ya maeneo ya watu lakini pia uanzishaji wa uchoraji wa ramani ya Mji wa Chalinze. Mpaka leo fedha zile zimeshindwa kukamilika hivyo Mji wa Chalinze bado unahitaji fedha ili tuweze kuupanga vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo pia nataka niikumbushe Ofisi ya Mheshimiwa Waziri, TAMISEMI kwamba Halmashauri ya Chalinze ni mpya, imeanza mwaka jana. Tunawashukuru kwa mambo mazuri waliyokwishatufanyia na ofisi nzuri tulinayo lakini ipo ahadi ya Serikali ya kujenga Ofisi za Halmashauri ya Chalinze katika Makao Makuu ya Halmashauri hiyo ambayo ni Mji wa Chalinze. Mpaka leo navyozungumza fedha zile zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya matumizi hayo ili tuweze kujenga makao makuu yetu bado hazijapatikana. Kwa hiyo, ningemuomba Mheshimiwa Waziri anapokuja hapa kufanya majumuisho au kutoa majibu au tafsiri ya mambo ambayo wameeleza Wabunge hawa basi hili jambo la Chalinze nalo liwe ni moja ya jambo ambalo akiliweka vizuri tutamshukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri amezungumzia kwamba upo Mfuko wa Barabara Vijiji. Chalinze kwa sura yake ilivyo ina Mamlaka ya Mji ambayo ni Chalinze na Ubena lakini pia mahitaji yetu makubwa sana au eneo kubwa sana la Halmashauri ya Chalinze bado ni vijiji. Kwa hiyo, napoona katika mpango huu ambao umepangwa kutekelezeka katika bajeti ya mwaka huu zimewekwa shilingi milioni tisa tu kwa ajili ya Mfuko wa Barabara, Wilaya ya Chalinze, binafsi naona fedha hizi ni ndogo sana haziwezi kufanya ile kazi ambayo Serikali hii inataka kuisimamia. Kubwa zaidi lazima wajue kwamba Mbunge mimi ni Mbunge nayependa kutembea, napenda sana kwenda vijijini na huko ili paweze kufikika barabara lazima zikae vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia limezungumzwa jambo la afya, niwashukuru sana kwa mipango yao mizuri ambayo wamekwishaionesha lakini pia nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa fungu kubwa sana la afya maana tunajua kwamba pasipokuwa na afya mambo hayaendi. Pamoja na hayo liko tatizo kubwa limeibuka Chalinze nafikiri la wiki hii, jambo hili nafikiri nilitolee taarifa kwamba kumetokea tatizo kubwa sana la upungufu wa chanjo ya surua. Wananchi wangu wa Jimbo la Chalinze wamekwenda kwenye vituo vya afya, wamekwenda kwenye maeneo mbalimbali kwenda kutafuta chanjo hizo lakini walipokwenda hapakuwepo na chanjo hiyo. Kwa hiyo, ni vyema Wizara kama Wizara mama TAMISEMI au Wizara ya Afya ikalitolea taarifa jambo hili ili wananchi wa Chalinze wajue kwamba Serikali yao inaendelea kujali na mambo ya afya ni moja ya vipaumbele vyao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa nishukuru sana Serikali ya CCM kwa kutupatia Hospitali ya Wilaya ya Chalinze. Hospitali hii zamani ilikuwa ni kituo cha afya pale Msoga na sasa ndiyo Hospitali yetu ya Wilaya. Kila panapokuja mazuri basi makubwa nayo hujitokeza. Hospitali ile inahitaji mabadiliko makubwa katika miundombinu ile ya kituo kile cha afya. Kwa hiyo, fedha kwa ajili ya upanuzi wa hospitali yetu ya Msoga nayo ni moja ya kitu cha msingi sana kutiliwa maanani. Ninaposimama hapa ningeomba Mheshimiwa Waziri anapokuja kuzungumza basi atuambie katika lile fungu aliloweka katika afya, je, fedha hizo zilizowekwa ni pamoja na upanuzi wa hospitali hiyo?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kipekee kabisa nimshukuru sana kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla na dada yangu Mheshimiwa Ummy kwa kazi nzuri waliyoifanya pale Tumbi maana ilikuwa ni kilio kikubwa kwa watu wanaosafiri na barabara ile. Likitokea tatizo hata mtu kwa mfano akifariki mortuary hakuna Tumbi, akina mama wakipata matatizo ni shida na ndiyo hospitali tulikuwa tuinategemea kwa ajili ya rufaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii napozungumza hapa kazi nzuri imekwishafanyika, mortuary ile iko vizuri na wodi nzuri imekwishakamilika. Kwa hiyo, ni mambo mazuri yamefanyika na tunaendelea kuwashukuru sana viongozi wetu hawa tuliowachagua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hilo katika hotuba ya Wizara imezungumzia juu ya mradi wa maji vijijini na fedha ambazo zimekwishatengwa. Napenda tu nitoe taarifa kwamba mradi wa maji wa Chalinze umekuwa ni mradi ambao kila siku hauishi kuharibika katika miundombinu yake. Pia mahitaji ya kufikisha maji katika vijiji vyetu nalo limekuwa ni jambo moja la msingi ambalo siku zote mimi kama Mbunge wa Chama cha Mapinduzi nimekuwa nalisimamia. Naomba sana tunapotenga fedha kwa ajili ya miradi ya maji vijijini basi Mheshimiwa Waziri ni vyema ukaliangalia hili nalo ili tuweze kuona watu wa Chalinze wanaendelea kupata mambo mazuri zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona katika randama yenu ya bajeti kwamba mmepanga kutumia shilingi milioni 10 kwa ajili ya miradi ya maji ya vijiji vya Chalinze, fedha hizi ni ndogo sana. Chalinze ni moja ya Majimbo makubwa sana katika Tanzania yetu na vijiji vingi sana vinahitaji maji hayo. Kwa hiyo, unapotenga fedha shilingi milioni 10 kwangu mimi hizi naziona ni fedha ambazo zitatosha kwa ajili ya uendeshaji tu na siyo mradi mzima tunaoutarajia.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo Serikali imeendelea kusaidia kuweka fedha katika miradi kama ya TASAF na MKURABITA, ni jambo la msingi sana. Hata hivyo, niendelee kuwasisitiza kuendelea kukagua na kutathmini kaya zenye uhitaji wa fedha za TASAF lakini pia kupeleka fedha nyingi kwenye mradi wa MKURABITA ili vijiji vyangu sasa viweze kupimwa na hati zile za kimila ziweze kupatikana ili kuondoa migogoro isiyo ya lazima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa maendeleo ya jamii, wananchi wa Chalinze wameendelea kulilia soko lao. Katika hotuba ya bajeti iliyopita ya Wizara ya Kazi ilizungumzwa hapa kwamba patajengwa soko la kisasa ndani ya Chalinze. Cha ajabu zaidi mpaka leo hii wananchi wangu wanasubiri hawaelewi nini hatima yake. Nakumbuka ilipangwa mipango mizuri hapa pamoja na kushirikiana na mashirika mbalimbali ya kiserikali kwamba wangeliangalia jambo hili lakini mpaka leo hii bado tunaendelea kusisitiza mahitaji hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Chalinze wanapounguliwa nyumba zao gari la kuzima moto halipo. Ile ni Mamlaka ya Mji na imani yangu ni kwamba mkiliangalia hili kwa vizuri basi tunaweza kuepusha vifo visivyo vya lazima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niunge mkono asilimia mia moja hoja za Ofisi zote mbili, lakini msisitizo mkubwa ukiwepo kwamba watupe jicho la karibu sana watu wa Chalinze kwa sababu Halmashauri ni mpya na mahitaji bado yako pale pale. Ahsante sana.