Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia Wizara hii ambayo ni muhimu sana kwa ujenzi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya hususani katika Wizara hii. Tumeshuhudia hivi karibuni tu kwa suala la madini ya kinywe kule Songwe na mambo mengine mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nimpongeze Waziri Dkt. Dotto Biteko pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Kihuswa. Vilevile Katibu wetu Mkuu Ndugu Kheri pamoja na wote wanaomsaidia na kwa ujmla Wizara yote ya Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza mchango wangu mwingine nisije nikasahau naomba niwaulize Wizara ya Madini, ni lini yule mwekezaji ambaye alisema anataka kuwekeza katika mgodi wa dhahabu kule Mpepo Wilaya ya Nyasa atakamilisha kulipa fidia zake na kuwaacha wananchi wawe huru wakaendelee na maisha yao maeneo mengine, kuliko hii hali ya kusubiri leo kesho, kesho hakuna kinachoendelea, naomba kwa kweli hilo nipate jibu kwa sababu ni suala ambalo linasumbua katika Wilaya yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hivyo nirudi katika masuala ya kitaifa. Rais wetu Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alisema namnukuu “usipokuwa na mjomba jijombeze mwenyewe” sisi Bunge hili hatuna mjomba mwingine wa kutujombeza bali sisi wenyewe, utakuta wadau wengine wanasema Wabunge wanakaa mle wanalala tu hawafanyi nini? Jamani katika Wizara hii kuna kazi kubwa imefanyika. Nakumbuka miaka ya 2009 mpaka 2010 tulivyofikia kutunga sheria ambayo ilikuwa inajaribu kujibu matatizo yaliyokuwa yanawapata wananchi wa Mikoa ambayo inachimba dhahabu hususani Geita, tulipoenda kule Kamati yetu ya Nishati na Madini wakati huo tuliona huruma tulitoka machozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini wananchi ambao maeneo yao zinatolewa dhahabu zinasafirishwa kwa ndege huku na huku watu wanastarehe, lakini watu wake ni maskini sana. Ilikuwa inaumiza yaani ilikuwa haifanani maeneo yanayochimbwa dhahabu na hali halisi lakini leo ukienda Geita, Kahama, Shinyanga maeneo yote ya dhahabu kwa kweli unafurahi, unaona kwamba Wabunge walitimiza wajibu wao wa kutetea nchi hii, kuteteta watu wao katika kipindi chote kuanzia huko mpaka leo hii kupitia taasisi mbalimbali pia zilizokuwa zinatusaidia na leo sasa unaona matokeo ya nini maana ya madini kwa kipato cha mwananchi mmojammoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza sana Wizara kwa usikivu wao ambao waliujenga hatua kwa hatua, kwa sbabu mwanzo walikuwa wabishi ukiwaambia wanakwambia mkataba ni siri, hii haiwezekani, hili halipo lakini sasa hivi tunakaa tunajadiliana na mambo yanafanyiwa kazi yanakwenda vizuri, hiyo ndiyo maana ya Bunge katika kushauri Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo STAMICO pia ilikuwa ni moja ya mashirika ambayo yalikuwa yabinafsishwe, lakini tukasema hapana hebu tuliache tusichulie STAMICO kama ni shirika la faida moja kwa moja, kazi yake inayofanyika inasaidia kujenga uwezo katika nchi kwa kuwajengea uwezo wachimbaji wadogowadogo ambao sasa ni Watanzania na hatimaye watakua, leo STAMICO imekuwa ni kinara inaonyesha mfano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tumeshuhudia STAMICO ikiongoza mapambano ya kuondoa uharibifu wa mazingira kwa kupanda miti, kusema kwamba lazima tupande miti katika maeneo ambayo tunachimba na maeneo mengine, lakini siyo hivyo tu imefikia kuweza kusaini mkataba wa Bilioni 55.2 wa uchorongaji, anaingia mkataba mkubwa na GGM ambayo ni kampuni kubwa ya uchimbaji. Huu ni mfano mzuri wa mashirika yetu kuigwa, kwa kweli nampongeza pia Dkt. Venance kwa kazi kubwa inayofanyika katika shirika hili la STAMICO ikizingatiwa na mimi nilianzia kazi STAMICO. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi kilichopita cha bajeti nilishauri nikasema kwa nini TANESCO au Wizara ya Nishati haipeleki umeme STAMIGOLD kwa uwezo wao ili kuondoa hasara inayopatikana ya matumizi makubwa ya nishati ya diesel kwa kutumia generator wakati wangepata umeme wangepunguza hayo matumizi, leo nimefurahi kusikia kwamba Mheshimiwa Waziri anatuambia jana umeme umewashwa, hayo ndiyo tunayoyapenda mashirikiano kati ya Wizara na Wizara, tena nawapongeza sana Wizara ya Nishati lakini nawapongeza ninyi wenyewe STAMICO chini ya Wizara yetu ya Madini kufuatilia na kuhakikisha kwamba mnaondoa hasara hizo kama ambavyo mlishauriwa na Waheshimiwa Wabunge .

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, naomba nizungumzie kidogo juu ya suala la wadau tunaowahamasisha kuanzisha viwanda mbalimbali kwa ajili ya kuongeza thamani ya madini yetu. Mara ya mwisho wakati tumeenda Geita kama Balozi wa Wachimbaji Wanawake, tuliamua kumtembelea mwanakiwanda mmoja, Ndugu Sara kwenye Kiwanda cha GGR. Baada ya kufika pale, kitu ambacho tulikiona, hatupata picha nzuri sana. Yule mama tuliposema tunamsalimia ili tujifunze anachokifanya, alituambia kwamba jamani msinione hivi, mwenzenu saa hizi nipo kwenye tension kubwa sana. Nini? Watu wa TRA na watu wa Tume ya Madini wameenda kumkagua, lakini jinsi ambavyo wanamsemesha, hawataki hata kumsikiliza vizuri. Yaani ni ile hali ya kama Polisi hivi sijui, na Polisi wenyewe sio wa siku hizi, wale wa zamani ambao walikuwa hawafuati ustaarabu. Eeh, nini? Hapana sijui nini! Kila wakati anafikiriwa kwamba mwanakiwanda ni mwizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuiache hiyo tabia. Sisi wenyewe kama hatuwezi kuwekeza, tunawaita private sector wasaidie kuwekeza, kwa nini hatuwajali? Kwa nini hatutumii lugha ambazo ni sahihi? Sikupenda suala lile, sikuipenda kabisa, na ndiyo maana tumesema lazima tuseme. Wale watu wamewekeza kiwanda kikubwa cha kisasa kabisa, lazima tuwajali, tuwaheshimu. Wawekezaji wote lazima tuwaheshimu, tuwasaidie, tuhakikishe wanapata dhahabu kwa ajili ya kusafisha kama ambavyo viwanda vyao vilianzishwa, lakini tukiendelea na mtindo huu wa kufikiria tu kwamba mimi naenda kukusanya mapato. Akifunga, utakusanya wapi hayo mapato? Utakusanya wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii hatuwezi kukubali. Tunawaambia, Bunge hili msituone sisi sijui tumekuwa wapole, hatuna upole wa kuharibu rasilimali au kazi ambazo tunajua zitaleta manufaa makubwa kwa nchi yetu. Kwa hiyo, tunaomba sana, wale ambao bado wanaendelea kuona kuwa na vile viukiritimba vya kizamani, waache. Sasa hivi wameona mfano mzuri, Mama mwenyewe, Mama yetu, Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, anavyosema namna gani tuwashughulikie wafanyabiashara; namna gani tuheshimu wawekezaji; kwa hiyo, ni lazima tuwe na tabia hizo za kuwaheshimu wawekezaji. Tutamfuatilia, mkiendelea kumfanyia fujo, tutawataja humu humu mmoja baada ya mmoja, hadharani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine naomba GST waongezewe kiasi cha fedha za utafiti. Hawa wachimbaji wadogo wadogo pekee yao hawawezi kuwekeza huko. Kama kweli tuna nia kama ambayo tumeanza nayo ya kuwasaidia, basi tufanye hivyo. Serikali ndio inayoweza kuwekeza fedha yake kwa kuchukua risk iliyopo na kujua kwamba baadaye huyu mchimbaji ataweza kunufaika yeye mwenyewe na pia kuisaidia nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana, GST isijikite katika baadhi ya maeneo tu. Tumegundua kwamba hayo madini yapo katika maeneo mbalimbali, ila haijajulikana. Kule Mbinga na Nyasa, tulikuwa hatujui kama makaa yangetusaidia kiasi hiki. Leo sasa hivi makaa ya mawe yamekuwa ndiyo chanzo kikuu cha fedha katika Mkoa wetu wa Ruvuma, lakini zamani tulikuwa tunaona ni ardhi tu tunaikanyaga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika, watu wamekuwa wanasema makaa ya mawe hayafai, ni nishati mbaya, tunakubali, lakini inakuwa ni nishati mbaya tu pale ambapo tunahitaji kutumia sisi kwa mambo mengine! Sasa hivi kunahitajika makaa ya mawe huko duniani, mbona sasa hatusikii, wanachukua kwa nguvu zote! Tumegundua kwamba kumbe tunakataa jambo pale tunapoona hatulihitaji sisi, lakini pale ambapo wao wanalihitaji, linakua ni suala la dharura, ni changamoto imetokea, basi leteni tu. Kwa hiyo, nasema kwamba tusiwe na mchezo huo wa kudanganyana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nitoe wito na rai kwa madini mapya ambayo tunaanza kuyachimba, haya wanayaita rare minerals, au critical rare minerals; naomba sana, tusije tukaingia tena kwenye mtego ule ule ambao tulianza nao wakati tunaanza kuchimba dhahabu. Kwa sababu hayo hatujui tabia yake, hatujui gharama zake. Kwa hiyo, tusipofanya utafiti wa kutosha tutajikuta tunaingia mikataba ambayo leo tunafurahi tunasema kwamba mikataba hii ina faida kumbe ni hasara tu. Kwa hiyo, tuwe makini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)