Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na nianze kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuonesha dhamira kubwa ya kukuza Sekta hii ya Madini hapa nchini. Vile vile namshukuru kwani alipokuja Njombe nilimwomba amtume Mheshimiwa Waziri wa Madini aje Ludewa aweze kuzungumza na Wachimbaji wadogo juu ya kuwagawia vitalu vya makaa ya mawe. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii pia kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Dkt. Doto Biteko na Naibu wake, kwani Naibu Waziri aliweza kufika Ludewa, nimshukuru sana. Vikao vile vimezaa matokeo mazuri. Kwa hiyo, naipongeza sana Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nashukuru sana kwa Mheshimiwa Dkt. Doto Biteko kuikuza Wizari hii ya Nishati na Madini, kwa sababu namba zinamtetea. Tumeona sasa Sekta ya Madini inatoa mchango kwa asilimia 9.7 kwenye pato la Taifa. Jitihada ambazo amezifanya siyo ndogo, kwa hiyo, anastahili pongezi sana. Kwa hiyo, tunamtia moyo kwamba aendelee kuhakikisha kwamba sekta hii inaongeza zaidi pato la Taifa. Kwa sababu tukiangalia Sekta ya Kilimo ina asilimia 26, Sekta ya Utalii ina asilimia 17. Kwa hiyo, nikiangalia madini tuliyonayo, na mwendo huu ambao Mheshimiwa Dkt. Biteko anao, naamini atasogea na sekta hii itakuwa na mchango mkubwa zaidi kwenye pato la Taifa, na vile vile kuzalisha ajira kwa wananchi. Ndiyo maana Wabunge wengi hapa wamechangia na kuona kwamba kuna haja sasa ya Serikali kuangalia sana wachimbaji wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze pia Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya na wananchi wote wa Ludewa kwa mapokezi mazuri ya Mwenge wa Uhuru. Nilikwenda huko, hamasa iliyokuwa mwaka huu siyo ya mfano. Kwa hiyo, nawapongeza sana wananchi na ninawashukuru. Naomba tunapowahamasisha awamu nyingine, wafanye kama mwaka huu. Kila mmoja aone jambo ni la kwake kama ilivyokuwa mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ziara ile ya Mwenge, tulipita Kijiji cha Mkomang’ombe, wananchi walikuwa wanalalamikia sana zile fidia zao za Mchuchuma na Liganga. Naishukuru sana Serikali, mnatambua kwamba exchequer ilishatoka ya Shilingi bilioni zote 15, lakini nilipofuatilia NDC kwa nini hawaendi kulipa fidia? Ilionekana hawajapewa fedha zile za kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nitumie fursa hii kumwomba sana Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha, namwona hapo, atusaidie wananchi waweze kupewa zile fedha, kwani wamezisubiri kwa muda mrefu sana. Kimsingi wananchi wale kwa Mkomang’ombe, Iwela, Kitongoji cha Malamba, wananchi wa Idusi, wanasubiri fedha hizi kwa hamu kubwa sana. Wananchi wale wa Kijiji cha Amani, wananipigia simu kila siku. Kwa hiyo, naomba kwa sababu Mheshimiwa Rais ameshaidhinisha hizi fedha, wale NDC wapewe zile fedha za kufanyia kazi ili waende mara moja tukamalize mgogoro na wananchi wa Liganga na Mchuchuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile naomba sana, kuna hoja hii ya wachimbaji wadogo. Nilikuwa nasoma ukurasa wa saba kwenye ule Mpango aliowasilisha Mheshimiwa Waziri wa Fedha, nikaona watu wa GST wamenunuliwa vifaa, mitambo kwa ajili ya kufanyia utafiti. Pia Mheshimiwa Waziri kwenye bajeti yake ule nadhani ni ukurasa wa 84 ameonesha kwamba hawa GST kwa mwaka huu wa fedha watakwenda kufanya utafiti wa madini Mkoa wa Njombe. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, naishukuru sana Serikali, kwani Wilaya ile ina madini mengi na hakuna tafiti ambazo zimefanyika ukiacha zile zilizofanywa na Wawekezaji wa Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kule Lupanga, kuna chuma unakiona kabisa na unajua ule mkondo wa madini umefika mpaka kule; maeneo ya Utilili, unakwenda mpaka Makete kule kwa Mheshimiwa Festo Sanga. Kwa hiyo, wakienda kufanya utafiti, tunaweza tukajua potential ambayo nchi hii tunayo, na tunaweza tukaweka mipango kwa ajili ya kuendeleza. Vile vile wananchi kule wanachimba dhahabu, ruby, sapphire na madini mbalimbali, hadi hizo earth minerals pale Mawengi zipo, lakini hakuna tafiti ambazo zimeweza kufanyika na kujua tuna madini kiasi gani, na je, yanafaa kwa uwekezaji wa kiwango kipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naipongeza sana Serikali kwa kwenda kufanya utafiti maeneo hayo. Hii itasaidia sana kuongeza ajira kwa wananchi, kwa sababu sasa hivi tuna vijana wengi ambao wamesoma na wengine walipelekwa nje ya nchi kwenda kusomea eneo hili la mafuta na gesi, wengine madini mbalimbali lakini waliporudi nchini hawajaweza kupewa ajira. Baadhi ya wananchi wamekuwa wakitusumbua sisi Wabunge. Kwa hiyo, tunavyokuza Sekta hii ya Madini hasa wachimbaji wadogo, tunazalisha ajira nyingi zaidi, licha ya kuwa tunaongeza pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kulizungumzia ni kwamba kule Ludewa wale wanaochimba makaa ya mawe, Serikali; namwona Mheshimiwa Jafo yupo, tuangalie sasa mpango wa kusimamia mazingira. Kwa sababu makaa ya mawe wote tunatambua kwamba yana sumu. Kwa hiyo, yanaweza kuleta hatari ya maji yake kwenda kwenye mito na mfumo mzima wa maji, hata haya maji ya chini ya ardhi. Tuweze kuwalinda wananchi kwa kushirikiana na wale watu wa OSHA na watu wengine kwa sababu unaweza kupita sehemu nyingine unakuta wananchi wanachambua makaa ya mawe kwa mikono. Hii ni hatari sana. Kwa hiyo, tuweke mpango mzuri wa kusimamia mazingira, kuangalia mfumo mzima wa maji ili kuweza kuwalinda wananchi wasiweze kupata maradhi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile hata kutoa elimu kwa wachimbaji wadogo; twende tukatoe elimu ili waweze kuujua vizuri huu mnyororo mzima wa thamani kwenye Sekta ya Madini. Waweze kujua, wawe na taarifa, tuanzishe information centers, waweze kupata taarifa ni namna gani wanaweza wakapata mitaji. Nina mfano mmoja wa mchimbaji yuko Kijiji cha Amani pale Ludewa, anaitwa Berege. Amehangaika, amemtafuta geologist, kamwandikia mradi mkubwa. Sasa anahangaika ili aweze kupata mtaji. Kwa hiyo, naomba Wizara hii iweze kuwaita hawa wachimbaji wadogo, iwape taarifa, wafanye nini ili waweze kupata hiyo mitaji kwa ajili ya uchimbaji? Kwa sababu wataajiri Watanzania wengine na fedha hii pia wanaiwekeza hapa hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, napenda sana kuishauri Serikali kama ambavyo Wabunge wengi wameshauri. Bajeti ambayo wanatengewa Wizara ya Madini hasa watu wa GST ni ndogo sana. Hakuna nchi ambayo imeendelea bila tafiti hapa duniani. Kwa hiyo, ilikuwa ni vyema sana, hata kama ni kurekebisha sheria, weka pale sharti kwamba haya mapato yanayotokana na Sekta hii ya Madini; tunaweza tukasema, Bunge likapitisha sheria asilimia tatu hadi tano ziende kwenye utafiti zaidi wa madini, kwa sababu hii itatusaidia kufanya Sekta hii ya Madini iweze kutimiza malengo ya kuongeza pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, bila kuwepo kwa sheria ambayo itatubana, itatulazimisha kuongeza fedha kwenye eneo la utafiti wa kisayansi wa madini, nina hofu kama safari yetu inaweza ikawa na changamoto nyingi. Kwa sababu nchi hii ina mambo mengi, na fedha inahitajika maeneo mengi. Kwa hiyo, kama hamna sheria ambayo inatubana, inaibana Serikali kutenga fedha kwa ajili ya utafiti wa kisayansi, tunaweza tukakutana na changamoto kidogo. Kwa hiyo, nitoe wito kwa Mheshimiwa Waziri atuletee hiyo na Mwanasheria Mkuu wa Serikali waangalie eneo hilo. Kuwepo sheria kabisa ambayo inatubana. Hizi tafiti zitatusaidia sana kuweza kuongeza mapato na ajira kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kulizungumzia, linahusiana na eneo la madini ya dhahabu. Kule kwetu Ludewa kuna wananchi ambao wanachimba hizi alluvial gold, na vile vile zile za kwenye miamba. Hoja hii ya utafiti, ndiyo maana nairudia zaidi, ni vizuri wananchi wale wanaweza, na Mheshimiwa Waziri hata siku moja ukipata nafasi, nikakukusanyia wale wananchi, wakakutana na wewe ukawasikiliza changamoto zao, itapendeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto mojawapo nashindwa kuisema sana kwako kwa sababu inagusa pia Wizara ya Viwanda na Biashara. Wale watu wa NDC, vile vitalu walivyovigawa vya makaa ya mawe, wangeweka na mpango mahususi kwa ajili ya wale wachimbaji wadogo, kwa sababu Mheshimiwa Waziri wanakunukuu kabisa, kwamba ulikwenda kwa maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na waliomba vitalu kwa ajili ya migodi yao ya shaba ambayo imechanganyika na dhahabu. Kwa hiyo, ukiwasikiliza, utaona namna ya kuweza kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nasema hivyo kwa sababu masharti yale yanayowekwa na NDC…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Kamonga.

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)