Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi nami niweze kuchangia Wizara hii muhimu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri na wataalam katika Wizara hii. Nampongeza Mheshimiwa Waziri kipekee kabisa na Naibu wake, watu hawa ni wasikivu sana. Mwaka 2022 nilipata malalamiko jimboni kwangu. Nilipoenda kuwaona, walinisikiliza vizuri na baadaye wakapanga safari. Kwanza nilienda na Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini baadaye akaja mwenyewe Waziri. Kwa kweli tulifanya Mkutano mkubwa sana sana wa Wadau wa Makaa ya Mawe. Kwa hiyo, kwa namna ya pekee nampongeza Waziri na Naibu wake, wanaitendea haki sana Wizara hii wanayoiongoza. Hongereni sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika kikao kile ambacho Waziri alikuja kwa wito wangu, kulikuwa na mambo mengi yamezungumzwa. Kwanza, tulizungumzia suala la CSR; na pili, tulizungumzia suala la local content. Mheshimiwa Waziri kwenye mkutano ule alitoa maelekezo mazuri sana, kwamba lazima madini haya yawanufaishe maeneo yanamochimbwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni sisi tumeanza uchimbaji huu wa makaa ya mawe. Nawapongeza sana wenzetu wa dhahabu, wameanza muda mrefu, na sasa hivi angalau manufaa kwenye maeneo yale yanaonekana wazi wazi, lakini maeneo yetu, bado wananchi walikuwa na manung’uniko na masononeko kwamba tunaona tu magari makubwa makubwa yanapita katika maeneo haya, lakini hamna kitu tunachokiona sisi hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika tunaona Serikali sasa na Mkoa wetu wa Ruvuma kipato kimeongezeka sana sana. Tunaishukuru sana Serikali. Ila pale yanapochimbwa madini, bado wananchi wale hawajaridhishwa kabisa na namna ile inayobaki pale. Kwa hiyo, mwaka 2022 Mheshimiwa Waziri alitoa maelekezo pale na nadhani mliongelea suala kwamba mnatengeneza kanuni. Sasa pengine ni wakati muafaka Mheshimiwa Waziri ukasema ni hatua gani imefikiwa ya kanuni ile ili sasa na sisi wa makaa ya mawe tuanze kunufaika sawa na wenzetu wa dhahabu kama walivyonuifaika ikiwepo pia na lile suala la local content. Ni masuala muhimu sana katika uchimbaji wa haya madini, hususan madini ya makaa ya mawe. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri najua unafahamu hiki kikao na maelekezo uliyotoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine Mheshimiwa Waziri alilozungumzia pale ni suala la leseni. Katika maeneo haya, ziko leseni zilizokwisha muda wake. Wapo wamiliki wamekaa na leseni hizi lakini hawafanyi kazi na muda wake umekwishwa. Kwa hiyo, kupitia kikao kile, Mheshimiwa Waziri alitoa maelekezo kwa wachimbaji wadogo. Nina orodha ya wachimbaji wadogo wadogo wanaendelea kufuatilia utekelezaji wa yale maelekezo yako. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, basi kama ziko hizo leseni, tuwatangazie wale wachimbaji wadogo wadogo nao wapate maeneo waweze kuchimba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina uhakika, kwa uwezo pamoja na Naibu wako na Wizara kwa ujumla, mtalifanyia kazi hili haraka ili wananchi wale wa Mkoa wa Ruvuma nao wanufaike na rasilimali iliyopo katika mkoa wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ninalotaka kuliongea ni la Kitaifa zaidi, ni suala la uchimbaji wa madini haya ya chuma (metallic minerals). Nchi yetu imebarikiwa sana na madini haya. Bahati nzuri yapo, na bahati nzuri yanatumika sana ndani ya nchi hii. Madini haya ndiyo yanayoenda kwenye viwanda hivi vya cement. Kwa wale ambao hawajui, utaona kama mawe hivi yamekaa humo barabarani, hayo ndiyo madini yanayoitwa metallic minerals, na kazi yake kubwa ni kwenda kutengeneza clinker kwenye viwanda hivi vya ciment.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wako wachimbaji waliokuwa wanaendelea kufanya hii kazi, lakini wanakatishwa tamaa na tozo zetu. Wanaochimba hii metallic minerals tumewawekea loyalty ya 6% pamoja na ushuru wa inspection wa 1%. Ukijumlisha wachimbaji hawa kwa jumla wanatoa 7%. Hii inakuwa tofauti na wachimbaji wengine wa madini kama ya gypsum, na madini mengine ya namna hiyo. Wao pamoja na makaa ya mawe, wao wanatoa 3% na inspection yao 1%. Kwa hiyo kule wanakuwa na 4% lakini wale kule wanakuwa na 7%.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiasi hiki ni kikubwa sana, nina ushahidi wa baadhi ya maeneo wachimbaji hawa wameacha uchimbaji, wameona sasa bora tufanye shughuli nyingine kuliko kuchimba na kuendelea kuumia wakati faida inayopatikana humu ni kidogo sana. Nikuombe Mheshimiwa Waziri unalijua hili vizuri sana, lifanyie kazi ikiwezekana basi wote twende kwa, iende flat rate kwa sababu wote hawa wanachimba ni minerals hizi za viwandani, wote hawa wanachimba raw materials za viwandani kwa hiyo kwa vile hawa tumewa-charge kwa 3% basi na wale nao wa metallic minerals basi tuwapige nao kwa 3%. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine hapo hapo kwenye hizi metallic minerals, nchi yetu hii ina viwanda vingi sana vinavyotumia hii metallic materials lakini kinachoonekana sasa hivi hivi karibuni kuna kitu kimefanyika ndani ya nchi yetu. Ninakumbuka sisi miaka mitano iliyopita na hadi sasa hivi tulikuwa tuna-promote viwanda vyetu vya ndani. Sasa kupitia hiki kinachoenda kuendelea sasa hivi kinaenda kuharibu utaratibu huu wa kulinda viwanda vyetu vya ndani na wazalishaji wetu wa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema nini? Viwanda vyetu vinavyotumia hizi metallic minerals zimeingia na mpango wa kutumia copper slug. Copper slug naweza kusema labda kwa lugha ya Kiswahili ni pumba, pumba za copper. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yaani copper ile inachimbwa huko inakochimbwa, inapelekwa huko nje, inaenda inachakatwa huko, yale mabaki mabaki yale yanarudishwa ndani ya nchi wanayatumia tena kwenye viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa vile viwanda vilivyokuwa vinatumia hizi metallic minerals hizi, vinakwepa sasa kununua metallic minerals hizi chuma hizi, haya mawe unayoyaona na wewe unapita hii njia ya kwenda kama unaenda Manyara, kuna mawe yanapatikana kuanzia hapa Maya Maya unaenda mpaka unapita Chemba hivi kuna mawe yanapatikana hapo. Yale mawe ni muhimu sana na ndicho chuma chenyewe kinachotumika watu wa viwanda vya cement wanayatumia haya kwa ajili ya uzalishaji wa cement.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wanakwepa kuyanunua haya, wanakwenda kuchukua hiyo copper slug mbadala wa hii metallic minerals. Athari yake ni nini? Athari yake tunaenda kupoteza hadhi kwa hawa wananchi wetu, tunaenda kupoteza ajira, tunaenda kupoteza mali zetu ambazo tunazichimba humu humu nchini. Hawa wanaenda kuchukua haya na bahati mbaya sana sina uhakika Mheshimiwa Waziri kama tuna uchimbaji mkubwa wa hii copper hapa nchini. Najua copper zinazalishwa nje zaidi kuliko sisi wenyewe na pale jimboni kwangu copper ninayo lakini hatujaanza kuchimba lakini hii inayotumika sasa ni ya wenzetu, tuna wanufaisha wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri kwa nia ile ile ya local content hapa tutakuwa tunaenda nje ya utaratibu wa local content kwa sababu tunajua lazima tuwape kipaumbele watu wetu na tunapowapa kipaumbele watu wetu ndipo tunapozalisha zaidi. Ndipo tunapotumia rasilimali zetu lakini pale tunapotumia hizi kutoka nje maana yake uchumi wote tunaupeleka wapi, nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri sijajua hili limetoka hivi vibali vimetoka kwako? Kwa sababu pale nyuma tulidhibiti hili hivi vibali vilikuwa havitolewi. Sasa aliyetoa hiki kibali kwa kweli sisemi kwamba haitendei lakini siyo sawa sawa. Lazima twende tuvilinde viwanda vyetu. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana naunga mkono hoja lakini nikuombe sana Waziri suala hili ulitolee maelezo na ufafanuzi ili tunufaike ndani ya nchi hapa. Ahsante sana. (Makofi)