Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa heshima siku ya leo tarehe 28 kuweza kufunga dimba la hii Wizara ya Nishati na Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nikushukuru wewe, nimshukuru Mwenyezi Mungu muumba wa ardhi na dunia kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia hii Sekta ya Madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Mjumbe wa Kamati ya Madini, kwanza napenda nimshukuru Waziri Doto Biteko Mbunge wa Bukombe, jirani yangu. Nimshukuru pia msaidizi wake Kiruswa, Naibu Waziri wa Madini pamoja na Katibu aliyeteuliwa hivi juzi wa madini ndugu yangu ambaye jina lake sijalikariri vizuri. Niwape shukrani za dhati ya moyo wangu bila unafiki. Nimshukuru Naibu Katibu wa Sekta hii ya Madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli kabisa shukrani ninazozitoa ni za dhati siyo za kisiasa wala za kifitina. Mmekuwa msaada mkubwa sana kwangu. Mwanzoni tulikuwa hatutembei pamoja. Ilikuwa kata funua kata funua kwa ajili ya kero ambazo zilizokuwa kwenye hii Wizara ya Madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nifahamishe Bunge Tukufu hili kwamba kwanza hii Sekta ya Madini hapo nyuma tulikuwa hatufaidiki nayo sisi kama Wananchi wa Mbogwe. Kulikuwa na makampuni ya nje ambayo yalikuwa yananufaika pekeyake. Mheshimiwa Doto Biteko Awamu ya Tano ulipoteuliwa kuwa Waziri kulikuwa na migodi kwa mfano Nyakafulu likuwa imekaliwa na Kampuni ya RUSROT. Tulikuwa tunaona magari tu yanapishana. Mjie wetu wa Mbogwe Masumbo ulikuwa haujengwi. Mlipowatimua hao mabeberu wananchi wakaingia kuchimba na sasa hivi wilaya ina changamka kwa speed kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimshukuru Rais wa Awamu ya Sita Mama yangu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada zake anazozionyesha kwa wananchi wote wa hapa Tanzania. Lakini pia napenda niwape pole wachimbaji wenzangu ambao wanahangaika na mihangaiko ya hapa na pale kuchimba kwa nguvu zao wenyewe bila kuwezeshwa hata na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda basi leo nijikite kuishauri hii Sekta ya Madini kwa mambo machache ambayo Mwenyezi Mungu atanijalia kuweza kuyataja. Kwanza ifahamike kwamba ninaposema Mkoa wa kimadini Mbogwe nazungumzia wilaya tatu, ambapo Wilaya ya Bukombe imo, ambapo anapotokea Waziri mwenyewe. Nazungumzia Nyang’hwale ni wilaya ambayo tunaungana kwa pamoja kufanya Mkoa wa kimadini Mbogwe. Naomba niishauri Sekta ya Madini hakuna kosa tunalolifanya kama kuandaa hizi bajeti na kutokuweka vipaumbele vya hii mikoa inayotuzalishia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia katika uzalishaji hapa kwenye Kapu Kuu tumeingiza zaidi ya shilingi bilioni 21 ndani ya mwaka mmoja lakini cha ajabu wale wakusanyaji wanaosimamia hizi shughuli hawana ofisi nzuri. Kwa hiyo, niiombe Sekta ya Madini itenge eneo na iweze kuwajengea watumishi wa madini wanaousimamia huu Mkoa wa kimadini Mbogwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimpongeze RMO uliyenipa Mheshimiwa Waziri ni RMO ambaye sasa hivi kausingizi sasa kana tulia maana tukero kila kakitokea kakero kwa wachimbaji nampigia simu sehemu fulani kuna mgogoro, anaenda. Ananisikiliza pamoja na wasaidizi wake nampongeza sana wajina langu ambaye anaitwa na yeye Maganga kama mimi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ndugu zanguni huwa siyo mwanasiasa mzuri yaani huwa ninaumia sana pale unapomuona mtu anasimama kuzungumza uongo sehemu yoyote ile. Wamezungumza wenzangu kwamba ukiangalia maandiko yanasema tumewawezesha wachimbaji wadogo tumewawezesha lakini kiuhalisia wachimbaji wadogo hawajawezeshwa chochote kile. Hizi shilingi bilioni 21 ninazozizungumzia ambazo zimeuza mauzo zaidi ya shilingi bilioni 200 ni wachimbaji wenye moko ambao wanaingia kwenye mashimo wenyewe. Serikali inaenda kuchukua pato la taifa na kuingiza kwenye Kapu Kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa watu ukiona mazingira wanayoyaishi. Barabara hazipitiki, watoto wao hawana madawati kwenye mashule, huku Mbunge wao wa Jimbo la Mbogwe nazungumzia shilingi bilioni 200 zimeingia kwenye Kapu Kuu bila kuangalia fedha hizi zilikotoka. Ni kwa nini Serikali isitengeneze utaratibu wa kuwalipa ruzuku na kuwalipa posho wachimbaji hawa wadogo ili na wao waone faida ya kuwa na Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hivi naweza nikasema haki vizuri haijakaa vizuri na ninaomba unilindie muda wangu nicheze maana bado muda mzuri sana hata nikipiga dakika 15 hamna shida ili kusudi niweke mchango wangu vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye mabenki unakuta watu wanasimama huko kwenye Wizara ya Fedha wanasema tumewezesha wachimbaji lakini kiukweli wanamaliza viatu hawa wachimbaji kwenda kwenye mabenki na mikopo hawapewi lakini tukiwa kwenye makongamano na sherehe mbalimbali unaweza ukamwona mtaalam ana-introduce hoja akiwa anasema kabisa tumewezesha wachimbaji wadogo, huwa naumia sana. Kwa kweli hilo suala lishindwe na lilegee kwa Jina la Yesu nianomba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri naomba ni- copy na ku-paste mchango wa Mheshimiwa yule wa mzee wangu nanilii, mzee aah! jina nimelisahau yule wa Musoma yule. Mchango wake Getere umekaa vizuri sana. Amezungumza vizuri naomba niunganishe, ni-copy na ku-paste ndiyo maana nimesema hivyo. Mheshimiwa Waziri fuatilia mchango ule na niko pamoja na Getere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natamani wachimbaji waonekane wanathaminiwa kwenye hii Awamu ya Sita. Hatupendi kuona mazingira yale yaliyokuwa yanatupata miaka ya 1995, wachimbaji waki nanilii wakihila tu wawekezaji wanakuja wazungu kuwafukuza wachimbaji wadogo na kuwafanya kanakwamba wao ni wakimbizi hawako kwenye nchi yao. Nakuomba sana Mheshimiwa Waziri usiingie kwenye laana hiyo wewe. Natamani uweke historia hata kama ukiona mambo yamegoma sana yaani kung’atuka nalo ni neno ukiona mambo hayaendi kwamba sasa wachimbaji wanaenda kuanza kukosa haki zao unaachia ngazi rafiki yangu kabisa tunakuja kulima na kujipanga kufanya shughuli zingine huko Bukombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumza hivyo kwa sababu tumeona sasa hivi kuna baadhi ya wawekezaji wakija hapa nchini hawawathamini wachimbaji wadogo wazawa. Wakifika wengine wanafikia polisi. Wanapokuta watu wamehila wanawafukuza kwenye maeneo yao. Hawafuati sheria za kuwalipa fidia wenye maeneo ambao wamekaa nayo maeneo miaka nenda rudi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana kuanzia wewe kama sheria zetu haziko vizuri tuzirekebishe ili kusudi tuwajali watu wetu. Haiwezekani mtu amemiliki ardhi zaidi ya miaka 100, mtu anaingia kwenye mtandao tu akiwa Australia au Marekani anapewa leseni. Anakuta tayari kuna wananchi wanaishi vizuri pale yeye kwa kuwa ana leseni anakuja na mabunduki anakuja kuhamisha wananchi. Wanabaki wananchi wanalia. Sawa natambua kwamba ardhi ni mali ya Serikali lakini lazima kauzalendo tukaweke sasa. Hii ardhi ya Serikali kuna watu ambao wamemiliki zaidi ya miaka 100, unawaachaje? Kwa nini na wao wasiingizwe kama maeneo yao wamemiliki yenye dhahabu wasiingizwe kwenye leseni humo ili kusudi na wao waweze kufaidika na ardhi yao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakujua una uwezo mkubwa kaka yangu. Kabla hata hujawa Mwenyekiti wewe ulikuwa Mwalimu wangu ulikuwa unanifundisha jinsi ya kuishi hapa Bungeni. Kwa hiyo, nikuombe sana kwa power uliyoipata tuweze kuwasaidia wananchi wetu waliotuchagua waweze kunufaika na rasilimali zao ili wawekezaji hawa wanaokuja kwa wingi wawafaidishe wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine hapa Mheshimiwa Waziri napenda nishauri, zipo kero ndogo ndogo ambazo zinaweza zikatuchelewesha zikatufanya hata kutukosesha usingizi tena. Kwa mfano, hizi kodi za matela ya punda, tunasema ni madini ujenzi, nakuomba Waziri hizi kero zingine ndogo ndogo ni kufuta tu ili wenye matoroli ya punda hata Bukombe huko pamoja na Bukombe na Nyang’hwale waweze kufanya shughuli hizi bure. Kwa sababu toka zamani ilikuwa ni bure tu lakini sasa hivi hizi fedha hata kwenye kapu lako huwa haziingii zinabaki halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri uwaonee huruma wananchi wako ambao ni wachimbaji wako uwe tayari kama Bashe ambavyo huwa namwona anapambana na mabeberu yanapokuja kununua mazao na kuwadhulumu wakulima na wewe uwe mkali hivyo ili kusudi wananchi wetu waweze kuishi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala jingine naomba nishauri hata hii Wizara ya Madini. Niombe maeneo yenye migodi yote barabara nyingi hazipitiki na ni maeneo yana uzalishaji kila siku yanatoa pamoja na kwamba sasa hivi hali siyo nzuri sana. Serikali ione sababu ya kwenda kuweka zahanati ili wachimbaji hawa wanapoumia waweze kutibiwa kwenye maeneo ya karibu. Tumeshuhudia watu wanaumia wakiwa wanachimba wakipondwa hata kuvunjika mguu mpaka akafike kwenye kituo cha afya anafika tayari ameshaathirika na kupata maradhi mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe sana Serikali kwa vile inakusanya tozo kwenye haya maeneo iyape kipaumbele yawekewe zahanati pamoja na huduma zingine, barabara ziwe safi lakini pamoja na vijiji vile vinavyozungukwa vinavyoathiriwa na madini, Serikali iweze kutoa mchango mkubwa ili kusudi tuweze kuona faida. Haiwezekani kuna wilaya zingine humu nikiangalia zinachukua mabilioni mengi kwenye Kapu Kuu sisi tunaokusanya vingi tunatoka bila bila na kukaa kwenye maeneo chakavu tunabaki tunatukanwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikuombe sana na kale kaswali kangu ka asubuhi nimeomba uwanja wa ndege. Watu wanahila kule kupanda ndege mpaka aende Mwanza zaidi ya kiometa 360. Mimi hapa nina marafiki wengi tundege tupo tudogo twingi tu hapa twa kuchukua lakini hakuna sehemu ya kutua mpaka ukashuke kwenye migodi tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kupitia hii Sekta ya Madini na Mheshimiwa Waziri kwa vile wewe ni wa kwetu kabisa na neno la Mungu linasema asiye wajali wa nyumbani kwao kubali kupambana huko kwenye vikao vya ndani na Mheshimiwa Rais umuombe na sisi tuwekewe kiwanja cha ndege pale Masumbwi mjini eneo lipo tayari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niseme tunafanya hizi shughuli kwa mujibu wa maelekezo ya Chama kwenye ukurasa wa 105 mpaka ukurasa wa 107 imefafanuliwa hii Sekta ya Madini kwamba tutafanya nini kuanzia mwaka 2020 mpaka 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaomba sana wataalamu wetu pale mnapoandaa hata hizi proposal muendane na mkataba wetu na wananchi kwamba tuliahidi nini kwa wananchi? Tusiende tu yaani kupuyanga tu halafu tuwe kama vile hatujasoma wote humu. Tuwe tunaangalia mkataba wetu na wananchi ni Ilani ya Chama cha Mapinduzi, tumeahidi tutawasaidia wachimbaji, tumeahidi tutawasaidia vifaa vya kuchimbia nashukuru nimeona ma-caterpillar wakati nasoma hotuba Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe kaka yangu, ninao wachimbaji pale Mbogwe nipe nafasi ya upendeleo wapatikane hata mabilionea hata watano pale kutokana na haya ma- excavator yanayomilikiwa na hili Shirika la STAMICO na Mkurugenzi wa STAMICO nina imani unanisikia. Pale Mbogwe kuna kila sababu ya kuweka CAP. Zikiwa zinachimba hizi caterpillar halafu tukawa na kiwanda CAP watu wanazalisha pale maana sasa hivi miundombinu tunayotumia ni ya plant. Tunachenjua huku tunakunywa sumu lakini tukipata CAP tunakuwa tunazalisha kwa haraka na pato litaongezeka zaidi ya 60%. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine GST. Watu wa GST nimeona humu mmeongeza bajeti. Niombe sasa kwenye maeneo yangu hii migodi 88 ambayo wananchi wanachimba wenyewe iende ikafanyiwe research na mtuambie hii migodi dhahabu inapatikana kilometa ngapi kwenda chini ili wananchi hawa wawe na imani wanapokuwa wanapambana wajue kwamba tunazama shimo la urefu wa kilometa ngapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa na cha mwisho kingine niiombe sana Sekta ya Madini. Huwa kuna Kiswahili hawa wanasema kwamba samaki mmoja akioza, wote wameoza. Mheshimiwa Waziri usisite kuchomoa wale wabovu pale wanapoonekana wanakuchanganya, chomoa tupa chini safari iendelee. Hata Yona alitupwa akamezwa na samaki baadaye akaenda kuibukia kwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo hizi bilioni ulizoziomba 89,357 sina kesi na wewe na wala sitashika shilingi. Nikuombe tu Mwenyezi Mungu akutangulie usiingie kwenye historia tena ya makaguzi makuu haya ya nanilii ya mafisadi nakuombea sana kwa Mwenyezi Mungu usije ukaingia huko wewe. Kila utakayemuona wewe uzuri wewe una mdomo ni mwanasiasa halafu ni mwalimu wangu, sema. Yaani najua ukisema mapema hata dunia inakuelewa siyo kitu kinaharibika wewe umenyamaza tu unalinda ustaarabu. Hakuna cha kulindana yaani wewe ukiona mtu anachanganya pasua ili safari iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na Bwana akubariki sana nashukuru sana (Makofi)