Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kunipa nafasi hii na mimi kuwa ni sehemu ya wachangiaji. Niwashukuru Mawaziri ambao wamewasilisha hotuba zao nzuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze mchango wangu kwenye suala zima la elimu. Eneo la elimu kwenye Jimbo la Mpanda Vijijini bado kuna changamoto kubwa sana. Zipo shule ambazo zimejengwa toka enzi za ukoloni, zimechakaa kwa kiwango kikubwa sana, tulikuwa tunahitaji katika bajeti hii Serikali iangalie mazingira ya kuziboresha zile shule ambazo zimechakaa kwa kiwango kikubwa sana.
Katika Tarafa ya Mwese kuna shule ya Lugonesi na Mwese, shule hizi zimejengwa toka kipindi cha wakimbizi wa Rwanda. Kwa hiyo, shule hizi zimechakaa, tulikuwa tunaomba Serikali iangalie jinsi ya kuzijenga upya ili ziweze kutoa huduma nzuri kwa wananchi na watoto wetu waweze kupata elimu iliyo bora. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini zipo shule ambazo zinahitaji kuboreshwa, shule hizo ni za sekondari. Tunazo shule za sekondari kwenye Jimbo la Mpanda Vijijini saba, bado zina uhitaji mkubwa sana wa walimu. Sambamba na kwenye shule za msingi ambako kunahitajika idadi ya kutosha ya walimu ili shule hizo zitoe elimu inayofanana.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo maeneo mengine mapya ya kiutawala, tunalo eneo la Mishamo ambalo raia wapya wamepata uraia. Eneo hili lina changamoto kubwa sana kwani idadi ya watu ni wengi lakini bado tunahitaji huduma za kijamii hasa kwenye suala la elimu. Tunaomba Serikali iangalie kwa kina yale maeneo ambayo yalisahaulika kupata huduma za kimsingi ambazo huko nyuma zilikuwa zinatolewa na UN kwa sasa zinategemewa sana kutolewa na Serikali yetu. Naomba Waziri mwenye dhamana aelekeze nguvu, aende akaone mazingira ambayo vijana wanasoma, shule moja inachukua idadi ya wanafunzi karibu 1,800 na darasa moja unakuta lina wanafunzi zaidi ya watoto 100, tunaomba eneo hilo mliangalie sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni maji. Jimbo langu lina tatizo sana la maji kwenye vijiji vingi. Kipo kijiji cha Kamjelam ambacho kiko eneo la Mishamo, hakuna maji. Tunahitaji eneo hili kwa ujumla kwenye Kata za Bulamata, Mishamo, Ilangu na Ipwaga, wajaribu kufufua visima ambavyo vilikuwa vimechimbwa na UN kipindi hicho cha nyuma. Serikali ione umuhimu sasa wa kuangalia vile visima ili viweze kutoa maji na wananchi waweze kupata huduma.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni barabara za vijijini. Maeneo ya Jimbo la Mpanda Vijijini yana vijiji vingi sana ambavyo havipitiki kwa sababu barabara zake si nzuri. Tulikuwa tunaomba Serikali iweze kuongeza bajeti hasa kwenye Wilaya ya Mpanda ambayo kimsingi ndio imezaa Halmashauri zote ambazo zimezaliwa katika Mkoa wa Katavi.
Kwa hiyo, tunaomba waelekeze nguvu kujenga miundombinu ambako kuna uzalishaji mkubwa sana wa mazao ya mahindi na mpunga, yanayotegemewa kuchukuliwa kutoka vijijini kuyaleta makao makuu ya Wilaya na mkoa na baadaye sehemu ya Mikoa ya Mwanza Shinyanga wanakuja kununua mazao hayo. Sasa ili kuweza kuboresha na wakulima waweze kunufaika, tulikuwa tunaiomba Serikali iboreshe barabara za kijiji cha Kabage kuja barabara kuu inayounganisha kutoka Kagwila - Karema. Iboreshe barabara za kutoka Kalilankurukuru kwenda kijiji cha Kamsanga na iboreshe barabara za kwenda kijiji cha Mnyagala ambako kuna uzalishaji mkubwa wa mazao. Ili wananchi waweze kuzalisha na wapate bei nzuri lazima Serikali iboreshe barabara.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara nyingine ambazo zinahitaji kufanyiwa urekebishwaji kwa kiwango kikubwa ni maeneo ya vijiji vya Mishamo ambako barabara nyingi zimeharibika. Tunaomba Serikali iweze kusaidia iweze kufanya kazi nzuri na iweze kutoa huduma nzuri kwa ajili ya kupita ili wananchi waweze kuzalisha mazao yao na yapate nafasi ya kupelekwa kwenye masoko.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama tutaiachia tu Halmashauri ya Wilaya kwamba ndiyo itaweza kusaidia hizo barabara, itakuwa ni jambo gumu kwa sababu eneo la Wilaya ya Mpanda ni kubwa na ukubwa wa Jimbo umekuwa mkubwa sana tofauti kabisa na maeneo mengine. Jimbo la Mpanda Vijijini ni jimbo ambalo lina uwezo wa kuchukua Mkoa mzima wa Kilimanjaro, ukachukua na sehemu ya Zanzibar, ukiunganisha unapata Jimbo ambalo naliongoza mimi. Lina kilometa za mraba 16,900 kitu ambacho kuwafikia wananchi inakuwa ni taabu. Naomba Serikali iangalie ukubwa wa Jimbo hili ili liweze kugawanywa na wakati mwingine kutoa huduma zinazofanana ili tuweze kuwafikia wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwenye suala la afya. Eneo la afya Mheshimiwa Anna Lupembe amezungumzia sana na mimi nalitilia mkazo wa aina yake kwa sababu eneo hili ni muhimu sana. Kwanza, hatuna vifaa vya kuwafikia wananchi kwa maana vituo vya afya havina ambulance. Halmashauri hii ilipokuwa inatoa mgawanyo kwa Halmashauri zingine, kila Halmashauri iliyokuwa inazaliwa walikuwa wanatoa magari kutoka Halmashauri mama kuyapeleka kwenye maeneo ya Halmashauri zingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Halmashauri Mama kwa maana ya Wilaya ya Mpanda bado haina vitendea kazi kwa maana ya magaari. Ukienda kwenye sekta ya elimu hawana magari, sekta ya afya na vituo vya afya havina magari. Naiomba Serikali iangalie umuhimu wa kununua ambulance kwa ajili ya Halmashauri ya Mpanda ambayo itasaidia kutoa huduma kwenye vituo vya afya vya Mishamo, Mwese na Karema. Idadi ya wananchi walio wengi hasa akina mama wajawazito wanapoteza maisha yao kwa sababu ya umbali wa kufikia huduma ya afya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho tunaomba Serikali iangalie kwenye sekta ya afya, itenge fedha za kutosha kwa ajili ya kujenga Hospitali ya Mkoa wa Katavi. Ni eneo pekee ambalo kiutawala halijakuwa na Hospitali ya Mkoa. Bado wanatumia Hospitali ya Halmashuri ya Wilaya ya Mpanda kama Hospitali ya Wilaya na Mkoa kwa ujumla. Kwa hiyo, tunaomba Serikali iangalie umuhimu wa kuweka mkakati wa kutoa fedha za kutosha ili kujenga Hospitali ya Mkoa itakayotoa huduma kwa wananchi wa Mkoa wa Katavi kwa ujumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, niishukuru Serikali kwa namna nyingine kwa kutupa Wilaya mpya ya Tanganyika. Bado Wilaya hii ya Tanganyika haijapata makao makuu yake. Niiombe Serikali iangalie mazingira ya kuweza kuharakisha mchakato wa kupeleka makao makuu hasa pale yalipokuwa yamelengwa na Waheshimiwa Madiwani walipokuwa wamependekeza. Ni vizuri Serikali itakapokuwa imepeleka huduma hiyo na mchakato wa Halmashauri kwa ujumla ukafanyika mapema utasaidia kupeleka maendeleo kwa haraka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na nashukuru sana.