Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Mwantumu Mzamili Zodo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja, nisije nikasahau maana ya Wizara hii kidogo ni mazito.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanza kuchangia Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi nashindwa nianzie wapi. Changamoto ya ajira ni kubwa sana, na wote tunashuhudia kila Mbunge sasa hivi ana kimemo cha kuombwa ajira na wananchi wake, lakini sasa matarajio yetu kuna baadhi ya Wizara ambazo zingeenda kutatua changamoto hii ya soko la ajira, ikiwemo Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Michezo pamoja na Wizara ya Madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa nasikitika sana sijui kama Wizara hii itaweza kutatua changamoto hii ya soko la ajira. Kwa sababu nikisoma hizi Taarifa za Waziri na Kamati, Wizara hii hata makusanyo yao tu yenyewe hawawezi kukusanya ambayo wenyewe wamekadiria ili wakusanye, hawawezi kukusanya na hawafiki lengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano mwaka 2022/2023 Wizara hii ililenga kukusanya bilioni 80.1 ambayo mifugo ikusanye bilioni 40.1 na uvuvi bilioni 40 lakini mpaka wanafikia mwezi Februari quarter tatu zimepita Wizara ya Mifugo imekusanya bilioni 16.6 na Wizara ya Uvuvi bilioni 13.3 kati ya bilioni 40 sawa na asilimia 33. Tumebakiza robo moja ya mwaka; na kwa makusanyo yote jumla wamekusanya kwa asilimia 37.5.
Kwa muundo huu hawawezi kufikia lengo; na sijui kwa nini hawafikii lengo na makadirio haya wameweka wao wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niko Kamati ya TAMISEMI, kule kuna halmashauri zinakusanya makusanyo yake zinavuka lengo, zinakwenda asilimia 104, 110, yaani wanakusanya mpaka wanavuka lengo. Hata wale ambao hawavuki lengo basi angalau wanakuwa juu ya asilimia 50, lakini kwa Wizara hii sidhani kama watafika hata asilimia 50 mpaka kufika mwezi wa saba; kwa hiyo napata wasiwasi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini makadirio ya bajeti ya kipindi kinachokuja cha mwaka 2023/2024 wameongeza tena bilioni mbili wakisema wataongeza makusanyo. Sasa napata wasiwasi; kama huu mwaka uliopita hata sidhani kama watafika nusu ya makusanyo lakini mwaka huu unaokuja wanasema wataongeza kidogo watakusanya bilioni 82.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ulega lazima waje na mikakati Madhubuti ya kuhakikisha wanaongeza makusanyo, vingenevyo hata mama mwenyewe hataona haja ya kuongeza bajeti kwenye hii Wizara. Kwa sababu hata kile ambacho wanakikadiria, yaani wao wenyewe hawajiwezi, kwa hiyo hataona sababu ya kuwawekeza sehemu ya watu ambao hawajiwezi, anaona akiweka huko fedha itaendelea kupotea. Fedha itakwenda, miradi itatekelezwa lakini hawatakusanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ulega yeye ndiyo umeingia juzi, wao ni wachapakazi, Mheshimiwa Silinde tumefanya wote kazi akiwa TAMISEMI, lakini Mheshimiwa Ulega mtani wangu yeye mwenyewe anajua; tangu mimi nimeingia Bunge hili kati ya Wizara ambazo nazifatilia kwa karibu sana ni Wizara ya Mifugo na Uvuvi na wewe mwenyewe ni shahidi. Kwa hiyo nimuombe, sina wasiwasi na uchapakazi wake, aenende akaweke mikakati pamoja na watendaji wake wa kuhakikisha anaongea makusanyo. Atatupa nguvu sana hata sisi Waheshimwa Wabunge wampiganie ili waendelee kuongezewa bajeti ya Wizara yao. Lakini sasa kama hawawezi kukusanya tutashindwa kupiga kelele wao waongezewe bajeti, kwa sababu hata kile kiasi wanachopewa kitakwenda kupotea. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha aje atueleze mikakati yake hasa ya kuhakikisha anakwenda kufikia lengo la makusanyo kwanza malengo ambayo wao wameyaweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya miradi hii ya maendeleo walipewa bilioni 182 ya miradi ya maendeleo, lakini sasa hizi fedha za maendeleo zinatengwa, ambazo kwa mifugo walipewa bilioni 46.7 na uvuvi bilioni 135; lakini hizi fedha hazipelekwi, yaani ni hela walizotengewa lakini hazipelekwi, kwa hiyo hawawezi kufanya kazi. Kwa mfano kwenye uvuvi kati ya bilioni 135.6 imepelekwa bilioni sita pekee kwa ajili ya miradi ya maendeleo, wakati sisi TAMISEMI mradi mmoja tu wa soko la Nyamagana ni bilioni 20. Kwa hiyo sasa unaweza ukaona hapo, Wizara nzima ni mradi mmoja wa soko kwenye halmashauri moja, ndio wanapewa kama fedha za maendeleo kwa Wizara nzima ya Mifugo na Uvuvi. Mheshimiwa Ulega hawawezi kutoboa, mradi mmoja wa maendeleo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mzamili, muda wako umeisha, malizia.

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, muda umekwisha ahsante sana nashukuru. Kwa hiyo nimuombe Mheshimiwa Waziri; Wizara hii ina migogoro mingi, na kati ya vitu vinavyosababisha migogoro pia ni malisho. Jana nilimsikia alikuja na mkakati wa malisho akasema atazalisha malisho ya kwenda kuuza mpaka nchi za Asia. Nishauri aachane na hii habari ya kuuza nchi za Asia kwanza …

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. MWANTUMU M. ZODO: … tutosheleze malisho ya hapa Tanzania kila mwaka ng’ombe wanakufa na wewe mwenyewe ni shahidi hauwezi kuuza Asia ilhali sisi wenyewe bado hatujajitosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nashukuru naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)