Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Sylivia Francis Sigula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. SYLVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia hotuba hii iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kuniwezesha leo kusimama katika Bunge lako hili Tukufu, pia kwa namna ya pekee sana naomba nimpongeze na nimshukuru Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kututeulia watu makini wanaoijua Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na muda naomba nijielekeze moja kwa moja kuchangia Fungu Namba 64 linalohusu masuala ya uvuvi, kuanzia ukurasa wa 68. Tunafahamu kabisa uvuvi na ufugaji hii ni sekta ya uzalishaji nasi kama vijana tunaamini sana sekta hii ingewekezwa vizuri ingetatua changamoto nyingi za vijana ikiwemo ajira lakini ikiwemo kutufanya vijana tuweze kufanya biashara kutokana na mazao ya uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa sana nimekuwa nikisimama kwenye Bunge hili mara nyingi, nikielezea na nikiomba Serikali itupe ufafanuzi wa namna ambavyo wanawekeza kwenye Ziwa Tanganyika. Majibu yamekuwa ni utafiti, utafiti, utafiti, utafiti unaendelea! Sasa hili ni jambo la aibu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tumebarikiwa Mungu ametujaalia tuna maziwa mengi, tuna Ziwa Tanganyika, tuna Ziwa Nyasa, tuna Ziwa Rukwa, tuna Ziwa Victoria pia tuna Bahari. Ni aibu kuona leo sekta hii ya mifugo na uvuvi inachangia kwa asilimia ndogo sana kwenye Pato la Taifa, ni aibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niseme tu tunawalaumu viongozi, lakini Serikali kwa kiasi kikubwa imefanya mchango wa uvuvi usionekane. Leo tukienda huko kwa Maafisa Uvuvi hali zao ni mbaya sana. Ukiangalia Mkoa wa Kigoma, ukiangalia Mkoa wa Katavi, ukiangalia Mkoa wa Rukwa vitendeakazi, miundombinu bado ni hafifu sana. Bado tunategemea sekta hiyo ya uvuvi izalishe, inazalishaje? Labda kama tunataka miujiza, lakini hatuwezi kuzalisha, hatuwezi kuona tija ya sekta hii kama hatutafanya uwekezaji wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naongea haya kwa sababu leo hii ukiangalia Mkoa wa Kigoma, Wilaya zinazofanya uzalishaji, Wilaya zinazofanya uvuvi ukiwaambia hata vitendeakazi wanafikaje site? Hawana magari, hawana hata pikipiki za kuwafanya wafanye movements za kwenda kufuatilia. Sasa unataka kuniambia kwa mazingira hayo ni namna gani sekta hii italeta tija kwa Taifa letu? Kwa hiyo, kuna haja kubwa sana ya Serikali kuwekeza katika sekta hii ili tuone tija yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nilitamani kulizungumza kwenye sekta ya uvuvi, wamezungumza hapa Wabunge wengi vizuri sana na mimi naungana nao. Sisi watu wa Mkoa wa Kigoma, Mkoa wa Rukwa na Mkoa wa Katavi, uchumi wetu kwa asilimia 90 unategemea Ziwa Tanganyika. Tumekuwa tukiongea hapa tuna masikitiko kwa sababu tunaona Serikali ni kama haitambui umuhimu wa Ziwa Tanganyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani leo hii bado siku Nane, Wawakilishi wa Wananchi hatuna taarifa rasmi kuhusu kufungwa kwa Ziwa! Bado siku Nane! Haiwezekani maamuzi makubwa kama haya, maamuzi ya kuwakosesha ajira watu wetu, ndani ya Mikoa mitatu bila kuwashirikisha wananchi…

MHE. KILUMBE S. NG'ENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sylvia kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kilumbe.

TAARIFA

MHE. KILUMBE S. NG'ENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba, wakati Serikali yetu na Serikali hizo nyingine zimefanya makubaliano katika jambo hilo, ukiingia kwenye internet Bunge la Congo limekataa hoja ya kufunga Ziwa Tanganyika, kwa maana hiyo na leo tuko kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tunazungumza nasi tunakataa. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sylvia taarifa unaipokea? Endelea na mchango wako.

MHE. SYLVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo taarifa ninaipokea kwa mikono miwili. Sisi Wawakilishi wa Wananchi hasa tunaotoka Ukanda wa Ziwa Tanganyika jambo hili hatukubaliani nalo kwa asilimia zote. Tutakubaliana nalo tu endapo Waziri atakapokuja atatuambia njia mbadala ya watu wetu ndani ya miezi mitatu hii wanaishije? Kama kuna vizimba kwa ajili ya watu wetu tutakubaliana nalo. Tunamuomba Waziri uandae majibu mazuri, kwamba ndani ya miezi mitatu hii tunapofunga Ziwa, wavuvi wetu, wafanyabiashara wadogo ambao wanategemea mazao ya samaki na sisi wananchi ambao tunategemea tupate kitoweo, tunaishije ndani ya miezi hii mitatu? Tunaomba tupate alternative ndiyo hapo tutakapounga mkono jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najiuliza hii ni Serikali yetu na ni Serikali sikivu, kama jambo hili ni kwa manufaa wavuvi kwa nini tusiambiwe mapema? Kwa nini msisikilize ushauri wetu? Kwa nini msitake maoni yetu? Kwa hiyo mimi niseme tu, Mheshimiwa Waziri wewe ni Kaka yangu na ninakuheshimu sana na wewe unajua mimi nakuheshimu sana, lakini katika jambo hili la kufunga Ziwa bila kutushirikisha wananchi, hapana hatuko tayari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana jioni tumesikia maagizo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, mwaka jana Tarehe 03 Novemba, Mheshimiwa Waziri Mkuu alizuia suala la herein, ukisoma taarifa ya Wizara utaona Tanzania ni ya pili Afrika kwa kuwa na mifugo mingi, lakini ukifuatilia kwenye suala la uuzaji wa mifugo yetu nje, Tanzania tunazidiwa na nchi ambazo hata haziko kwenye top 10. Hii yote inatokana na sababu mifugo yetu bado haina quality ya Kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuwa kama tuko kisiwani, Waziri Mkuu kaongea vizuri na mimi ningependa niishauri Serikali kwamba changamoto ya hereni ilikuwa ni bei ya hereni, lakini kama Serikali itafanya utaratibu mzuri ambao hautakuwa na changamoto kwa wafugaji, jambo hili lina tija ili kuongeza Pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema, ameongea hapa Mheshimiwa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, watu wa Tanganyika, watu wa Ziwa Tanganyika, watu wa Mkoa wa Kigoma, Rukwa na Katavi tunaomba Serikali ichukulie jambo hili kwa uzito sana, tunaomba Serikali ije na majibu mazuri itueleze ni amna gani tunaenda kumaliza suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)