Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. INNOCENT E. KALOGERES: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami nitumie nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi ya kuchangia katika bajeti ambayo iko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2022 katika Wizara hii nilikamata Shilingi, na niliahidiwa ahadi nyingi tu na Mheshimiwa Waziri aliyetangulia, lakini mdogo wangu Mheshimiwa Ulega, yeye ndiye alikuwa Naibu Waziri katika Wizara hii. Katika yote niliyoahidiwa, ni moja tu ambalo nimelipata. Bahati mbaya sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha hayupo, lakini siku hiyo yeye ndio alikuwa amenipa ushawishi mkubwa sana katika kusema kwamba, shida kubwa ya wafugaji ni malisho, shida kubwa ya wafugaji ni maji. Serikali imenunua mitambo mikubwa, adha hiyo ambayo mwaka ule ilipatikana, kwa mwaka huu haitapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niliambie Bunge lako Tukufu, hadi tunapozungumza leo hii, wakulima na wafugaji bado wana migogoro mikubwa inayotokana na wafugaji katika kutafuta malisho na maji. Napata shaka, niliambiwa mwaka ule nisubiri mpaka mwaka huu. Naomba nitangaze tu, nina dhamira ya kushika shilingi ya Waziri wakati utakapofika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliahidiwa majosho kumi, mpaka dakika hii nimepata majosho manne tu. Niliahidiwa mabwawa mawili, mpaka tunazungumza dakika hii, hakuna hata bwawa moja ambalo limechimbwa. Niliahidiwa visima, hakuna hata kisima kimoja. Vilevile tuliahidiwa kupata madume bora ya nyama kwenye Halmashauri ya Morogoro Vijijini, hakuna kitu kama hicho. Ni kielelezo tosha kwamba Serikali haiwezi kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na ushauri kwa Serikali. Cha kwanza, ninaamini na ninaomba, sisi Wabunge tupambane wote hapa, hasa kwenye sekta ya mifugo; wale Wabunge ambao mikoa yao wanatoka wafugaji, tuone ni jinsi gani tunaishauri na kuishawishi Serikali, katika kipindi ambacho ni cha siku zile tano, Serikali na Kamati ya Bajeti wanakaa, na bahati nzuri Mwenyekiti ambaye leo unaongoza kikao ndio Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti, tuone jinsi gani tunasaidia sekta ya mifugo kuongezewa fedha ili iweze kukabiliana na changamoto za migogoro ya wakulima na wafugaji, na changamoto wanazozipata wafugaji wetu katika kuhamahama ambapo inawaletea hasara kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri, amekuja na hoja ya kusema kwamba anataka kuanzisha mamlaka maalum ambayo itashughulikia matatizo au changamoto za wafugaji na wavuvi. Kwa ushauri wangu, tulikuwa na changamoto kwenye barabara, maji, na umeme. Ushauri wangu Mheshimiwa Waziri, hebu tusiende kwenye mamlaka, twende kwenye wakala. TARURA, imeondoa changamoto za barabara katika nchi yetu, lakini RUWASA imeondoa changamoto za maji, ndiyo maana sasa hivi Waziri wa Maji anatamba. Kwa hiyo, nakuomba na wewe, badala ya kwenda kwenye mamlaka, twende kwenye wakala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na changamoto kubwa za upatikanaji wa umeme katika nchi hii, vijijini hata mijini, lakini kupitia REA, leo kila Mbunge anapata faraja na wananchi wanaona kazi ambayo inafanywa na REA. Kwa hiyo, namwomba tu Mheshimiwa Waziri, kwenye suala la mamlaka, tusiende kwenye mamlaka, twende kwenye wakala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuishauri Serikali yangu, hebu tuangalie, sasa hivi wafugaji wanapata wakati mgumu, na vilevile hata watumiaji wengine wa ardhi. Angalieni uwezekano wa kukutana na Wizara ya Maliasili na Utalii, na Wizara ya Ardhi, twende tukaweke mipaka kwenye maeneo ya hifadhi. Wafugaji na wakulima, hawana GPS. Utajikuta ghafla bin vup, wameingia ng’ombe kwenye hifadhi, wakulima wameingia kwenye hifadhi, wanapata fine kubwa ambazo zinawapa wakati mgumu wafugaji na wakulima wetu. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, hebu tuangalie katika mwaka huu wa fedha, jinsi gani Wizara tatu; Ardhi, Wizara yako ya Mifugo na Uvuvi na Wizara ya Maliasili na Utalii, mwende mkaondoe chagamoto ambazo wanapata wafugaji na wakulima wetu katika maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile namwomba Mheshimiwa Waziri, sijajua katika mwaka huu wa fedha mmetenga kiasi gani cha fedha kwenda kuendelea kutafuta maeneo ya malisho. Nimeona katika bajeti yake amesema kuna maeneo 77 yamepatikana ambapo zimepatikana hekta 994,827, lakini kuna Wilaya 14, Wizara ya Ardhi imetenga maeneo ya ardhi, naomba tuendelee kutenga kuweka fedha, ili tuendelee kutenga maeneo makubwa tuondokane na matatizo ya malisho na maji kwa wafugaji wetu na vilevile watumiaji wengine wa ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania bado ni kubwa. Ninaamini kabisa kwamba, tunaweza kuwa na maeneo mengine kama tulivyofanya pale Handeni, kama Serikali itajipanga vizuri. Katika hili naomba tu, Mheshimiwa Waziri, wewe ndiye mwenye dhamana hii. Waziri wa Maliasili katika kuinusuru Ngorongoro, alishirikisha Ofisi ya Waziri Mkuu, Ofisi ya Ardhi na wewe Waziri wa Mifugo mkaweza kupeleka kule ng’ombe. Sasa nakuomba, bado tuna changamoto, migogoro mikubwa itaendelea kutokea, lakini pamoja na migogoro tunaipeleka nchi kwenda kwenye jangwa. Lazima tuandae maeneo ambayo tutapeleka wafugaji wetu kwenda kufanya shughuli zao za mifugo bila migogoro yoyote kwa wananchi, na wao bila kupata hasara kwenye maeneo yao. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Innocent. Muda wako umeisha. (Makofi)

MHE. INNOCENT E. KALOGERES: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)