Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami nichangie sekta hii muhimu ya mifugo na nianze kwanza kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watumishi wote wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa ushirikiano ambao walikuwa wametupa kwenye Kamati ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo kwa sababu ni Mjumbe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Wabunge wenzangu kusema kwamba sekta ya mifugo na uvuvi ni sekta muhimu ya uzalishaji kwenye nchi yetu. Na wenzangu pia wamesema Waziri anapaswa kuonesha wivu na suala la mifugo kama Mawaziri wengine wanavyofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninalisema hili, mifugo imekuwa ikikamatwa hovyo na wafugaji kutozwa gharama kubwa ambayo wakati mwingine wengine wamefilisiwa. Wengi wamekuwa wakizunguka kwenye corridors za Wizara kwa sababu mifugo wao wametaifishwa, lakini hali ya wafugaji nchi hii ni mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafugaji wamelazimika kuhama sehemu moja kwenda nyingine sababu kubwa ni uhaba wa malisho na maji. Na wanapohama tunawashangaa kwa nini wanahama, lakini nikwambie tu Mheshimiwa Waziri, kwa sisi wafugaji unaporudi nyumbani jioni ng’ombe hawajashiba ni sawasawa na mama ambaye watoto wake wana njaa, wewe hupati usingizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hilo lazima lichukuliwe kwa uzito mpana kwamba suala la malisho kwa mifugo nchi hii ni suala kubwa na lazima tufanye kazi ya ziada. Nimekusikia ukisema kwamba utahakikisha ranchi zote zitatumika kutengeneza malisho kwa mifugo yetu. Lakini sioni kama kuna muujiza utakaotokea Mheshimiwa Waziri, fedha zilizoongezwa kwenye bajeti hii tunayokwenda kuipitisha ni fedha kidogo mno. Hata utekelezaji wa bajeti ya 2023/2024 fedha zilizotolewa ni kidogo mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiiangalia sekta ya Kilimo, Fungu 99, iko kwenye asilimia kama 49 tu. Na ninaomba nitaje vitu vichache ambavyo vimetekelezwa. Vitu hivi hata kama vikitekelezwa kwenye Jimbo la Hanang pekee hakutaleta mabadiliko yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilivyotekelezwa; ujenzi wa Bwawa la Kimambi lita milioni 95; ujenzi wa Bwawa la Matekwe, lita milioni 102 – na bahati nzuri hili bwawa mimi nimelitembelea na Kamati. Ni bwawa dogo ambalo hata kuhudumia kijiji kimoja cha wafugaji hakitoshelezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmekarabati Bwawa pale Mwanga, Itigi lita milioni 54; kisima kirefu kimoja na mabwawa mengine 11. Kwa mwendo huu wa kibajeti na fedha hazitoki zote, kwa hakika kazi inayofanyika ni ndogo sana, haitawasaidia wafugaji wa nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye Wilaya yangu ya Hanang, kwanza nishukuru tumepata mbegu 8,000 za kuhimirisha mifugo yetu ili tuweze kuiboresha; mpaka sasa tumeweza kuchukua tu mbegu 300. Changamoto kubwa ni sehemu ya kutunzia mbegu hizo ili ziwafikie wafugaji, haipo. Vifaa vilivyopo ni vidogo havitoshelezi hata kidogo; lakini kwa sababu hizi zinaenda kwa wafugaji ambao hiyo taaluma hawajaelimishwa vya kutosha, wanachajiwa shilingi 25,000. Elfu ishirini na tano ni sawa sawa na bei ya mbuzi, kwamba hii ni kumpandisha ng’ombe uuze mbuzi. Kwa wafugaji hii ni gharama kubwa na haiwezekani, kwa sababu hawana elimu hiyo. La muhimu kwanza Serikali iwezeshe mifugo yao ihimirishwe bure ili wengine wakajifunze kule, wakijifunza baadae watakuwa tayari kugharamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini upande wa watumishi, tunao watumishi wachache. Wilaya ya Hanang’ yenye kata 33, vijiji 96 tuna watumishi 17 tu na tuna pikipiki mbili tu. Sasa ni namna gani utawafikia wafugaji? Mheshimiwa Waziri lazima achukue hatua ya ziada kuwakaribia wafugaji. Wafugaji wanahangaika sana. Wafugaji wetu wanapaswa kuelimishwa, watu wanaacha ufugaji sasa hivi wengi wanakimbilia kwenye upande wa kilimo, kwa sababu ukienda kwenye kilimo unajua kabisa kwenye hekari moja ukilima unapata magunia mangapi utafaidika kiasi gani, kwenye mifugo hamuwaelezi mambo hayo. Wafugaji wangu wa Gehandu, Mureru na Mulbadaw, wanataka elimu hiyo iwasogelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amekuwa Naibu Waziri muda mrefu kwenye Wizara hiyo hajatembelea Jimbo la Hanang. Hakuna Waziri aliyekuja jimbo la Hanang’ akaongea na wale wafugaji wakapata ile elimu inayotakiwa. Ninaomba eneo hilo muwakaribie wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nigusie kidogo eneo la uvuvi. Sisi tunategemea ziwa Bassotu kwa ajili ya Uvuvi. Ziwa lile limeanza kujaa mchanga, sasa waangalie namna ya kulikarabati. Zaidi ya hapo kuna mwalo pale Mulbadaw tumeomba muda mrefu lile mwalo lifunguliwe wananchi waweze kufanya shughuri za uvuvi. Ninaomba wakati anasimama hapa awaelekeze watu wake ndani ya Wilaya kwa sababu nimeona wakiyumba yumba bila kufanya kazi hiyo. Wananchi wanasubiri wakafanye kazi maandalizi ya awali yameshafanyika, ule mwalo ukafunguliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna bwawa la Gidahababieg, tathmini imefanyika mara nyingi. Ungana na watu wa idara ya maji, watu wa kilimo pale tujenge bwawa ambalo litawasaidia watu kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji lakini litasaidia kwa ajili ya kunyweshea mifugo; na pia pale tunaweza kupata mboga ya samaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona kama muda wangu unaanza kukimbia. Sekta ya mifugo; Jimbo la Hanang ni jimbo la wafugaji, Hanang wanahitaji kusogelewa. Tunaomba tuone miguu yenu ndani ya Jimbo la Hanang’; hakuna chochote cha Wizara ya Mifugo na Uvuvi inafanyika kwenye Jimbo la Hanang’ ili wafugaji wangu wale waone Serikali iko nao na inafanya kazi ya kuwahudumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya ninaunga mkono hoja, ahsante sana.