Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ili na mimi niweze kupata fursa hii ya kuchangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Awali ya yote nianze kwa kuwapongeza sana mawaziri wote wawili, kwa maana ya Mheshimiwa Ulega na Mheshimiwa Naibu Waziri Silinde, ndugu zangu hawa, kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais kuongoza sekta mbili hizi za Mifugo na Uvuvi. Mimi kwa upande wangu, kama mimi, binafsi sina shaka kabisa na Waheshimiwa Mawaziri hawa lakini pili niishukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutekeleza kile ambacho sisi Wabunge tulipitisha katika Bunge lako kama mpango wa maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipitisha ujenzi wa bandari ya uvuvi pale Kilwa Masoko, nitoe tu taarifa kwamba ujenzi wa Bandari ya Uvuvi ambayo mkataba wake ulisainiwa mwaka
jana mwezi wa sita unaendelea kwa kazi kubwa sana pale Kilwa Masoko; pongezi sana kwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Wanakilwa kwa ujumla wao, lakini wana. Kilwa Masoko kwa upekee wanaomba sana itakapofikia hatua yoyote ile ama ya kuweka jiwe la msingi au kuzindua bandari hii Mheshimiwa Waziri tunaomba ushauri mamlaka husika, Mheshimiwa Rais aje afanye kazi hiyo pale wananchi waje wampe pongezi wakiwa live pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na ujenzi wa Bandari ya Uvuvi pale Kilwa Masoko kulikuwa na changamoto ya wapiga kura wangu 54 kutolipwa fidia. Niliwahi kuzungumza katika Mkutano wa Nane wa Bunge hili, lakini pia niliwahi kuzungumza katika Kikao cha Pili cha Mkutano huu wa Kumi na Moja katika Bunge hili. Vilevile tarehe nne mwezi wanne nilizungumza na Mheshimiwa Waziri Ulega ofisini kwake kuhusiana na wananchi 54 ambao bado hawajalipwa fidia; tuliweka sawa mambo pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kutoa shukrani sana kwa Serikali lakini kupitia Wizara ya Uvuvi na kupitia kwa Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana husika, Mheshimiwa Ulega. Ninayo furaha kumjulisha kwamba wananchi wangu 54 wakiwemo Fatma Musa Mjaka, Bibi Mwanawetu Zarafi, Mwanafadhila Sudi pamoja na Bwana Said Bungara a.k. a Bwege tayari wameshalipwa fidia ya bilioni 8.5. Sasa mambo ni mazuri hakuna tena mgogoro kati ya wananchi wangu na Serikali ya Awamu ya Sita. Pongezi sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Bunge hili katika mpango wetu wa maendeleo wa miaka mitano, lakini kwa upekee wake katika bajeti ya Wizara hii mwaka jana tulipitisha kwamba tutajenga masoko ya samaki Kilwa Kivinje pamoja na Kilwa Somanga. Nielezee kwa masikitiko tu kwamba mpaka tunaelekea mwishoni mwa mwaka huu, sasa hivi tuko robo ya nne tumeianza hii hatujapata fedha yoyote kwa ajili ya ujenzi wa masoko ya samaki, Kilwa Kivinje na pale Kilwa Samanga. Nitumie fursa hii kuikumbusha Wizara sisi wana-Kilwa Kivinje na wana-Kilwa Somanga bado tunahitaji masoko haya kutokana na uzalishaji mkubwa wa samaki katika maeneo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti,nielezee mambo ambayo nimeyazungumza kupitia Wizara hii na kupitia hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu mara kadhaa hapa Bungeni kuhusiana na Kanuni za Uvuvi za Mwaka 20202 ambazo zimekuwa kikwazo kwa wavuvi wetu. Niliwahi kuuliza swali la msingi hapa ili kufahamu ni lini Wizara ya Mifugo na Uvuvi itabadilisha kanuni hizi; Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana sasa hivi Mheshimiwa Ulega wakati huo akiwa Naibu Waziri alijibu swali hili kwamba muda si mrefu kanuni hizi zinakwenda kubadilishwa. Kwa masikitiko niseme kwamba kilichofanywa na Wizara ni kubadilisha kanuni za tozo peke yake lakini kanuni za usimamizi wa masuala ya Bahari ambazo ni kikwazo kwa wavuvi wetu bado hazijabadilishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niseme tu kwamba wakati anajibu vile Mheshimiwa Ulega alikuwa ni Naibu Waziri, sasa ni Waziri kamili; nenda kabadilishe kanuni hizi kwa maslahi ya wavuvi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Bunge hili bajeti ya mwaka jana ya Wizara hii tulipitisha hapa kwamba Wizara hii itakwenda kununua boti 320 kwa ajili ya kukopesha wavuvi wetu, lakini taarifa ya hotuba ya Waziri hapa leo anatuambia mpaka sasa hivi boti zilizogawiwa ni 150 tu. Hizi zingine zaidi ya 150 zinasubiri nini kupelekwa kwa wavuvi wetu katika maeneo mbalimbali katika ukanda wetu wa Bahari lakini pia katika ukanda wa maziwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapenda kuona wavuvi wetu wasotee kule Mkuranga kwa Mheshimiwa Ulega wanapata boti hizi. Tunapenda kuona wavuvi wetu wa Mafya kule Bwajuu kwa Mheshimiwa Kipanga wanapata boti hizi, tunapenda kuona wavuvi wetu wa Msanga Mkuu kule Mtwara kwa Mheshimiwa Mtenga wanapata bodi hizi. Tunapenda kuona wavuvi wetu wa maeneo ya Pwani, Kibiti, Tanga, Dar es Salaam na kwenye maziwa yetu wanapata boti hizi; ndio utakaokuwa ukombozi pekee kwa wavuvi wetu kuinua uchumi katika sekta hii ya uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nizungumzie suala la migogoro ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji. Migogoro ya ardhi ya wakulima na wafugaji hili lipo ndani ya Wizara hii. Wizara ya Mifugo na Uvuvi wakiratibu vema na Wizara zingine ikiwemo TAMISEMI, migogoro hii wanaimaliza. Nieleze tu kwamba juhudi kadhaa zimefanyika na Serikali lakini migogoro hii bado ipo. Nitoe tu mfano hapa, mimi katika jimbo langu la Kilwa Kusini bado migogoro hii bado ipo, ukienda Kikole migogoro ipo, ukienda Nanjirinji migogoro ipo, ukienda Kilanjelanje migogoro bado ipo; lakini hata jimbo jirani kwa jirani yangu pale kwa Mheshimiwa Ndulane kule Kilwa Kaskazini ukienda Nginjo, Mitole, Miguruwe, Kandalale bado migogoro ipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti,tatizo ni nini? Wakati utaratibu wa kupeleka mifugo unafanyika katika maeneo yote mikoa ya kusini; utaratibu na makubaliano ulikuwa kwamba Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi ikaweke maandalizi ya kupokea hawa wafugaji, lakini mandalizi hayo hayajafanyika, kulikoni? Nitumie fursa hii kuikumbusha Serikali hebu wakaweke utaratibu wa kupokea hii mifugo ili wafugaji waishi vizuri, malambo yawepo, majosho yawepo na migogoro ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji ikomeshwe na imalizwe kabisa na Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti,baada ya hapo naomba kuunga mkono hoja.