Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji kwenye hotuba ya Waziri. Awali ya yote nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa jitihada kubwa sana ambayo anaifanya pamoja na Naibu wake na Wasaidizi wake kwenye Ofisi, wanafanya kazi nzuri lakini yapo ambayo tunahitaji kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Spika, nianze kwenye eneo la mifugo. Kwenye eneo la mifugo, Serikali ina wajibu wa kuimarisha Ranch ambazo zitasaidia wakulima au wafugaji wadogo wadogo waweze kupeleka mifugo kwenye hizo Ranch na Ranch hizo zitumike kwa ajili ya kuwa kama soko ambalo litakusanya mifugo ya wafugaji wadogo wadogo ili mifugo ikinenepeshwa wao wanaiuza kwenye masoko ya nje. Hili litasaidia sana kukuza sekta hii ya ufugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ufugaji wetu asilimia kubwa wamekuwa wachungaji kwa sababu ya kukosa huduma zile za msingi. Hawana malisho ya kutosha, hawana malambo na majosho. Kwa hiyo, wafugaji wanalazimika kutafuta malisho na kutafuta huduma zile ambazo zinaweza zikasaidia mifugo iweze kuishi. Kwa hiyo, niombe Serikali iimarishe eneo hili ili kuwasaidia hawa wafugaji wetu ambao maisha yao kweli ni ya kuhamahama kwa sababu wanahitaji kupeleka mifugo ili iweze kupata huduma.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine nizungumzie suala la uvuvi. Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia sana hoja au mapendekezo ya Serikali juu ya kufunga Ziwa Tanganyika. Mimi ni miongoni mwa Wabunge ambao wapigakura wetu wapo kwenye eneo hilo la Ziwa Tanganyika. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, endapo kama zoezi hili litakuwa limekubalika na likatekelezwa, ukanda mzima wa Ziwa Tanganyika kuanzia Kasanga hadi Kigoma tutatengeneza wezi wengi na majambazi wengi, kwa sababu maisha yote ya wananchi wa ukanda wa mwambao wa Ziwa Tanganyika, yanategemea suala zima la uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuwaeleze tu ule ukweli, Serikali haijafanya utafiti mzuri. Ziwa Tanganyika ni Ziwa ambalo linajifunga lenyewe kulingana na jiografia ilivyo. Ziwa Tanganyika, muda mchache sana wanatumia wavuvi kufanya shughuli za uvuvi kwenye Ziwa hilo. Tunayo miezi ambayo Ziwa Tanganyika haliwezi kutoa hata samaki wa mboga, kwa sababu Ziwa lile lina kina kirefu na ndio Ziwa kubwa ambalo lina kina kirefu karibu mita 1500 ambazo kina chake kinaenda chini. Kwa hiyo, kuna kipindi samaki wanakwenda chini wanakimbia ubaridi wa huku juu. Kipindi hicho wavuvi huwa hawapati kitu chochote. Sasa sioni sababu Serikali inapokuja na mawazo ya kulifunga hili Ziwa kwa sababu jiografia na uhalisia ulivyo Ziwa huwa linajifunga lenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie jambo lingine la pili kwenye eneo hili la uvuvi wa Ziwa Tanganyika. Uvuvi haramu ndio chanzo cha mawazo ya kufikiria kwamba Ziwa lifungwe, lakini kuna mambo ambayo yanafanywa Serikali wanashindwa kusimamia wao wenyewe. Uvuvi haramu chanzo chake ni kuleta nyavu zile ambazo zimekatazwa na Serikali. Pia inanisikitisha sana kama nchi ya Zambia, Congo na Burundi waliafikiana kulifunga hili Ziwa wakati wao wanaruhusu nyavu hizo haramu zinauzwa bila kuwa na shida yoyote. Mfano halisi, nenda pale mpakani Tunduma, ukivuka tu upande wa pili unakuta zile nyavu zipo zinauzwa wala hazina shida ya aina yoyote, marufuku iko huku huku nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wavuvi wanaovua na nyavu hizo haramu wanatoka Nchi za DRC Congo, Burundi na Zambia. Mvuvi wa Tanzania hawezi kwenda kuvua kwenye eneo la Ziwa linalomilikiwa na Zambia wala Congo wala Burundi. Asilimia kubwa ya wavuvi wanaoendesha shughuli za uvuvi haramu ni wenzetu wa kutoka nchi za jirani. Kwa hiyo, naomba hili Mheshimiwa Waziri alielewe. Mbaya zaidi Maafisa wetu wa Serikali ambao ndio wenye jukumu la kulinda rasilimali za kwetu, wao ndio wamekuwa wahusika wakubwa wa kuwalinda na kuwahifadhi hao wanaovua kwa njia ya haramu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutamsaidia Mheshimiwa Waziri, akituhitaji na bahati nzuri tumeona kuna mwaliko ambao amewaalika Wabunge wote wa Mikoa ya Rukwa, Katavi na Kigoma. Tutamweleza uhalisia jinsi ulivyo. Maafisa wao wanatumika. Mfano, tunapopakana Mkoa wa Katavi na Mkoa wa Kigoma, kuna eneo ambalo wavuvi wa nchi zote hizo nilizokutajia hasa DRC Congo na Burundi wapo pale katikati na Maafisa wao wanakwenda kuchukua michango ambayo inawaruhusu waweze kuendeleza shughuli za uvuvi haramu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zipo zile nyavu haramu ambazo ni hatarishi kwa maisha ya viumbe hai kwenye maeneo ya Ziwa. Hizo nyavu zinatumika na Maafisa wa Wizara wanazikuta na hawachukui hatua ya aina yoyote. Kwa hiyo, sioni sababu ya Mheshimiwa Waziri kuungana na tamko ambalo wamekubaliana kwamba tulifunge hili Ziwa, kwa sababu uzembe upo Serikalini. Kwa hiyo, naomba hili Mheshimiwa Waziri alifanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri hawezi kufunga Ziwa hajaweka vitendea kazi. Uvuvi ule wa kisasa ambao ungepelekwa kwenye eneo la Ziwa Tanganyika hajawapelekea, dhana zote wamepeleka Ziwa Victoria. Kwa sababu, kule kama ni tamko la kufunga Ziwa wangepeleka kule kwa sababu walishaandaa utaratibu. Kwa Ziwa Tanganyika hawajapeleka kitu chochote kile. Kwa hiyo, naomba hili wasiende wakafanya maamuzi ambayo yatawaumiza wananchi na baadaye wakaumiza Serikali na Chama cha Mapinduzi kwa ujumla. Niombe hili walifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yapo ambayo tutaishauri Serikali, kama dhana ni kulinda rasilimali, kitu cha kwanza ambacho tunahitaji kukifanyia kazi waende wakaisimamie sheria ambayo itaondoa tatizo la uvuvi haramu. Wakaimarishe doria, wakatafute watu ambao watawasaidia ili waweze kulinda rasilimali.

Mheshimiwa Spika, la pili, ni kulinda baadhi ya maeneo ambayo yatatenga mazalia ya samaki ambayo yatakuwa yamehifadhiwa na walianzisha vizuri na kuna dalili ambayo walianza, wakaweka mpaka maboya kwenye maeneo ambayo wanaonesha kwamba maeneo haya yatakuwa ya matunzo na mazalia ya samaki. Ile ndio njia sahihi ambayo wanaweza wakasaidia hawa wavuvi. Wawapelekee sasa uvuvi na ufugaji wa samaki wa kisasa ambao wamepeleka Ziwa Victoria na Ziwa Tanganyika wawapelekee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, wapeleke zana za kisasa ambazo zinaweza zikavuna kwenye eneo la Ziwa Tanganyika. Ziwa Tanganyika ndilo Ziwa pekee ambalo wapo samaki ambao kumwona mpaka aweze kufa yeye mwenyewe ndio anapanda huku juu, kwa sababu hakuna zana za kuweza kuwavuna. Naomba hili wakalifanyie kazi kuliko yale ambayo wanaweza tu wakifika wanakubaliana mikataba ambayo itakuja kuwaumiza Watanzania na mkataba huo asilimia kubwa watakaonufaika ni nchi jirani kuliko sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema hivi kwa sababu asilimia kubwa ya wavuvi wanaokuja kuvua eneo letu ni Nchi ya Congo, Nchi ya Burundi na upande ule wa Kusini ni Zambia wanavua kwenye maeneo ya kwetu. Ukiangalia maeneo haya yote uvuvi wa kwao na maeneo wanayoyamiliki ni kidogo sana lakini ndiyo wanaovua kwa kiwango kikubwa kuzidi kwenye maeneo ya kwetu. Zambia wamewekeza, wamepeleka vifaa ambavyo vinaweza kuwasaidia wavuvi lakini kwenye maeneo mengine kama DRC Congo, Burundi wameruhusu nyavu hizo ambazo ni hatari kwetu na kwa maendeleo ya sekta ya uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunayazungumza haya ili kuepusha tafrani ambayo inaweza ikajitokeza endapo Serikali itaenda kwa mawazo ambayo wakakubaliana kitu ambacho hakitakuwa na tija kwa wananchi wetu. Mimi naamini Serikali mkijipanga vizuri mkasikiliza mawazo ya Wabunge, mnaweza mkatatua tatizo ambalo kimsingi litaleta furaha kwa wananchi ambao tunawasimamia.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Kakoso, kengele ya pili ilishagonga.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naomba Mheshimiwa Waziri ayafanyie kazi. Ahsante. (Makofi)