Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa nafasi uliyonipa ili na mimi niweze kuchangia hii Wizara muhimu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hii ya mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, kwanza ni-declare interest kwamba niliwahi kuwa Waziri wa Wizara hii tangu mwaka 2017 mpaka 2020, ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri Abdallah Hamis Ulega kwa uteuzi na kwamba mimi namwamini kwa sababu wakati ule alikuwa Msaidizi wangu, najua uwezo wake na najua kwamba atafanya kazi nzuri kwenye Wizara hii. Nakumbuka mambo mengi tuliyofanya pamoja lakini pia nawakumbuka Watumishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Upande wa sekta ya mifugo namkumbuka Dkt. Asimwe, Dkt. Furaha Mramba, Dkt. Mwambene, Dkt. Mlawa, Dkt. Shirima, Ndugu Stephen Michael pamoja na Iman Sichalwe na Ndugu Noel.

Mheshimiwa Spika, upande wa uvuvi pia nawakumbuka vizuri sana Ndugu Chama Marwa, Ndugu Madaha, Ndugu Komakoma ambaye alipima samaki hapa Bungeni, ninamkumbuka Ndugu West Mbembati, Ndugu Romani Mkenda, Ndugu Ruhasile, Ndugu Judith Mgaya, Dkt. Sweke na Dkt. Mgalila, tulifanya kazi nzuri pamoja na watumishi wengine wote wa Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi ambao tulifanya kazi nzuri, kuzunguka nchi hii karibu kila sehemu, pia tulifanya kazi hadi Saa Saba usiku wakati mwingine hata wakati mwingine tulikesha ofisini katika slogan ya masaa ni namba. Nawashukuru sana bado nakumbuka mchango wenu mkubwa katika Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipongeze sana hatua za Wizara ambazo sasa hivi wanaendelea na ujenzi wa bandari, hili ni jambo ambalo nililitamani sana lakini uwekezaji unaoendelea NARCO sasa hivi, napongeza sana ni jambo zuri, tofauti na mawazo ambayo tuliletewa mwanzo kwamba sasa inabadilishwa tena inakuwa shamba la alizeti. Hii mipango ndiyo tunayoitaka na Waziri aendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri utakumbuka kwamba Wizara iliahidi ujenzi wa mnada wa Kimataifa Mwambea na eneo lilishapatikana wataalam walishalikagua, sasa tunachokitaka ni huu mnada ujengwe, tunataka utuambie utakapokuwa una-wind up, sasa mnada huu wa Kimataifa ulioahidiwa na Serikali toka mwaka 2020 wa Mwambea unaenda kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni wapangaji katika Ranchi ya Mabale, kuna wananchi waliopanga zaidi ya vitalu 23 na walishasaini mikataba yao muda mrefu, zaidi sasa ya mwaka mzima, lakini nakala ya mikataba hiyo hadi sasa kampuni la Ranchi za Taifa (NARCO) haijawarejeshea mikataba yao tatizo ni nini? Waziri kamilisha maliza hili tatizo la migogoro ya hawa wafugaji ili waweze kupata haki yao kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu ni ukamataji holela wa mifugo. Kumekuwa na tatizo kubwa sana la ukamataji holela wa mifugo, sheria ziko wazi, Sheria ya Magonjwa ya Wanyama Na. 17 ya mwaka 2003 (The Animal Disease Act No. 2003) lakini pia na Sheria ya Ustawi wa Wanyama Na. 19 ya mwaka 2008 na Kanuni ya The Animal Welfare Impounded Animal Regulation 2020.

Mheshimiwa Spika, hizi kanuni ziko vizuri sana juu ya ukamataji wa mifugo lakini bahati mbaya sana watendaji wengi wa Serikali wamekuwa wakizivunja kanuni hizi, mambo haya yamekuwa yakijirudia. Kikubwa ni kwamba kuna maslahi makubwa juu ya ukamataji huo wa kiholela, tunasikitika kwamba kila tunapozungumza hapa Bungeni hakuna hatua zinazochukuliwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, mfano ni ukamataji holela ambao unapelekea Wanyama wanayimwa malisho, wananyimwa maji, wanayimwa dawa, wananyimwa chanjo, matokeo yake mifugo imekuwa ikifa tu ikiwa imeshikiliwa na Serikali. Tunazungumza wafugaji wa mwisho wa mwaka 2020 waliokamatiwa mifugo yao ikafa zaidi ya 6,000 mpaka leo hii wanakuja kudai hapa mifugo, wafugaji zaidi ya 12 kutoka Jimbo la Kisesa wamekuja na fimbo zao kufuata ng’ombe zao hapa Dodoma.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni ukamataji bila kushirikisha viongozi. Mifugo inakamatwa viongozi hawashirikishwi, wafugaji hawaitwi kuhakikisha mifugo yao, matokeo yake mifugo inaibiwa, mifugo inapotezwa, mifugo inauzwa kiholela. Sasa hivi tunavyozungumza kule Kilombero, DC wa Kilombero amekamata mifugo zaidi ya siku 10 sasa. Mifugo hawakuwa kwenye hifadhi zaidi ya ng’ombe 2,082, hawakuwa kwenye hifadhi lakini wameshikiliwa tu, maelezo hayatolewi, ushirikishwaji haukutolewa, mifugo wanaendelea kufa na wengine wanazidi kupotea na wengine wanazidi kuibiwa.

Mheshimiwa Spika, lingine ni mifugo kuuzwa kiholela. Mifigo inakamatwa baadae inauzwa kuholela tu kwa sababu haijahesabiwa haijulikani inauzwa kuholela. Sheria zinasema mifugo hii lazima iuzwe kwenye minada kwa bei ya ushindani na kwa uwazi, matokeo yake mifugo hii imekuwa ikiuzwa porini na Serikali inaruhusu hilo jambo kuendelaa.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilituletea hapa kuishia Disemba Serikali iliuza mifugo ng’ombe 3,828, hawa ng’ombe baada ya hapo Serikali ikauza kwa milioni 685, kwa maana ya kwamba kila ng’ombe aliuzwa kwa shilingi 180,000 wakati average ya mifugo ng’ombe mmoja ni 750,000 maana yake zinaibiwa karibu 570,000 kwa kila ng’ombe. Katika transaction hiyo tayari wale watumishi walijinufaisha zaidi ya bilioni 2.18, haya yanafanyika na Wabunge tuko hapa na Serikali iko hapa (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile wafugaji wanatozwa faini ya Shilingi 100,000 ambayo haimo kwenye Sheria ya Wanyamapori, haimo kwenye Sheria ya Misitu lakini wanaendelea kutozwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu alitoa tamko hapa la kuzuia hayo mambo kutokea, lakini mambo hayo yamekuwa yakiendelea, mimi siamini kama wale watumishi wana uwezo wa kuzuia maelekezo ya Waziri Mkuu, isipokuwa Waziri Mkuu mwenyewe anaruhusu haya mambo yafanyike na yanafanyika kwa ridhaa yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la hereni Mheshimiwa Waziri Mkuu alitoa tamko hapa la kuzuia suala …

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Mpina kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Dkt. Ndumbaro Waziri wa Katiba na Sheria.

TAARIFA

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mpina kwamba hakuna uthibitisho huo kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa ridhaa, huko ni kutumia vibaya jina la Mheshimiwa Waziri Mkuu jambo ambalo kauli ambayo siyo nzuri na siyo ya kiungwana. Jambo la pili nimpe taarifa pia kwamba….

SPIKA: Taarifa ni moja Mheshimiwa.

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Luhaga Mpina unapokea taarifa hiyo?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, sipokei taarifa yake na ninaomba niendelee. Suala la ufungaji wa hereni mifugo, Mheshimiwa Waziri Mkuu..

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, ananimalizia muda wangu naomba usipokee taarifa yoyote. (Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Mpina kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji, kati ya watu mahiri sana wanaosaidia wafugaji katika kutatua matatizo yao ni Waziri Mkuu, kwa hiyo naomba hilo jambo asiliingize kwenye mchango. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Luhaga.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, naomba niendelee na unilindie muda wangu, naweza nikaendelea pamoja na makofi haya yakiendelea.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, naombeni mkae kimya.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, suala la ufungaji wa hereni linaloendelea hivi sasa, Mheshimiwa Waziri Mkuu alitoa taarifa hapa……

(Hapa Waheshimiwa Wabunge waliendelea kupiga makofi ambayo yalisababisha Mheshimiwa Luhaga J. Mpina kushindwa kuendelea kuchangia)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge,…

MHE. LUHAGA J. MPINA: Hizo ni fujo, Mbunge huwezi kufanya mambo hayo, hizo ni fujo, waniachie muda ambao..

(Waheshimiwa Wabunge waliendelea kupiga makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Mpina subiri kwanza, umepewa taarifa na Mheshimiwa Getere unaipokea taarifa hiyo?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, siipokei taarifa naomba niendelee.

Mheshimiwa Spika, baadhi ya mambo yanayolalamikiwa katika Wizara hii, yapo mambo yanayolalamikiwa katika Wizara hii, wananchi na Wabunge lakini Wizara imekaa kimya. Mambo ambayo wakati mwingine yanaenda kupelekwa mpaka kwa Rais wa Awamu ya Tano Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, mambo ambayo yalitekelezwa kwa mujibu wa sheria, mambo hayo mfano uchomaji wa vifaranga…..

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, (SERA, BUNGE NA URATIBU): Mheshimiwa Spika, Kuhusu Utaratibu.

SPIKA: Mheshimiwa Mpina kuna Kanuni inavunjwa inaonekana. Mheshimiwa Waziri wa Nchi Kanuni inayovunjwa.

KUHUSU UTARATIBU

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Spika, Kuhusu Utaratibu Kanuni ya 71(1)(a) na Kanuni ya 75 kama nilivyoanza nayo, kinasema: “Mbunge hatatoa ndani ya Bunge taarifa ambazo hazina ukweli.” Katika ku-support Kanuni hiyo, inanipasa mimi kuthibitisha ni kwa namna gani Mbunge huyo anatoa taarifa ndani ya Bunge ambazo hazina ukweli.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mpina anamtuhumu Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba ni chanzo cha kutotekelezwa kwa utendaji bora kwenye masuala hayo ya kutetea wafugaji na kusimamia haki za wafugaji.

Mheshimiwa Spika, naomba kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba taarifa zinazotolewa na Mheshimiwa Mbunge hapa ndani hazina ukweli kwa sababu, ni juzi tu Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa kauli hapa ndani mbele ya Bunge lako kuonesha ni kwa kiasi gani Serikali, na yeye akisimamia na kutoa maelekezo kwa Serikali, namna bora ambayo Serikali itafanya kushughulikia migogoro ya wafugaji, kushughulikia migogoro ya hifadhi na kuhakikisha pia malalamiko ya Wabunge, malalamiko ya Watanzania na Maazimio ya Bunge yanafanyiwa kazi ipasavyo, ili kulinda heshima ya Serikali na heshima ya Wabunge na vile vile kujali hali na malalamiko ya Watanzania katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba utaratibu wako kama jambo hili analoendelea nalo Mheshimiwa Mbunge pamoja ya kupewa taarifa mbili amezikataa, kama ni jambo sahihi na linakubalika ndani ya Bunge lako. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, amesimama Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri wa Nchi, akionesha kwamba kuna kanuni inavunjwa wakati Mheshimiwa Mpina akichangia na ametupeleka kwenye Kanuni ya 75 ambayo inampa fursa ya yeye kusimama na kueleza ni Kanuni gani inayovunjwa na ametupeleka kwenye Kanuni ya 71(1)(a), akieleza kwamba, kanuni hiyo inakataza Wabunge kutoa taarifa ambazo hazina ukweli. Pia ameeleza kuhusu mchango wa Mheshimiwa Mpina ambao kwa yeye Mheshimiwa Jenista ameona ametoa taarifa ambazo hazina ukweli.

Waheshimiwa Wabunge, mimi nimemsikiliza Mheshimiwa Mpina, ameeleza maelekezo aliyoyatoa Mheshimiwa Waziri Mkuu huko nyuma, na kwamba hayo maelekezo aliyoyatoa Mheshimiwa Waziri Mkuu hayafuatwi katika hili eneo analochangia yeye. (Makofi)

Kwa muktadha huo, ndiyo anasema, ikiwa Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa maelekezo na hayafuatwi na wale wanaopaswa kuyafuata, basi maana yake mtoa maelekezo, yeye mwenyewe pia anaona sawa. Ndiyo mchango wake ulipo. Kwa sababu mimi nimemsikiliza kwa maneno aliyoyasema. Sasa Mheshimiwa Jenista ameomba utaratibu kwamba taarifa alizozisema hazina ukweli.

Sana sana hapo mimi nitataka kujua katika yale maelekezo ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyasema, ni kweli aliyasema hayo maelekezo ama hayapo? Kama yapo, je, yamefanyiwa kazi au Hapana? Kama hayajafanyiwa kazi, hoja ya Mheshimiwa Mpina ni kwamba, kama hayafanyiwi kazi, na yapo maelekezo, maana yake mtoa maelekezo ameona kwamba yale maelekezo yake yanaweza yakafuatwa, ama yasifuatwe. Ndiyo hoja ilipo ya kisheria kabisa kuhusu utaratibu. (Makofi)

Kwa hiyo, ndivyo mimi nilivyomsikia Mheshimiwa Mpina. Sasa kama amesikika vinginevyo, Mheshimiwa Jenista mimi nitakupa nafasi nyingine. Hicho ndicho nilichokisikia ili niweze kutoa maamuzi kuhusu utaratibu huu ulioombwa. Kama maelezo yapo tofauti na hayo niliyotoa, Mheshimiwa Jenista nakupa tena fursa, na kama sio haya, basi nitaenda kufuatilia kwenye Hansard halafu nitakuja kutoa uamuzi hapa.

Mheshimiwa Jenista nakupa nafasi nyingine.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE NA URATIBU): Mheshimiwa Spika, nadhani wote tumemsikia Mheshimiwa Mpina maelezo aliyoyatoa Bungeni. Maeneo yote ambayo Mheshimiwa Mpina anayazungumzia kwa muktadha wake yanahusu migogoro ambayo inawahusu wafugaji. Nimesimama kusema kwamba, Serikali haitekelezi ama hakuna hatua ambazo zimechukuliwa kwa namna moja ama nyingine.

Mheshimiwa Spika, nilichotaka kulithibitishia Bunge lako ni kwamba, mfano halisi ambao Serikali tunao, huku ndani na hasa katika michango ya Bunge la Bajeti lililopita na michango mingine ya Wabunge ambayo ilikuwa inazungumzwa kuhusu migogoro hii, Bunge liliiomba Serikali iunde Timu za Uchunguzi, itafute njia za kufanya na kusuluhisha migogoro yote ambayo imekuwa ikijitokeza. Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa ujumla wa hayo yote, yakiwemo hayo ambayo anayazungumza Mheshimiwa Mpina, aliyajumisha utekelezaji wake katika taarifa aliyoitoa akionesha yaliyofanywa na Serikali na maelekezo ya ziada kwa Mawaziri na Serikali kuhakikisha mambo hayo yote yanafanyiwa kazi ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaposema kwamba ama Waziri Mkuu hajasimamia, ama Serikali haijachukua hatua, ndiyo inawezekana yapo maeneo machache, lakini kwa ujumla wa maagizo ya Serikali na mwongozo ambao umekuwa ukitolewa na aliyeutoa Mheshimiwa Waziri Mkuu hapa ndani, unadhihirisha kabisa kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu mwenyewe, Serikali kwa ujumla na sekta zinazohusika zimechukulia uzito suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe taarifa kwako, tayari tumeshaelekezwa na shughuli zimeshaanza na ratiba za kushughulikia masuala hayo zilishaanza na zinaendelea. Hata weekend hii zipo ratiba ambazo zitaendelea. (Makofi)

SPIKA: Haya. Mheshimiwa Mpina maeneo mahususi ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyatolea maelekezo ili usiwe umeeleza kwa ujumla hayo mambo ili tushughulike na hayo, nitoe maamuzi juu ya jambo hili.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika,…

SPIKA: Ni maelekezo gani Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyatoa na hayajafanyiwa kazi?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, nilifurahi sana uliposema kwamba tutaenda kwenye Hansard ili kwenda kuthibitisha kile nilichokizungumza mimi. Nilisema hapa, Wabunge hapa wamezungumza wengi, nami nina ushahidi. Mheshimiwa Waziri Mkuu alisema, sasa hivi kamata kamata ya bila kushirikisha wananchi ni marufuku. Toka Agizo la Waziri Mkuu la kamata kamata ya mifugo bila kuzingatia sheria; na hii kanuni ninayoizungumza, mimi ndio nilikuwa Waziri, niliisaini mimi ya kuzuia ukamataji ovyo ovyo; watu wanakamatwa.

Mheshimiwa Spika, toka Waziri Mkuu alipotoa tamko, watu wameendelea kukamatwa, na ushahidi upo. Sasa Waheshimiwa Wabunge, Waziri Mkuu ni Mtendaji wa Shughuli za Serikali hapa Bungeni, na sisi ndio tunamthibitisha. Sasa unapotokea upungufu kama huu hatuwezi kuufumbia macho kuusema.

Mheshimiwa Spika, hata kama anavyotaka yeye kuleta, ushaidi wa matukio…

SPIKA: Mheshimiwa Mpina, tuelewane vizuri. Maelekezo ya Waziri Mkuu aliyoyatoa siku ya Alhamisi wiki iliyopita, ndiyo unayosema? Kati ya ile Alhamisi alipoyatoa mpaka sasa, kamata kamata imeendelea?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, ndiyo.

SPIKA: Hilo eneo ndilo ambalo wewe una ushahidi nalo?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, ndiyo.

SPIKA: Sawa.

Waheshimiwa Wabunge, kwa sababu, jambo hili limefika mahali ambapo linahitaji ushahidi. Sasa ili niweze kutoa huu mwongozo, kwamba yale aliyoyasema Mheshimiwa Waziri Mkuu yanafanyiwa kazi, Mheshimiwa Mpina anasema yeye anao ushahidi kwamba yale aliyoyasema Mheshimiwa Waziri Mkuu hayafanyiwi kazi.

Mheshimiwa Mpina utaniletea huo ushahidi. Kwa hiyo, hiyo hoja unaiacha ili uendelee na nyingine mpaka nitakapopata ushahidi ili nitoe mwongozo kwenye hoja hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mpina, malizia mchango wako.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, najua umenitunzia muda wangu. Sasa nilikuwa…

SPIKA: Ngoja, ngoja, tuelewane vizuri. Muda wako uliotunzwa vizuri ni ule unaohusu Utaratibu, siyo unaohusu taarifa. Kwa hiyo, usije ukaanza kudai dakika zako za Mheshimiwa Getere na za Mheshimiwa Waziri hapa. Dakika pekee unazonidai ni zile za kuhusu utaratibu ambazo nilikuwa namsikiliza Mheshimiwa Jenista hapa.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, utaniongeza kidogo tu.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nazungumzia suala la utekelezaji wa mambo yaliyotekelezwa kwa mujibu wa sheria, halafu mwisho wa siku anakuja kulaumiwa mpaka wanalaumiwa viongozi wetu wakuu. Analaumiwa Hayati Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Awamu wa Tano wa Nchi hii, mambo ambayo Wizara ya Mifugo na Uvuvi iliyatekeleza kwa mujibu wa sheria, halafu Wizara iko kimya. Waziri yuko kimya, na watendaji wa Serikali wako kimya.

Mheshimiwa Spika, suala la uchomaji wa vifaranga. Wizara ya Mifugo na Uvuvi ilichoma vifaranga 6,550 kwa mujibu wa sheria. Tunalo zuio la kuingiza mazao yote ya ndege kutoka nchi yoyote ile kutokana na nchi yetu kuwa suspected na kuenea kwa magonjwa ya mafua makali ya ndege. Tuna zuio la toka mwaka 2006, hairuhusiwi. Kosa lingine, ni kwamba huyu aliyekuwa anaingiza, hakuwa na kibali chochote kinyume cha Sheria ya Magonjwa ya Wanyama Namba 17 ya Mwaka 2003. Hana kibali chochote na haijulikani hao vifaranga wametoka wapi?

Mheshimiwa Spika, la pili, hakukuwa na cheti cha afya. Ukaguzi wowote wa kujua hao mifugo walikuwa wamechanjwa wana magonjwa gani? Hakuna kibali chochote. Sasa katika mantinki hiyo, sheria inasema, ukikutana na bidhaa za namna hiyo uzichome. Serikali ingefanya nini? Utawapeleka wapi? Hawajulikani walipotoka, hakuna kibali cha afya, hawajachanjwa, yaani Waziri au Serikali ikubali kuridhia Watanzania waje kufa na magonjwa ya mafua ya ndege hapa! Serikali ikubali kuridhia wafugaji wa Tanzania zaidi ya kuku 76,000,000 wa Watanzania, Waziri uliyeapishwa kwa mujibu wa sheria, uje uruhusu wafugaji hawa wote kuku wao wafe kwa magonjwa ya ndege kwa kumbeba mfanyabiashara mmoja, ili mfanyabiashara tu huyo wa vifaranga 6,000 aingize vifaranga vyake hapa nchini! Hayo mambo kwa nini hayazungumzwi na Wizara?

Mheshimiwa Spika, la tatu, suala la kupima samaki kwa rula Bungeni. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, nini kinachomfanya Waziri wa Mifugo na Uvuvi kutamka kwa sauti kwamba samaki anapimwa kwa urefu, na kwa urefu huo anapimwa kwa kutumia rula? Waziri wa Uvuvi anashindwa nini kusema nini kwa sauti kwamba ili uweze kukidhi matakwa ya Kanuni Namba 58 ya Kanuni ya Uvuvi ya Mwaka 2009, ni lazima umpime kwa rula ili uthibitishe vipimo kama ni sangara au sato? Anashindwa nini kufanya hivyo? (Makofi/Vicheko)

Mheshimiwa Spika, mambo haya wanazidi kutapakazwa viongozi, walipima kwa rula, walifanya hiki na kile!

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Mpina, muda wako umekwisha, ahsante sana.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, dakika moja, dakika moja tu. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba dakika moja tu. (Makofi)

SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, dakika moja.

SPIKA: Hiyo dakika ilikuwa nikupe, lakini nachelea unatukumbusha mtu anapima na rula samaki ambaye ameshapikwa, yuko tayari kwa ajili ya kuliwa! (Kicheko/Makofi)

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, nusu sekunde. Nusu dakika.