Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Mifugo na Uvuvi, kwa hotuba nzuri iliojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika utekelezaji wa ustawi wa jamii na maendeleo endelevu, na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/22 – 2025/26 ambayo ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Spika, kulingana na takwimu za mifugo na uvuvi ya mwaka wa kilimo 2022/2023 inaonesha kuwa idadi ya ng’ombe ilikuwa milioni 36.6 kutoka milioni 35.3 waliokuwepo 2021/2022. Kati ya hao, wakulima wadogo walikuwa na ng’ombe milioni 36.4 na mashamba makubwa yalikuwa na ng’ombe milioni 0.2. Aidha, wakulima wadogo walikuwa na mbuzi milioni 26.3 na mashamba makubwa mbuzi milioni 0.34.

Kwa upande wa kondoo, wakulima wadogo walikuwa na kondoo milioni 8.9 na mashamba makubwa kondoo milioni 0.24. Vilevile nguruwe waliofugwa na wakulima wadogo walikuwa milioni 3.7 na mashamba makubwa yalikuwa na nguruwe 5,123 na kulikuwa na jumla ya kuku milioni 98 ambapo wakulima wadogo walikuwa na kuku milioni 85.5 na mashamba makubwa yalikuwa na kuku milioni 12.5.

Mheshimiwa Spika, pamoja na idadi hiyo kubwa ya mifugo, mchango wa sekta ya mifugo na uvuvi wa asilimia saba bado ipo chini sana na tija ikiboreshwa kuna fursa kubwa ya sekta hii kuchangia sehemu kubwa ya pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, mifugo na uvuvi ni utajiri mkubwa, lakini pamoja na ukuaji wa asilimia tano, na Tanzania kuwa nafasi ya tatu kwa nchi za Bara la Afrika, na kuchangia asilimia saba katika uchumi wa Taifa, sekta hii ya mifugo na uvuvi inazalishwa kwa tija ndogo sana. Katika hali hii, sekta ya mifugo haijamsaidia mfugaji na mvuvi kwa kiasi kikubwa kunajinasua kwenye umaskini na kimeendelea kutoa mchango mdogo kwenye pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, Serikali ichukue hatua zaidi ili kuboresha sekta ya mifugo na uvuvi ikiwemo ujenzi wa mabwawa, kuwezesha mashamba ya kuzalisha lishe/chakula cha mifugo, kuwezesha sekta binafsi kuzalisha mitamba ya kisasa na vifaranga wa samaki. Napendekeza Serikali ianzishe vitalu vya mifugo katika Kata za Mjele na Mshewe, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, ikiwemo kuchimba mabwawa na visima.

Pia napendekeza kuwezesha kuanzisha mashamba makubwa ya kuzalisha lishe ya mifugo ikiwemo ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, nashauri Serikali imalizie kujenga Kiwanda cha Nyama cha Utengule (Mji wa Mbalizi) ambacho kwa muda mrefu ujenzi umesimama pamoja na kuwepo vifaa vyote muhimu vilivyotolewa na wafadhili. Kutokana na kuwepo uwanja wa Kimataifa wa Songwe ambao ni wa kimkakati kusafirisha mazao ya kilimo na mifugo kwa masoko ya nje, napendekeza umaliziaji wa kiwanda hiki cha nyama na pia uwezeshaji wa vitalu vya kunenepesha mifugo katika Kata za Mjele na Mshewe.

Mheshimiwa Spika, Serikali iongeze Maafisa Ugani; waliopo kwenye Halmashauri ya Mbeya ni wachache na wale waliopo hawaonekani kutoa huduma za ugani kwa wananchi. Wizara iweke msukumo wa kuhamasisha, kuanzisha na kutoa elimu kuhusu kilimo cha malisho ili kuwezesha malisho kutosheleza mifugo mwaka mzima na pia kwa soko la nje ili isaidie mapato ya fedha za kigeni.

Pia Serikali iongeze kasi ya uzalishaji wa mitamba kutokana na idadi ndogo ya ng’ombe wazazi kwenye mashamba ya Serikali na matumizi madogo ya teknolojia ya uhimilishaji kwa kutumia mbegu bora za mifugo. Kuwepo na mkakati wa kuongeza mazao ya uvuvi ikiwemo deep sea fishing ili kuwezesha samaki wapatikane kwa tija na kuwezesha ushindani kwa soko la nje. Vijana wenye nia thabiti na wanaopenda kujishughulisha na ujasiriamali wa ufugaji samaki kwenye mabwawa watambuliwe na uwekwe utaratibu maalum wa uwezeshaji kupitia Halmashauri zao kupata mitaji na utaalam wa kufuga samaki kwenye vizimba na mabwawa na hivyo kuweza kujiajiri wenyewe na kujipatia kipato. Serikali ishughulikie changamoto ya chakula cha samaki na uhaba wa

vifaranga hapa nchini. Vijengwe vitotoleshi vingi katika vituo vya ukuzaji viumbe maji.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.