Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mheshimiwa Abdallah Ulega, Naibu wake Mheshimiwa Ernest Silinde, taasisi zilizopo chini ya Wizara na wataalam wa Wizara na wadau wa sekta hizi kwa kazi nzuri wanazofanya.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyochangia mwaka jana kwenye kipindi cha bajeti, Mkoa wa Kilimanjaro una fursa nyingi za kufuga aina mbalimbali za wanyama kama vile ng’ombe na mbuzi wa maziwa na nyama, kondoo, nguruwe, sungura, kuku, bata na samaki kwa kutumia rasilimali zilizopo. Tunaiomba Serikali ipeleke teknolojia bora za ufugaji wa wanyama hawa katika Jimbo la Moshi Vijijini, kwani kwa kufanya hivyo tutaongeza tija katika uzalishaji na kuwaongezea wafugaji kipato na kulisaidia Taifa kupata fedha.

Mheshimiwa Spika, maeneo ya mlimani (Kilimanjaro) yanaweza kutumika kwa ufugaji wa ndani (zero grazing) kwa ng’ombe wachache na mbuzi wa maziwa, nguruwe, sungura, kuku na bata. Katika maeneo haya, tunaiomba Wizara ifikirie kupeleka mbegu bora za wanyama wanaofugwa na wafugaji.

Mheshimiwa Spika, eneo la ukanda wa tambarare kwenye Kata za Arusha Chini na Mabogini lina wafugaji wa Kimasai na lina uwezekano wa kuzalisha kwa tija ng’ombe, mbuzi na kondoo wa nyama.

Mheshimiwa Spika, pamoja na juhudi za wafugaji wa Jimbo la Moshi Vijijini, aina za kienyeji za wanyama (ng’ombe, mbuzi, nguruwe, kuku) wanaofugwa ni kikwazo kikubwa kwenye maendeleo ya sekta ya mifugo.

Mheshimiwa Spika, sekta ya uvuvi inaweza kuwapatia wananchi wa Jimbo la Moshi Vijijini kipato kikubwa iwapo itaendelezwa. Hili litawezekana ikiwa wananchi watapatiwa mafunzo ya kitaalamu ya jinsi ya kufuga na kukuza samaki kwa kutumia teknolojia ya mabwawa. Ufugaji endelevu wa samaki unaweza kutatua changamoto za umaskini kwa kuwaongezea kipato na kuchangia kikamilifu kwenye pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Arusha Chini kwenye Bwawa la Nyumba ya Mungu, wavuvi wanaweza kusaidiwa na Maafisa Ugani wa Uvuvi mbinu bora za ufugaji wa samaki, ikiwepo matumizi ya vizimba. Uwekezaji wa vizimba unaweza kufanyiwa majaribio kwenye Bwawa la Nyumba ya Mungu.

Mheshimiwa Spika, ili kufanikisha ufugaji wa ng’ombe na mbuzi wa maziwa na nyama, kondoo, nguruwe, sungura, kuku, bata na samaki katika Jimbo la Moshi Vijijini, ninaishauri Wizara itusaidie yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza naishauri Serikali iwe na programu maalumu ya kuzalisha mitamba wa maziwa wenye sifa zinazohitajika, ikiwa ni pamoja na mifugo mingine kama mbuzi wa maziwa, ng’ombe wa nyama, nguruwe na kuku. Wafugaji wengi hawana mbegu bora za ng’ombe na mbuzi wa maziwa. Kwa ujumla, huwa wanabahatisha.

Mheshimiwa Spika, pili, naishauri Serikali ihamasishe kuanzishwa kwa vikundi vya ushirika wa wafugaji mifugo na samaki ambavyo itakuwa rahisi kuwapatia huduma za mitaji na utaalamu.

Mheshimiwa Spika, tatu, naishauri Wizara ianzishe mashamba darasa ya samaki Jimboni Moshi Vijijini kwani kuna rasilimali nyingi za maji katika maeneo yote jimboni. Hii ni pamoja na kuanzisha kituo cha kuzalisha vifaranga wa samaki ili wafugaji wavipate kwa urahisi.

Mheshimiwa Spika, nne, naishauri Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri ya Moshi, wawezeshe kupandikiza vifaranga bora vya samaki katika Bwawa la Nyumba ya Mungu, kwani wavuvi waliniambia kwenye kampeni kuwa samaki wamehama, ikiwa na maana kuwa wamepungua.

Mheshimiwa Spika, tano, napendekeza Serikali ifanye majaribio ya kuweka vizimba kwenye Bwawa la Nyumba ya Mungu ili kuongeza tija kwenye ufugaji wa Samaki; na sita, naishauri Serikali iwekeze kwenye kujenga majosho ya kuogesha mifugo katika maeneo ya Kata za Arusha Chini na Mabogini zenye uhitaji mkubwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.