Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuungana na Watanzania wenzangu kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia baraka zake katika nyanja mbalimbali za ustawi wa kijamii, kiplomasia, kisiasa, amani na utulivu katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuungana na viongozi wenzangu wote kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali nzima ya Awamu ya Sita kwa jinsi ilivyotekeleza Ilani ya CCM ya mwaka 2020-2025.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Kamati yetu na watendaji wake wote kwenye Wizara hii kwa ujumla. Kwa kweli mambo mengi yaliyoshindikana muda mrefu yamefanyika sana katika jimbo langu, kwa mfano mradi wa ujenzi wa skimu ya umwagiliaji Tlawi Endayaya katika Halmashauri ya Mbulu Mjini ulifanyiwa usanifu toka mwaka 2003 lakini tunashukuru Serikali sasa unajengwa kwa shilingi bilioni saba.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa daraja la Gunyoda ulikuwa kilio cha wananchi wa halmashauri ya Mbulu Mjini, Karatu na Mbulu Vijijini mwaka 1998 lakini sasa imejengwa kwa shilingi bilioni 1.4.

Kuhusu ujenzi wa barabara ya lami kutoka Karatu, Mbulu Mji, Haydom, Sibiti mpaka Lalago mradi huu unaounganisha majimbo matano ya Karatu, Mbulu Mjini, Mbulu Vijijini, Mkalama na Meatu unajengwa na Kampuni ya Kichina sasa.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli kila sekta kazi kubwa sana imefanyika kwa lengo la kutatua kero za wananchi na maombi ya muda mrefu, hakika tuliadi wakati wa uchaguzi kupitia ilani yetu ya CCM na tumetekeleza.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba kutoa mchango wangu kupitia mapendekezo ya bajeti ya Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi, Serikali iangalie utaratibu wa kuongeza bajeti ya Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi kama zinavyoombwa ili tuweze kuona tija ya uzalishaji katika Wizara hii muhimu sana kwani takwimu ya mifugo tulionao ni wengi sana, lakini tija ya kiuchumi ni ndogo sana.

Mheshimiwa Spika, Serikali iangalie mpango kabambe wa mafunzo na mikopo kwa ajili ya vikundi vya wafugaji na wasindikaji wa mazao ya mifugo na uvuvi kwa lengo la kuleta mageuzi makubwa ili kuleta tija kubwa zaidi kiuchumi kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, Serikali iangalie wawekezaji wadogo watakaoanzisha ranchi ndogo ndogo na mabwawa ya kufugia samaki katika ngazi za tarafa na kata, hali hii itawabadilisha wafugaji wengi kuona umuhimu wa kufuga mifugo wachache wenye tija badala ya kuthamini idadi kubwa.

Mheshimiwa Spika, Serikali iangalie matumizi sahihi na muhimu kwenye vituo vya mafunzo na zana za kilimo zilizojengwa toka mwaka 2013 kwa kuwapeleka wataalam na kuanzisha kalenda ya mipango kazi zao kulingana na maoni ya wafugaji na wavuvi. Wizara iangalie usimamizi na uendeshaji wa majosho ya mifugo na maeneo ya minada ya mifugo uwe chini ya Maafisa Ugani wa Mifugo badala ya kuziachia Serikali za Vijiji na Mitaa kwani tunazidi kusababisha uharibifu na kupoteza ukubwa wa maeneo.

Mheshimiwa Spika, mwisho naomba Wizara itoe fedha za ujenzi wa majosho kumi katika Halmashauri ya Mbulu Mjini kwenye Kata za Tlawi, Gunyoda, Gehandu, Bargish na Marang ambayo niliomba kwenye barua yangu kwa Katibu Mkuu mwezi Februari, 2023 kupitia maelekezo ya Mheshimiwa Abdallah Ulega, Waziri wa Mifugo kwangu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja asilimia mia moja na naomba kuwasilisha.