Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nashukuru na mimi kwa kunipa nafasi. Nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, pia nitumie nafasi hii kumpongeza sana Kaka yangu, Mheshimiwa Bashe, na Naibu wake Mheshimiwa Mavunde na Wataalam wote wa Wizara ya Kilimo, kwa kazi nzuri wanazozifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoifanya. Waswahili wanasema mzigo mzito mpe Mnyamwezi, lakini mzigo mzito usimpe Mnyamwezi, mzigo mzito mpe mwanamke, anaweza kuubeba mzigo wa aina yoyote na akaufikisha ukiwa salama. Kwa hiyo, Mama yetu Samia Suluhu Hassan anaubeba mzigo mzito na umekuwa mwepesi na anaupiga mwingi, mpaka 2030 mwanamke anajikubali, anajiweza. Hongera sana Rais wetu Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite sasa kwenye hoja zangu ambazo nimeziandaa. Nianze na BBT (Building a Better Tomorrow, block farms). Nitumie nafasi hii kumpongeza sana Kaka yangu, Mheshimiwa Bashe kwa ubunifu mkubwa sana amebuni mbinu hii ambayo imeweza kuajiri vijana wengi wakiwemo wa kike na wa kiume. Mheshimiwa Bashe amebuni mtindo huu, lakini usiishie tu kwa vijana. Huu utaratibu umelenga vijana wa kike na wa kiume. Mimi ninamshauri kwamba utaratibu huu uwahusishe pia wanawake, wanaweza pia kulima. Wanawake ni wakulima wakubwa, kwa hiyo ukimuwezesha mwanamke umeliwezesha Taifa zima kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu lingine kuhusiana na hii BBT, ninaomba kwa sababu tayari utaratibu umeanza Dodoma lakini bado kuna Mikoa mingine ambayo inalima kwa uhakika, ninashauri huwezi ukamtoa kijana Mkoa wa Rukwa akaja kulima Dodoma. Kwa nini hizi block farms zisianzshwe na Mikoa mingine ikiwemo Rukwa, Ruvuma, Mbeya, Katavi na Kigoma. Huko ukiweza kuanzisha hizi block farms utaweza kupata vijana wengi ambao watajiajiri na wanawake kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie kwenye suala zima la Benki ya Kilimo. Benki hii imezungumziwa muda mrefu lakini hatuioni. Tunasikia tu benki iko Dar es Salaam, Da es Salaam ndiyo kuna mashamba? Mashamba yako mikoani? Kwa nini benki hii isiweze kuanzishwa mikoani, ikaandikwa kabisa Benki ya Kilimo, siyo mnasema kwamba eti wakulima waende kukopa kwenye mabenki mengine ambayo Benki ya Kilimo itakuwa ndani yake. Tunaomba Benki ya Kilimo ianzishwe hata kama itakuwa kwenye baadhi ya Mikoa lakini iwepo kwenye Mikoa ambayo inalima chakula kwa wingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie kwenye suala zima la mbolea. Tunaishukuru sana Serikali imeweza kuingiza pesa nyingi sana kwenye mbolea. Hapo katikati kuna kidudumtu, hawa mawakala wanachakachua, unakuta kwamba mbolea unafikiri ni urea kumbe humo ndani imechanganywa na uchafu. Wizara naomba ijipange kuhakikisha kwamba wakulima wanapata mbolea kwa wakati, mbolea ambayo ni original isiyochakachuliwa. Mimi naomba Mheshimiwa Bashe utakapokuja ku-wind up hapo atueleze amejipangaje kuhakikisha suala hili unalidhibiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mbegu bora. Wananchi wa Mkoa wa Rukwa tunapata mbegu nyingi zinatoka nchi za nje. Kwa mfano, tunatoa mbegu Zambia, sasa huwezi ukawa na uhakika mbegu imetoka Zambia huwezi kujua humo ndani wamechanganya na vitu gani. Tunaomba Serikali ianzishe mashamba ya kulima mbegu bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Mazao Mchanganyiko. Hii taasisi ni nzuri sana kwa sababu ni soko la uhakika ambalo liko ndani ya nchi. Ninaiomba Serikali iongeze mtaji kwenye Bodi ya Mazao Mchanganyiko. Pamoja na kwamba shirika hili linajiendesha kibiashara, lakini bado halijawa na uwezo wa kununua mazao mengi. Naomba Serikali iwaongezee pesa Bodi ya Mazao Mchanganyiko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii pia kumpongeza Mkurugenzi wa Bodi ya Mazao Mchanganyiko, Kaka yangu Maige, anafanya kazi nzuri. Hapo ni kuongeza mtaji tu ili Bodi hii iweze kujiendesha vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu bima ya wakulima. Nasikia tu kwamba kuna bima ya wakulima lakini hatuoni kinachoendelea imeishia wapi? Tunajua wakati mwingine kunakuwa na mabadiliko ya nchi, huwezi kujua kunaweza ikatokea mvua isinyeshe, ukame ukawepo, wadudu wakatokea, lakini bima ya wakulima ikiwepo itasaidia sana wakulima waweze kujiendesha na kukabiliana na changamoto hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni Maafisa Ugani. Kwanza ninaishukuru sana Serikali, imeweza kutoa pikipiki takribani zaidi ya 7,000 zimekwenda kwa Maafisa Ugani lakini hatuwaoni Maafisa Ugani hawa wanachakarika kwenda kuwasaidia wakulima. Wakulima wanajitegemea wenyewe, wanalima pasipo utaalam wakati tayari pikipiki zimetolewa. Tatizo ni nini? Kama tatizo ni mafuta, tunaomba Serikali iweze kuwawekea hawa Maafisa Ugani mafuta ya kwenda kufanya ziara huko kwa wakulima ili wakulima waweze kulima kilimo kilicho bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)