Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuchangia katika bajeti hii tunayoiita ni bajeti yetu, bajeti ya wakulima. Nasema ni bajeti yetu au bajeti ya wakulima kwa sababu karibia kila Mbunge hapa amezaliwa na mkulima, hata kama hujazaliwa na mkulima unakula chakula ambacho amelima mkulima. Kwa hiyo, nianze kwa kuwaomba Wabunge wote tupitishe bajeti hii kwa sababu ni bajeti yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Waziri kwa kazi nzuri anayofanya pamoja na timu yake yote. Jamani, mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni; Mheshimiwa Bashe na timu yake, Naibu wake pale, Katibu Mkuu na viongozi wote wa taasisi wanaitendea haki sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja pia kumpongeza Rais wetu kwa maono yake. Wakati ameingia madarakani bajeti yake ya kwanza ilikuwa shilingi bilioni 294, lakini kwa kuwa anajali sana wakulima akaipandisha kufikia shilingi bilioni 954 kwenye hii bajeti tunayoimalizia sasa hivi, na hiyo inayokuja amepandisha tena imekuwa shilingi bilioni 970, sawa na asilimia 2.2 ya shilingi trilioni 44.4 ya bajeti yetu ya Taifa. Kwa hiyo, tunamshukuru sana Rais kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kuomba kwamba ikiwezekana, bado bajeti hii haijakidhi matakwa ya wakulima, tunaomba iongezwe, ikiwezekana ifikie shilingi trilioni mbili ili Mheshimiwa Bashe na timu yake waweze kufanya kazi ya uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema hivyo kwa sababu wakulima ndiyo sehemu kubwa ya uchumi wetu, kama tutawawezesha, sasa hivi wanachangia 29.1 percent kwenye GDP ya nchi yetu, tukiiongeza hii bajeti najua tutaonesha maajabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miradi inayotekelezwa na Wizara ya Kilimo, fedha ambayo imetengwa kwa ajili ya miradi kwa mwaka huu ni shilingi bilioni 731 ambapo ni karibia asilimia 85 ya bajeti yote ya Wizara ya Kilimo. Kwa hiyo pesa yote kwenye ile 900, 700 na kitu iko kwenye miradi ya maendeleo ya kilimo, kwa hiyo pesa yote iko site na tunawapongeza sana Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya mwaka huu ambayo tunaiombea ni shilingi bilioni 767 kwa bajeti ya maendeleo. Kwa hiyo niwaombe ikiwezekana hii bajeti iongezeke ili hawa ndugu zetu waweze kufanya mambo ya maana. Kuna miradi ya kielelezo mingi ambayo Wizara imeshatekeleza na nitai- discuss kwa ufupi sana. Mradi wa ruzuku ya mbolea wamefanya vizuri lakini niwaombe, pamoja na kwamba mmefanya vizuri, tulishatumia karibu shilingi bilioni 342, zile changamoto za usambazaji ambazo tulikumbana nazo naomba mzi-address ili isije ikaleta shida tena. Mwaka wa kwanza ulikuwa ni wa kujifunza, tunategemea kwa kuwa zoezi bado ni endelevu, waboreshe pale ili tuweze kufanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa harakaharaka nitachangia kuhusu utafiti na uzalishaji wa mbegu kwa wakala wa mbegu. Ninaomba, mbegu ndiyo msingi wa maendeleo katika sekta ya kilimo. Watafiti na wale wazalishaji wapewe pesa ya kutosha ili tuwe na mbegu bora ambayo wakulima wataitumia kule mashambani waweze kupata tija kutokana na kilimo chetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, hapa niombe kitu ile sheria ya mbegu tunaomba iboreshwe. Kuna watu wanazalisha mbegu za asili, ile sheria inawakataza watu kuuza mbegu ambazo hazijapitia kwenye mfumo rasmi. Tunaomba ile sheria iboreshwe ili mbegu za asili kama zile za mpunga wa Kyela kama wakikidhi vigezo nao waweze kuuza hizo mbegu za asili ziwafikie walaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haraka haraka nitakwenda kwenye Tume ya Ushirika. Naishukuru Serikali imeongeza bajeti ya Tume ya Ushirika kutoka shilingi bilioni 1.1 hadi shilingi bilioni mbili sawa na ongezeko la asilimia 109. Hawa wameongezewa pesa ili kuimarisha vyama vya ushirika hapa nchini. Naomba kama Mbunge mwenzangu kutoka Kilimanjaro alivyosema asubuhi, kuna tatizo kwenye Tume ya Ushirika, kwenye vyama vya ushirika kuna matatizo makubwa sana. Nendeni mkasimamie ushirika tuhakikishe kwamba tunaboresha ushirika, wananchi wasiibiwe pesa yao kule waliko. Kuna wizi mkubwa sana unaendelea, hata kule Kilimanjario kwangu. Naomba kabisa Tume ya Ushirika iende COASCO wasimamie wahakikishe kwamba tunafanya kitu ambacho kitawapendeza wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haraka haraka naomba niongelee mambo ya jimboni kwangu. Katika Jimbo la Moshi Vijijini tuna changamoto kubwa moja. Changamoto ya kwanza kubwa kabisa ni maji ya kumwagilia. Zile skimu za umwagiliaji za asili zimeshachoka. Nami Mbunge nilivyopata pesa ya Mfuko wa Jimbo, katika kata 16, kata 14 zote nimepeleka kwenye skimu ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa namwomba Mheshimiwa Waziri, mimi pesa yangu ya Mfuko wa Jimbo nimepeleka kusaidia wakulima wapate maji. Sasa jamani ni wakati wenu na ninyi mnisaidie. Kuna skimu za asili ambazo tunaomba zijengwe, Kibosho Magharibi, kuna skimu ya Shumeli; Kibosho Mashariki, skimu ya Lyalenga, Shumbe ya Kimangara; Kaskazini, skimu ya Tumbo, Kusini skimu ya Kisarika; Mbokomu skimu ya Ondou; Kibosho Magharibi, Makeresho; Kibosho Kilima Lengurutu; na Old Moshi Skimu ya Muu. Naomba Mheshimiwa Waziri mtusaidie ili watu wapate maji tuweze kuchangia kwenye pato la Taifa. Tukishapata maji, tutazalisha kitu ambacho tunataka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine, tunaomba tujengewe skimu mpya kwenye kata ya Arusha chini ambapo kuna hekta 2000 ambazo zipo pale zinangojea zijengewe skimu na tukishapata hiyo skimu, nina uhakika tutachangia vizuri kwenye pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nihitimishe kwa kusema hivi, hapa Afrika Mashariki, Tanzania tuna mazingira mazuri sana ya ku-practice kilimo. Tuna eneo kubwa ambalo tunaweza tuka transform nchi yetu ikazalisha chakula kingi sana. Waziri leo hapa asubuhi amesema karibu hekta milioni 44 zinaweza zikatumika kuzalisha kilimo. Tumezipita nchi zote, hata Kongo tumeipita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo maziwa makuu matatu na mito mingi. Nimalizie kwa kusema, hii Wizara ya Kilimo ina wasomi wengi; ina maprofesa ina madaktari ina watu wenye masters, degree ya kwanza, diploma na certificates. Naiomba Wizara iwatumie hao wataalam vizuri. Mkiwasikiliza watachangia kwenye pato la Taifa na tutatoka kwenye ile low-income country ya Dola 1,080 na tutakwenda juu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na muda, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Naomba kuunga mkono hoja.