Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa nafasi na kuwa mchangiaji wa kwanza siku hii ya leo. Jimbo la Mbinga Vijijini, kama inavyotamkwa vijijini ni wakulima. Kwa niaba ya wakulima wote na mimi mwenyewe ni mkulima wa Mbinga, tunaishukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita kwa mpango ule wa mbolea za ruzuku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbinga bila mbolea hatuvuni. Mwaka uliotangulia kabla ya msimu huu tulipata shida sana kupata mbolea, lakini tunaishukuru Serikali, tunamshukuru Mheshimiwa Waziri, tunamshukuru Naibu Waziri, kwa mpango huu wa ruzuku ya mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu hii kupitia hizi mbolea za ruzuku kila mkulima alipata mbolea na amelima vizuri, shida ndogo tu kwamba mbolea hizi awamu hii kwa sababu ulikuwa ni mpango wa awamu ya kwanza haukufika kwa wakati, kulikuwa na ucheleweshaji wa baadhi ya mbolea. Kwa hiyo, ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri kwamba msimu huu unaokuja, najua mpango huu bado upo, nimepitia kwenye bajeti, lile lililotokea msimu uliopita basi tusilione safari hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na shida ya baadhi ya mbolea, mbolea za ya CAN na SA hazikuwa zinapatikana, kama zinapatikana basi ni kwa shida sana, ninashukuru ulinialika kwenye kikao chako cha maandalizi ya msimu ujao kupitia watu wa TFS na wale wengine wanaoagiza hizi mbolea, nimeona maandalizi yanakwenda vizuri. Hivyo, Mheshimiwa Waziri ninakuomba na ninakuamini sana, uko vizuri kwenye kupanga na kusimamia, msimu huu ile mipango niliyoishuhudia kwa watu wa TFC basi isimamie vizuri kusiwe tena na wimbi la wananchi kulalamikia baadhi ya mbolea kutopatikana ndani ya nchi yetu. Hili nina uhakika Mheshimiwa Waziri utalitekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la ushirika. Ni ukweli kabisa umoja ni nguvu, utengano ni udhaifu. Nimesikiliza baadhi ya michango jana, watu wanasema tuachane na ushirika tukaribishe mnunuzi mmoja mmoja. Kwetu Mbinga habari hiyo ya kuachana na ushirika hatuitaki, tunajua wanunuzi hawa wana nia tofauti tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna mfanyabiashara mwenye lengo la kumsaidia mkulima, hayupo. Mfanyabiashara yeyote anayefanya biashara nia yake ya kwanza ni kupata faida, kwa hiyo hatakuwa na nia ya kuwasaidia wakulima, lakini wakulima hawa wakiwa pamoja ninajua watajenga nguvu ya pamoja na watauza kwa pamoja, watauza kwa bei nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, anaweza akaja mfanyabiashara mmoja akajifanya ananunua vizuri kwa mtu mmoja rafiki yake, akapandisha bei ataenda ku-substitute kwa wakulima wengi kwa kununua bei ya chini. Kwa hiyo, najua kuna matatizo kwenye ushirika, lengo hapa liwe kuboresha siyo kwenda kubomoa kabisa na kwamba tuanze upya, hapana. Hata mimi mambo yangu hayajawa vizuri sana kwenye ushirika lakini nashukuru vyama vingi msimu huu uliopita vimelipa vizuri, vichache havijalipa, nami najua kwa nini havijalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ushirika hapa upo utaratibu wa hizi AMCOS kukopa kwenye mabenki. Hapa Mheshimiwa Waziri mimi nikushauri kwamba utaratibu huu ulisumbua sana kwenye korosho, kwamba AMCOS inakwenda kukopa halafu inakuja kuwalipa wakulima malipo ya awali, inalipa malipo ya pili na inalipa malipo kule kwenye korosho walikuwa wanaita majaliwa. Ilikuwa ni shida sana kwa wakulima hawa kulipwa malipo ya pili na yale ya majaliwa, lakini malipo ya awali kwa sababu wanakwenda kuchukua benki wanalipa, ikifika yale ya pili ni ngumu sana kulipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ninakuomba korosho sasa hivi wanalipa kwa mkupuo, mkulima akipeleka korosho zake kwenye AMCOS zikaja zikauzwa analipwa malipo yake yote, sasa hivi hakuna kelele, lakini huu mfumo wa benki kuruhusu AMCOS ikakope waje walipe mara ya kwanza, waje walipe mara ya pili, fedha zote zinaishia kulipa kwenye benki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitolee mfano Mahenge AMCOS ni chama kizuri sana lakini kimeshindwa kulipa malipo ya pili hata mkulima mmoja, milioni zaidi ya 89 wanadaiwa, hawajamlipa hata mkulima mmoja. Siyo kwamba hawana uwezo, walikusanya mazao wakauza kwa milioni 480 lakini huku nyuma kwa sababu walikopa benki milioni 500 ikabidi malipo yale yote yaingie benki na wakulima sasa hawajalipwa, wanabaki wanalalamika mpaka leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nikuombe, vyama vile ambavyo vinalipa malipo kwa mkupuo safari hii hawana kelele, lakini vyama vile ambavyo vimeenda kukopa benki halafu wakalipa malipo ya awali halafu wanakuja walipe tena malipo ya pili wengi wamepata matatizo kwa sababu kiasi wanachouza kinakwenda kuishia kulipa benki. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ninakuomba sana toa kauli vyama hivi vilipe kwa mkupuo, hatutakuwa na shida wala malalamiko kama yale waliyosema Songwe, nasi Mbinga tutakuwa na furaha zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, mwaka jana au mwaka juzi tulisherehekea hapa kwa kauli ya Waziri Mkuu ya kupunguza makato kwenye kahawa. Sasa hivi karibuni msimu huu ulioisha Mheshimiwa Waziri mmeweka makato pale ya shilingi 200 kwa kilo bila makubaliano na mkulima, ninakuomba utakapokuja hapa utoe ufafanuzi yale makato kwa nini umeyaweka, yana manufaa gani kwa mkulima na kwa nini akatwe mkulima?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kama huku tunapunguza kwa nini huku tena tunaongeza kwa njia nyingine? wakulima wangu wanalalamikia sana hilo. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri utakapokuja hapa utoe majibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, hivi kwa nini kwenye vikao hivi vya wadau wa kahawa hamuwaaliki Wabunge…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Benaya Kapinga.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: …ambao ndiyo wanapokea kero zote za wakulima?

MWENYEKITI: Ahsante sana, muda wako umekwisha.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja lakini ninaomba Waziri ujibu haya maswali niliyokuuliza hapa mwisho, ahsante sana. (Makofi)